Sports
Kikosi cha Voliboli Chipukizi Junior Wafalme Stars watinga Nusu Fainali Mashindano ya Bara Afrika
Timu ya taifa ya mpira wa voliboli ya vijana chini ya miaka 20, Junior Wafalme Stars, imefuzu kwa nusu fainali ya Mashindano ya Mataifa ya Afrika baada ya kuibuka na ushindi wa seti 3-1 dhidi ya Algeria katika robo fainali ya kusisimua iliyochezwa katika ukumbi wa ndani wa Hassan Mostafa mjini Giza, Misri, Alhamisi.
Kikosi kinachoongozwa na Luke Makuto kilianza kwa kusuasua, kikisalimu amri kwa Waafrika wa Kaskazini kwa seti ya kwanza 25-21, kabla ya kurejea kwa nguvu na kushinda seti ya pili na ya tatu 25-22 na 25-17 mtawalia.
Seti ya nne ilishuhudia Junior Wafalme Stars wakipambana kwa nguvu na kushinda 26-24, baada ya Waalgeria kulazimisha mchezo uendelee kwa matumaini ya kuipiku Kenya na kulazimisha seti ya maamuzi, juhudi ambazo ziligonga mwamba.
“Mchezo ulikuwa mgumu lakini ninafurahi vijana walipambana vikali na kushinda. Algeria pia ni timu nzuri na wametupa upinzani mkubwa,” alisema Njine.
Bethwel Kiplagat, aliyekuwa Mchezaji Bora Zaidi (MVP) wakati wa michezo ya mashule ya Jumuiya ya Shule za Upili Afrika Mashariki (FEASSSA), aliibuka shujaa wa mchezo huu na hadi sasa ameiwezesha Kenya kupata jumla ya pointi 102 zikiwemo mashambulizi 89.
Mshambuliaji huyo wa Shule ya Upili ya Cheptil alionekana mwenye furaha kubwa baada ya kutunukiwa tuzo ya MVP na kusaidia Junior Wafalme Stars kutinga nusu fainali.
“Ninafurahia sana kwa mchezo wa leo, ulikuwa mgumu lakini tuliweza. Tuna imani tunapoingia katika mechi ya kesho na tuko tayari kutoa makali yetu yote,” alisema.
Kenya sasa itamenyana na wenyeji Misri kesho katika nusu fainali ya kusisimua, ambapo nafasi ya kufika fainali itakuwa tiketi ya kufuzu kwa Mashindano ya Dunia ya 2028.
Awali, mechi hizi zilitarajiwa kutoa tiketi kwa Mashindano ya Dunia ya 2026, lakini yamefutwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Voliboli (FIVB) ili kupunguza msongamano wa mashindano.