Business
Mgomo wa Tuktuk Tezo waathiri biashara
Shughuli za kibiashara katika soko la Tezo kaunti ya kilifi ziliathirika jumatatu ya Julai, 21, 2025 kufuatia mgomo wa wahudumu wa tuktuk.
Kulingana na wafanyibiashara katika soko hilo, wengi wao wanategemea huduma za tuktuk kusafirisha bidhaa zao hadi katika soko hilo.
Wakizungumza na cocofm wafanyibiashara hao waliongeza kuwa wateja wengi pia hutegemea usafiri wa tuktuk kufika sokoni humo, na kufuatia mgomo huo wengi walikosa kufika hali ambayo iliwasababishia hasara kubwa.
Aidha waliitaka sekta ya tuktuk kurejesha huduma hizo ili kuwapa afueni wafanyibiashara ikizingatiwa kuwa wanategemea biashara kujikimu kimaisha.
Mgomo huo wa wahudumu wa tuktuk uliwapa wadumu wa bodaboda mjini kilifi kaunti ya kilifi fursa ya kuvuna zaidi kimapato.
Kulingana na wanaboda wa eneo la Tezo mgomo wa wahudumu wa tuktuk uliwapelekea fursa ya kuongeza nauli kutokana na idadi kubwa ya wateja.
Kutoka eneo la Tezo hadi Chumani wahudumu hao walibeba abiria mmoja kwa shilingi 200 tofauti na shilingi 100 ya hapo awali.
Wahudumu wa tuktuk waligoma kutokana na kupanda kwa bei za mafuta aina ya petroli na dizeli, hali ambayo wanasema inasawababishia harasa kubwa.
Taarifa ya Pauline Mwango
Business
Bei za mafuta kuongezeka katikati ya mwezi aprili
Kenya sasa inakabiliwa na hatari ya kupanda kwa bei za mafuta, huku mgogoro unaoendelea mashariki ya Kati ukianza kuathiri bei nchini.
Serikali sasa imeonya kuwa kufikia katikati ya mwezi Aprili, bei za mafuta huenda zikapanda ikionya kuwa ongezeko la bei ya mafuta kwa sasa haliwezi kuepukika kufuatia kupanda kwa bei za mafuta kimataifa.
Waziri wa hazina kuu ya kitaifa John Mbadi aliwahakikishia wakenya kuwa hakuna cha kuhofia kwani wameweka mikakati kupunguza athari zake.
Ili kupunguza athari za bei za mafuta kuongezeka, serikali ilisema itatumia shilingi bilioni 17 kutoka mfuko wa ada ya uwekezaji wa mafuta kusaidia kudhibiti bei kwa mda wa miezi 3 ijayo.
Kwa sasa serikali inasema kuna akiba ya kutosha ya mafuta na shehena zaidi zinatarajiwa nchini hivi karibuni.
Taarifa ya Joseph Jira
Business
KPA yaimarisha usafirishaji wa makasha na kampeni za kimataifa
Halmashauri ya bandari nchini (KPA), imeimarisha ushirikiano wake na kampuni ya kimataifa ya usafirishaji kwa njia ya bahari, Maersk, katika juhudi za kuboresha huduma na kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo katika eneo la Afrika Mashariki.
Makubaliano hayo yameafikiwa katika mkutano uliofanyika katika makao makuu ya KPA jijini Mombasa ambapo Mkurugenzi wa Maersk Kanda ya Afrika Mashariki, Tito Okuku, alieleza kuwa kampuni hiyo ina nia ya kupanua shughuli zake zaidi nchini na katika eneo la Afrika Mashariki kwa ujumla.
Moja ya maeneo yatakayopata kipaumbele ni kuimarisha matumizi ya Kituo cha Makontena cha ndani cha Naivasha kinachotazamwa kama kitovu muhimu katika kushughulikia usafirishaji wa mazao ya kilimo kutoka Kenya kwenda masoko ya kimataifa, huku kikitoa njia ya haraka na ya kuaminika kwa wauzaji kufikia masoko ya kimataifa.
Mkurugenzi Mkuu wa KPA, Nahodha William Ruto, alieleza kukubaliana na hatua hiyo akisema ni wakati mwafaka kwa pande zote mbili kuimarisha ushirikiano huo.
Aidha alibainisha kuwa Bandari ya Mombasa pamoja na vituo vyake vya ndani vinaendelea kushuhudia ongezeko la shehena, na akahakikishia kuwa KPA iko tayari kushughulikia mahitaji yanayoongezeka kupitia maboresho ya miundombinu na huduma.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

