Sports
Norway yatinga fainali ya kombe la dunia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1998
Taifa la Norway limefuzu Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza tangu 1998 baada ya Erling Haaland kufunga tena katika ushindi mnono wa 4-1 dhidi ya Italia siku ya Jumapili, ushindi uliowapa nafasi ya kushiriki fainali za msimu ujao zitakazofanyika Marekani, Kanada na Mexico.
Haaland alifunga bao muhimu mara mbili ndani ya sekunde chache katika Uwanja wa San Siro uliokuwa ukimwaga mvua, na Norway wakamaliza Kundi I wakiwa na alama 24 kamili kutokana na mechi zao nane za kufuzu.
Norway ingehitaji kufungwa kwa tofauti ya mabao tisa au zaidi ili kupitwa na Italia kwa nafasi ya moja kwa moja ya kufuzu, lakini kikosi cha Stale Solbakken kilimaliza kampeni yao kwa njia ya kuvutia mbele ya mashabiki 70,000.
Hata hivyo, Solbakken hakutaka kutoa ubashiri kuhusu nafasi ya kikosi chake chenye nguvu baada ya kutamatisha ukame wa miaka 28.
“Hebu tusubiri ratiba ya makundi kwanza… sijaifikiria hata. Kwangu mimi, leo ilikuwa kuanzia asilimia 99 hadi 100, na sasa tumefanikisha kwa njia nzuri,” Solbakken aliwaambia wanahabari.
“Tusubiri tuone droo italeta nini kabla ya kuingia kwenye maswali hayo.”
Baba yake Haaland, Alf-Inge, bado alikuwa mchezaji wa timu ya taifa wakati Norway ilipocheza Kombe la Dunia mara ya mwisho miaka 27 iliyopita, mashindano yaliyotwaliwa na Ufaransa ya Zinedine Zidane.
Na mshambuliaji huyo wa Manchester City—aliyeitwa “mashine ya mabao” na Solbakken—atakua mmoja wa wachezaji wa kuangaliwa Amerika Kaskazini baada ya kufunga mabao 16 katika hatua ya kufuzu.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25 ana wastani wa zaidi ya bao moja kwa kila mchezo msimu huu kwa klabu na nchi, na alikuwa mwandishi wa mabao kwa ustadi mkubwa alipopewa nafasi ya kuiweka Norway mbele kisha kuongeza bao la pili dakika ya 78 na 79.
Norway wazama Italia
Pio Esposito aliifungia Italia bao la kuongoza dakika ya 11, lakini mara tu Antonio Nusa aliposawazisha kwa shuti kali dakika ya 63, kulionekana wazi kuwa timu moja tu ingeibuka mshindi—na bao la kuvutia la Jorgen Strand Larsen dakika za nyongeza likaimaliza Italia.
Italia sasa wataelekea hatua ya mchujo mwezi Machi baada ya kumaliza kundi wakiwa nyuma ya Norway kwa alama sita na baada ya kupokea vipigo viwili vizito kutoka kwa Norway. Mashabiki wachache wa nyumbani waliobaki walipiga kelele za kuwazomea wachezaji walipotoka uwanjani San Siro.
Kocha Gennaro Gattuso aliwaomba radhi mashabiki kupitia mahojiano mafupi kwenye kituo cha RAI, na alionyesha wazi wasiwasi wake kuhusu kuporomoka kwa kikosi chake katika kipindi cha pili.
“Ni jambo linalotia wasiwasi, ningekuwa muongo nisingesema hivyo, kwa sababu unapokuwa na usiku kama huu ni rahisi zaidi kama mko pamoja na kuboresha siku hadi siku,” alisema Gattuso.
“Kinachonitia wasiwasi ni kwamba tutakutana tena baada ya miezi mitatu.”
Jitihada za Italia kufuzu moja kwa moja zilitetereka tangu mechi yao ya ufunguzi dhidi ya Norway, walipofungwa 3-0, matokeo yaliyomfanya Luciano Spalletti kuondolewa kama kocha.
Tangu Gattuso apewe timu, Azzurri wameimarika, lakini hakuna mchezaji katika kikosi chao aliye na ubora wa Haaland—jambo la kusikitisha kwa taifa lililowahi kutoa baadhi ya wachezaji bora zaidi kuwahi kutokea duniani.
