Magoli mawili kutoka kwa Emily Moranga na Mganda Zaina Namileme yaipa Kenya Police Bullets ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya miamba wa Eritrea, DenDen FC, na kutinga nusu fainali za kufuzu kwa Ligi ya Mabingwa wa Afrika Kanda ya CECAFA.
Mechi hiyo iliyochezwa katika Uwanja wa Nyayo Jumatano alasiri ilishuhudia mabingwa wa Kenya wakichukua ushindi wao wa pili mfululizo katika hatua ya kufuzu, baada ya kuanza kampeni kwa ushindi wa 1-0 dhidi ya Kampala Queens ya Uganda Alhamisi iliyopita.
Ushindi huo sasa unaweka timu hiyo ya maafisa wa polisi kileleni mwa Kundi A wakiwa na alama 6, tatu mbele ya Kampala Queens huku DenDen wakiwa hawajapata ushindi wowote katika mechi za makundi. Kipigo hicho pia kiliwaondoa mabingwa hao wa Eritrea kwenye mashindano, baada ya kubamizwa 7-0 na Kampala Queens katika mechi yao ya ufunguzi.
Police walitarajiwa kushinda kwa mabao mengi zaidi lakini Elizabeth Ochaka alipiga shuti lililogonga mwamba dakika ya 36.
Nafasi nyingine ya moja kwa moja ilijitokeza dakika ya 50 kipindi cha pili baada ya mchezaji wa akiba Vidah Okeyo kupiga shuti la mbali lililoondolewa vyema na kipa Sofanit Gebresilasie.
DenDen walionekana kucheza mchezo wa kujilinda katika kipindi cha kwanza, lakini nafasi yao ya kufunga ilijitokeza dakika ya 62 baada ya mshambuliaji Rahwa Hans kupiga shuti lililoelekezwa langoni, lakini kipa wa Police, Annedy Kundu, alipangua kwa ustadi.
Kocha Odemba alifanya mabadiliko kadhaa kwa kuwaleta Sharon Vidah, Purity Anyetu, Rebecah Odato na Lucy Jirah, waliowachukua nafasi Margaret Kunihira, Zainab Namileme, Lourna Nyabuto na Leah Cherotich.