Sports
Timu ya Taifa ya Kenya ya Para Air Badminton yashinda wenyeji Uturuki, yajikatia tiketi ya fainali
Timu ya taifa ya Kenya ya Para Air Badminton iliibuka na ushindi mnono dhidi ya Uturuki A kwa alama 3–0 katika kipengele cha Mixed Triples na pia ikaishinda Uturuki 2 katika Mixed Triples Relays wakati wa Mashindano ya Dunia ya Michezo ya Uwezo (World Ability Sports Beach Games) yanayoendelea katika ufuo wa Pompei, Mersin, Uturuki siku ya Jumatano. Ushindi huo uliihakikishia Kenya tiketi ya kucheza fainali siku ya Alhamisi na Ijumaa mtawalia.
Akizungumza baada ya mechi, kocha mkuu John Mburu alionyesha furaha kubwa kutokana na matokeo hayo, lakini alilalamikia changamoto ya ukosefu wa lugha ya kimataifa inayowaunganisha wageni.
“Waamuzi wanazungumza Kituruki, bahati nzuri mmoja wa wachezaji wetu, Nicholas Keiyo, anaelewa lugha hiyo. Hilo limetusaidia sana kufanikisha ushindi huu,” alisema Mburu, ambaye aliwateua Benson Nduva, Caleb Omollo, Mary Nduku, Patrick Mwema na Boniface Were kwa mechi ya robo fainali dhidi ya Uturuki 1, ambapo Kenya ilishinda 3–0.
Katika nusu fainali za Jumatano, Caleb Omollo, Patrick Mwema, Benson Nduva, Mary Nduku na Boniface Were waliichapa Uturuki 2 iliyokuwa na Sükrü Gül, Cemre Gül Arïn na Fuhat Soruklu, katika mchezo mkali uliomalizika kwa ushindi wa 3–0 kwa Kenya, na hivyo kufuzu fainali ya Ijumaa.
Jioni ya Jumatano, Kenya ilijiandaa kwa pambano la Mixed Triples Relays, mbio za kusisimua ambapo timu hufukuzia kufikisha alama 60, kila robo ikiwa na alama 15, na kila timu ikiwa na wachezaji sita.
Timu ya Kenya A chini ya Mburu iliwajumuisha Mary Nduku, Benson Nduva na Caleb Omollo, huku Nicholas Keiyo, Elizabeth Nabwire na Patrick Mwema wakiwa wachezaji wa akiba, walipokutana na Ali Altiparmak, Burak May, Iremnur Yazgan, Mustafa Tugra na Sedat Tumkaya wa Uturuki 1.
Kenya ilianza vizuri kwa kufungua pengo kubwa — Kenya 56 dhidi ya Uturuki 29 — lakini wenyeji wakapunguza pengo hilo, na Burak May kufunga kwa sekunde za mwisho kuwapa ushindi wa 60–59, licha ya juhudi za Patrick Mwema kuokoa mchezo huo.
Katika mchezo mwingine, Kenya B iliyoongozwa na Newton Gatobu, Japheth Kaikai, Ashley Autai, Boniface Were, Petronila Muhani na Martin Gikonyo ilipoteza 42–60 dhidi ya timu ya mchanganyiko ya Bahrain/Uturuki iliyokuwa na Ahmed Abuseter, Kerim Kíyak, Zeinab Ali, Sukru Gul na Elfi Dokuzluoglu.
Tegemeo la mwisho la Kenya lilikuwa Kenya A kurejea kwa mchezo wa lazima kushinda dhidi ya Uturuki 2. Kwa kutumia uzoefu na mbinu zake, Kocha Mburu aliwapanga nyota wake bora — Benson Nduva, Caleb Omollo na Elizabeth Nabwire — katika robo ya mwisho iliyokuwa na mvutano mkubwa hadi sekunde za mwisho. Kenya ilishinda 60–50, ikiwanyamazisha wenyeji waliokuwa wakishangilia.
Kwa ushindi huo, matumaini ya Kenya ya kupata medali katika Air Para-Badminton Mixed Triples Relays na Mixed Triples yako hai, huku timu mbili zikijihakikishia nafasi katika fainali za Alhamisi na Ijumaa.
Sports
Klabu ya Arsenal guu moja kuingia hatua ya Nusu fainali Klabu bingwa baada ya ushindi dhidi ya Sporting
Sports
Wakili George Kithi akabidhiwa rasmi Cheti cha uenyekiti wa bodi ya Michezo marufu kama Sports Arts and Social Development Fund (SASDF)
Waziri wa Wizara ya Masuala ya Vijana, Uchumi bunifu na Michezo, Salim Mvurya, ameshudia hafla rasmi ya kukabidhiwa uenyekiti wa Bodi ya Sports, Arts and Social Development Fund (SASDF) kutoka kwa Luteni Jenerali Mstaafu Jackson Tuwei kwenda kwa Mheshimiwa wakili George Kithi. Hafla hiyo ilifanyika, jijini Nairobi hii leo.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Mvurya alimpongeza Luteni Jenerali (Mstaafu) Tuwei kwa uongozi wake wa mfano na kujitolea kwake katika kipindi chake cha utumishi. Alibainisha kuwa chini ya uongozi wake, bodi hio iliimarika na kuwa taasisi imara na yenye mwitikio zaidi katika kusaidia na kuendeleza vipaji vya Wakenya.
Aidha, Waziri alieleza imani yake kwa uongozi wa Mheshimiwa wakili George Kithi, akimhakikishia ushirikiano na msaada kamili kutoka kwa Wizara katika kutekeleza majukumu ya Bodi kwa kipindi chake cha miaka mitatu.
SASDF inaendelea kuwa nguzo muhimu katika kulea na kukuza vipaji vya Kenya, pamoja na kuimarisha hadhi ya nchi kimataifa kupitia michezo na uchumi wa ubunifu. Kupitia uwezeshaji wa wanamichezo, wasanii na wadau wa utamaduni, mfuko huo unachangia pakubwa katika ukuaji wa sekta za michezo na ubunifu nchini.

