Sports
Nyota wa U20 Lawrence Ouma Okoth na Austine Odhiambo Waitwa Harambee Stars Kwa Mara ya Kwanza
Mshambuliaji chipukizi wa Kenya U-20 Lawrence Ouma Okoth amepokea wito wake wa kwanza katika kikosi cha timu ya taifa ya wakubwa baada ya kocha mkuu Benni McCarthy kutangaza kikosi cha Harambee Stars kitakachocheza mechi za mwisho za kufuzu Kombe la Dunia la FIFA dhidi ya Burundi na Ivory Coast.
Okoth, mshambuliaji anayechezea klabu ya ngazi ya juu nchini Finland SJK Seinäjoki, ni mmoja wa nyota waliyojumuishwa. Fowadi huyo mwenye umri wa miaka 19 anatoka katika Michael Olunga Football Academy (MOFA) na aliweka historia mapema mwaka huu kwa kuwa Mkenya wa kwanza kufunga bao kwenye AFCON U-20, akifunga kichwa cha kukumbukwa dhidi ya Morocco.
Kikosi pia kinashuhudia kurejea kwa Austin Odhiambo na Daniel Sakari, waliokosa mechi za kufuzu zilizopita dhidi ya Gambia na Shelisheli. Beki anayesakata soka Uingereza Vincent Harper pia ameitwa tena, akitafuta kucheza mechi yake ya kwanza ya kimataifa baada ya kuwa kwenye kikosi kilichocheza kirafiki dhidi ya Urusi mwaka 2023.
Orodha ya wachezaji 25 ya McCarthy imechanganya vipaji vipya na wale wazoefu waliowawezesha Kenya kufika robo fainali ya CHAN 2024, akiwemo kipa Byrne Omondi, kiungo Alpha Onyango, na mabeki Sylvester Owino na Alphonce Omija.
Kenya itasafiri kwanza kwenda Bujumbura kuvaana na Burundi mnamo Oktoba 9 katika Uwanja wa Intwari, kisha kuhitimisha kampeni yao dhidi ya Ivory Coast mnamo Oktoba 14 katika Uwanja wa Alassane Ouattara, Abidjan.
Kwa sasa Stars wako nafasi ya tano kwenye kundi lao wakiwa na pointi tisa na hawawezi tena kufuzu kwa Kombe la Dunia 2026, lakini watahitaji kuhitimisha kampeni kwa heshima. Kikosi kinatarajiwa kuingia kambini mapema Oktoba, huku safari za mwisho zikitegemea tathmini za kiafya na mazoezi ya utimamu wa mwili.
Wito kwa Okoth na Harper unaonyesha dhamira ya Benni McCarthy ya kuunganisha vipaji vya vijana na wale wa nje ya nchi katika kikosi cha wakubwa, ishara ya mwelekeo wa kujenga timu thabiti kwa mashindano ya bara na dunia yajayo.
Kikosi cha Harambee Stars
Makipa:
Faruk Shikhalo, Byrne Omondi, Brian Bwire
Mabeki:
Manzur Suleiman, Vincent Harper, Sylvester Owino, Alphonce Omija, Collins Sichenje, Michael Kibwage, Ronney Onyango, Abud Omar, Daniel Sakari
Viungo:
Alpha Onyango, Duke Abuya, Timothy Ouma, Ben Stanley, Marvin Nabwire, Austin Odhiambo
Viungo wa pembeni (Wingers):
William Lenkupae, Job Ochieng, Boniface Muchiri
Washambuliaji:
Michael Olunga, Ryan Ogam, Lawrence Okoth