Sports
Thunder Yaang’ara Kasarani, Yatwaa Taji la East Division Elite 16 kwa Mara ya Pili Mfululizo
Ikiwa imeungwa mkono na umati mkubwa wa mashabiki waliofurika Kasarani Indoor Arena, Nairobi City Thunder iliibwaga Johannesburg Giants ya Afrika Kusini kwa ushindi wa 94–84, na kutwaa taji la Road to BAL East Division katika fainali yenye msisimko mkubwa usiku wa Jumapili.
Ushindi huo uliihakikishia Thunder ubingwa wa pili mfululizo wa East Division Elite 16, mafanikio ya kihistoria yaliyosherehekewa na mashabiki zaidi ya 5,000 walioujaza ukumbi hadi kufikia kiwango cha juu kabisa.
Thunder na Giants zote zilikuwa tayari zimefuzu kwa Basketball Africa League (BAL) ya mwaka 2026 baada ya kufika fainali, lakini ilikuwa ni miamba wa Kenya — waliokuwa wenyeji wa mashindano kwa mwaka wa pili mfululizo — waliothibitisha ubabe wao kwenye ardhi ya nyumbani.
Thunder yapaa tangu nusu fainali
Chini ya kocha Brad Ibs, Thunder ilikuwa tayari imetia kibindoni tiketi ya BAL baada ya ushindi wa kishindo wa 109–70 dhidi ya Ferroviario de Beira ya Msumbiji katika nusu fainali.
Wakipanda juu ya kasi hiyo, waliutawala mchezo wa fainali mapema, wakichukua robo ya kwanza kwa 28–17, na kuongoza ya pili 22–21 na hivyo kwenda mapumzikoni wakiwa mbele 50–38.
Thunder waliendeleza moto wao kipindi cha tatu, wakiwazidi Giants 33–23. Hata hivyo, Afrika Kusini walijaribu kurejea mchezoni na kushinda robo ya nne 23–11, lakini uongozi wa mapema wa Thunder uliwahakikishia ushindi wa 94–84.
Ongwae na Majok waangaza, Adera aperform kivyake
Nahodha Tylor Ongwae na mchezaji wa kati Ater Majok waliiongoza Thunder kwa alama 17 kila mmoja na rebounds nne, huku Albert Odero akiongeza alama 14.
Lakini ilikuwa ni Eugene Adera aliyeng’ara kwa mchango muhimu, akivuna rebounds 12 na assists 8, akicheza jukumu muhimu sana katika ushindi wa timu katika pande zote mbili za uwanja.
Sports
Wakili George Kithi akabidhiwa rasmi Cheti cha uenyekiti wa bodi ya Michezo marufu kama Sports Arts and Social Development Fund (SASDF)
Waziri wa Wizara ya Masuala ya Vijana, Uchumi bunifu na Michezo, Salim Mvurya, ameshudia hafla rasmi ya kukabidhiwa uenyekiti wa Bodi ya Sports, Arts and Social Development Fund (SASDF) kutoka kwa Luteni Jenerali Mstaafu Jackson Tuwei kwenda kwa Mheshimiwa wakili George Kithi. Hafla hiyo ilifanyika, jijini Nairobi hii leo.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Mvurya alimpongeza Luteni Jenerali (Mstaafu) Tuwei kwa uongozi wake wa mfano na kujitolea kwake katika kipindi chake cha utumishi. Alibainisha kuwa chini ya uongozi wake, bodi hio iliimarika na kuwa taasisi imara na yenye mwitikio zaidi katika kusaidia na kuendeleza vipaji vya Wakenya.
Aidha, Waziri alieleza imani yake kwa uongozi wa Mheshimiwa wakili George Kithi, akimhakikishia ushirikiano na msaada kamili kutoka kwa Wizara katika kutekeleza majukumu ya Bodi kwa kipindi chake cha miaka mitatu.
SASDF inaendelea kuwa nguzo muhimu katika kulea na kukuza vipaji vya Kenya, pamoja na kuimarisha hadhi ya nchi kimataifa kupitia michezo na uchumi wa ubunifu. Kupitia uwezeshaji wa wanamichezo, wasanii na wadau wa utamaduni, mfuko huo unachangia pakubwa katika ukuaji wa sekta za michezo na ubunifu nchini.
Sports
Bingwa wa dunia mbio za mitaa 1500 Faith Kipyegon ateuliwa kuwania tuzo za kila mwaka za ‘Laureus World Sportswoman of the Year.’
Nyota wa mbio za masafa ya kati kutoka Kenya, Faith Kipyegon, amepata uteuzi wake wa tatu mfululizo kuwania tuzo ya Mwanamichezo Bora wa Kike wa Mwaka katika hafla maarufu ya Laureus World Sports Awards, hatua inayozidi kuthibitisha ubabe wake katika kizazi hiki cha wanariadha.
Tuzo hizo, zinazotambuliwa kimataifa kama “Oscars za Michezo”, huandaliwa na Laureus Sport for Good Foundation na hulenga kutambua mafanikio ya kipekee, uthabiti na mchango chanya wa michezo duniani.
Uteuzi wa Kipyegon kwa miaka mitatu mfululizo unaonyesha si tu kipaji chake, bali pia uimara wa kiwango chake cha juu kwa muda mrefu. Mwaka 2024 aliteuliwa baada ya msimu wa kihistoria wa 2023 ambapo alivunja rekodi tatu za dunia na kushinda dhahabu mbili katika Mashindano ya Dunia.
Mwaka 2025 alirejea tena kwenye orodha ya wateule kufuatia mafanikio makubwa katika Michezo ya Olimpiki ya Paris, ambako aliweka historia kwa kuwa mwanamke wa kwanza kushinda medali tatu za dhahabu mfululizo katika mbio za mita 1,500.
Sasa mwaka 2026, anawania tuzo hiyo tena baada ya kuvunja rekodi yake mwenyewe ya dunia ya mita 1,500 na kutwaa taji lake la nne la dunia katika msimu bora wa 2025.
Katika kinyang’anyiro cha mwaka huu, Kipyegon anakutana na ushindani mkali kutoka kwa nyota wengine wa kimataifa akiwemo Sydney McLaughlin-Levrone, Melissa Jefferson-Wooden, Aitana Bonmati, Aryna Sabalenka, na Katie Ledecky.
Uteuzi huu unaendeleza hadhi ya Kipyegon kama mmoja wa wanariadha bora zaidi duniani na fahari kubwa kwa Kenya katika jukwaa la kimataifa.