Sports
Wakili George Kithi akabidhiwa rasmi Cheti cha uenyekiti wa bodi ya Michezo marufu kama Sports Arts and Social Development Fund (SASDF)
Waziri wa Wizara ya Masuala ya Vijana, Uchumi bunifu na Michezo, Salim Mvurya, ameshudia hafla rasmi ya kukabidhiwa uenyekiti wa Bodi ya Sports, Arts and Social Development Fund (SASDF) kutoka kwa Luteni Jenerali Mstaafu Jackson Tuwei kwenda kwa Mheshimiwa wakili George Kithi. Hafla hiyo ilifanyika, jijini Nairobi hii leo.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Mvurya alimpongeza Luteni Jenerali (Mstaafu) Tuwei kwa uongozi wake wa mfano na kujitolea kwake katika kipindi chake cha utumishi. Alibainisha kuwa chini ya uongozi wake, bodi hio iliimarika na kuwa taasisi imara na yenye mwitikio zaidi katika kusaidia na kuendeleza vipaji vya Wakenya.
Aidha, Waziri alieleza imani yake kwa uongozi wa Mheshimiwa wakili George Kithi, akimhakikishia ushirikiano na msaada kamili kutoka kwa Wizara katika kutekeleza majukumu ya Bodi kwa kipindi chake cha miaka mitatu.
SASDF inaendelea kuwa nguzo muhimu katika kulea na kukuza vipaji vya Kenya, pamoja na kuimarisha hadhi ya nchi kimataifa kupitia michezo na uchumi wa ubunifu. Kupitia uwezeshaji wa wanamichezo, wasanii na wadau wa utamaduni, mfuko huo unachangia pakubwa katika ukuaji wa sekta za michezo na ubunifu nchini.
Sports
Bingwa wa dunia mbio za mitaa 1500 Faith Kipyegon ateuliwa kuwania tuzo za kila mwaka za ‘Laureus World Sportswoman of the Year.’
Nyota wa mbio za masafa ya kati kutoka Kenya, Faith Kipyegon, amepata uteuzi wake wa tatu mfululizo kuwania tuzo ya Mwanamichezo Bora wa Kike wa Mwaka katika hafla maarufu ya Laureus World Sports Awards, hatua inayozidi kuthibitisha ubabe wake katika kizazi hiki cha wanariadha.
Tuzo hizo, zinazotambuliwa kimataifa kama “Oscars za Michezo”, huandaliwa na Laureus Sport for Good Foundation na hulenga kutambua mafanikio ya kipekee, uthabiti na mchango chanya wa michezo duniani.
Uteuzi wa Kipyegon kwa miaka mitatu mfululizo unaonyesha si tu kipaji chake, bali pia uimara wa kiwango chake cha juu kwa muda mrefu. Mwaka 2024 aliteuliwa baada ya msimu wa kihistoria wa 2023 ambapo alivunja rekodi tatu za dunia na kushinda dhahabu mbili katika Mashindano ya Dunia.
Mwaka 2025 alirejea tena kwenye orodha ya wateule kufuatia mafanikio makubwa katika Michezo ya Olimpiki ya Paris, ambako aliweka historia kwa kuwa mwanamke wa kwanza kushinda medali tatu za dhahabu mfululizo katika mbio za mita 1,500.
Sasa mwaka 2026, anawania tuzo hiyo tena baada ya kuvunja rekodi yake mwenyewe ya dunia ya mita 1,500 na kutwaa taji lake la nne la dunia katika msimu bora wa 2025.
Katika kinyang’anyiro cha mwaka huu, Kipyegon anakutana na ushindani mkali kutoka kwa nyota wengine wa kimataifa akiwemo Sydney McLaughlin-Levrone, Melissa Jefferson-Wooden, Aitana Bonmati, Aryna Sabalenka, na Katie Ledecky.
Uteuzi huu unaendeleza hadhi ya Kipyegon kama mmoja wa wanariadha bora zaidi duniani na fahari kubwa kwa Kenya katika jukwaa la kimataifa.

