Sports

Mashindano ya CHAN 2024 Yaingia Hatua Robo Fainali

Published

on

Mashindano ya TotalEnergies African Nations Championship (CHAN) 2024 yameingia hatua ya robo fainali baada ya mechi za mwisho za makundi kukamilika hapo jana kwa msisimko mkubwa.

Kwa mara ya kwanza katika historia ya CAF, mashindano makubwa yameandaliwa kwa pamoja na mataifa matatu β€” Kenya, Tanzania na Uganda β€” na yote yamefuzu robo fainali, jambo linaloendeleza hamasa kubwa ya mashindano haya barani.

Ufanisi wa wenyeji umeongeza uzito zaidi kwa kaulimbiu ya mashindano haya, β€œPamoja,” huku Afrika Mashariki ikijiandaa kushuhudia raundi nyingine ya viwanja vilivyojaa na mashabiki wenye shauku.

Kenya Yaongoza Kundi A Katika Debut;

Harambee Stars ya Kenya imekuwa moja ya simulizi kuu za mashindano, ikibatilisha matarajio kwa kufuzu robo fainali kwa mara ya kwanza katika historia yake ya CHAN na kuibuka kinara wa Kundi A.

Bao la dakika za mwisho la Ryan Ogam dhidi ya Zambia liliihakikishia Kenya ushindi wa 1-0 na kukamilisha alama 10 kileleni. Kikosi cha Benni McCarthy kimeruhusu bao moja pekee katika mechi nne, kikiashiria uimara wake wa kiulinzi.

Kenya sasa itasalia Nairobi kucheza dhidi ya Madagascar Ijumaa katika Uwanja wa Moi Kasarani. Kwa msaada wa mashabiki wa nyumbani na hali nzuri ya matokeo, Harambee Stars wamebadilika haraka kutoka wanyonge hadi kuwa tishio.

Tanzania Yatinga Robo Fainali Kwa Nguvu

Taifa Stars ya Tanzania pia iliibuka vinara wa Kundi B kwa alama 10, ikipata ushindi mara tatu na sare moja. Kikosi hiki kiliwasisimua mashabiki kwa mashambulizi makali na uthabiti, huku kiporo pekee kikiwa sare dhidi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Tanzania sasa itakutana na Morocco Ijumaa jioni jijini Dar es Salaam. Atlas Lions, mabingwa mara mbili wa CHAN, waliibuka wa pili katika Kundi A nyuma ya Kenya.

Uganda Yavunja Nuksi ya kuondolewa mapema;

Baada ya kushindwa kufuzu hatua ya mtoano mara sita mfululizo, Uganda hatimaye imepiga hatua hadi robo fainali. Sare ya mabao 3-3 dhidi ya Afrika Kusini jijini Kampala iliwatosha Cranes kuibuka vinara wa Kundi C kwa pointi saba. Penalti ya dakika za majeruhi ya Rogers Torach ilisababisha shangwe kubwa katika Uwanja wa Taifa wa Mandela.

Uganda sasa itakutana na Senegal Jumamosi usiku, mechi inayotarajiwa kuvutia umati mkubwa zaidi katika historia ya mashindano haya.

Kundi D Laamuliwa Zanzibar

Huko Zanzibar, Sudan na Senegal zilitoka sare tasa ya 0-0 na zote zikafuzu kutoka Kundi D. Sudan, ambayo haijapoteza chini ya kocha Kwesi Appiah, iliibuka kinara kwa tofauti ya mabao, huku mabingwa watetezi Senegal wakimaliza wa pili.

Sudan itasalia Zanzibar kuvaana na Algeria Jumamosi mchana, huku Senegal wakielekea Kampala kwa mtanange wao wa robo fainali dhidi ya Uganda.


Mechi za Robo Fainali

Ijumaa, 22 Agosti 2025

  • Kenya πŸ‡°πŸ‡ͺ vs Madagascar πŸ‡²πŸ‡¬ – Saa 11:00 jioni, Uwanja wa Moi Kasarani, Nairobi

  • Tanzania πŸ‡ΉπŸ‡Ώ vs Morocco πŸ‡²πŸ‡¦ – Saa 2:00 usiku, Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam

Jumamosi, 23 Agosti 2025

  • Sudan πŸ‡ΈπŸ‡© vs Algeria πŸ‡©πŸ‡Ώ – Saa 11:00 jioni, Uwanja wa Amaan, Zanzibar

  • Uganda πŸ‡ΊπŸ‡¬ vs Senegal πŸ‡ΈπŸ‡³ – Saa 2:00 usiku, Uwanja wa Taifa wa Mandela, Kampala

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Trending

Exit mobile version