Business
Wahudumu wa Uchukuzi Kilifi Walia na Kupanda kwa Bei ya Mafuta
Siku moja baada ya mamlaka ya udhibiti wa kawi nchini, EPPRA kutangaza kupandishwa kwa bei ya mafuta, sekta ya uchukuzi katika kaunti ya Kilifi inaelezea hofu ya kuathirika kwa biashara zao.
Wahudumu wa tuktuk,teksi, bodaboda na magari ya usafiri wa umma hapa mjini Kilifi wanasema kupanda kwa bei ya petrol na diseli kutaathiri pakubwa sekta hiyo ya uchukuzi.
Sasa wanasema kuwa watalazimika kuongeza nauli kwa abiria kutokana na gharama ya mafuta.
Ni hali ambayo imeathiri wakaazi ambao wanatarajiwa kutumia vyombo hivyo vya usafiri wakisema kuwa watalazimika kutembea kwa mguu kwa safari fupi fupi katika utekelezaji wa shughuli zao za kawaida.
Hatahivyo wametoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwa inaingilia kati ili kuona kwamba bei za mafuta zinadhibitiwa.
Haya yamejiri huku lita moja ya mafuta aina ya petrol kaunti ya KIlifi ikiuzwa kwa shilingi 183.88 huku diseli ikiuzwa kwa shilingi 169.16 kila lita.
Lita moja ya mafuta ya taa inauzwa kwa shilingi 153.29.
Business
Bei za mafuta kuongezeka katikati ya mwezi aprili
Kenya sasa inakabiliwa na hatari ya kupanda kwa bei za mafuta, huku mgogoro unaoendelea mashariki ya Kati ukianza kuathiri bei nchini.
Serikali sasa imeonya kuwa kufikia katikati ya mwezi Aprili, bei za mafuta huenda zikapanda ikionya kuwa ongezeko la bei ya mafuta kwa sasa haliwezi kuepukika kufuatia kupanda kwa bei za mafuta kimataifa.
Waziri wa hazina kuu ya kitaifa John Mbadi aliwahakikishia wakenya kuwa hakuna cha kuhofia kwani wameweka mikakati kupunguza athari zake.
Ili kupunguza athari za bei za mafuta kuongezeka, serikali ilisema itatumia shilingi bilioni 17 kutoka mfuko wa ada ya uwekezaji wa mafuta kusaidia kudhibiti bei kwa mda wa miezi 3 ijayo.
Kwa sasa serikali inasema kuna akiba ya kutosha ya mafuta na shehena zaidi zinatarajiwa nchini hivi karibuni.
Taarifa ya Joseph Jira
Business
KPA yaimarisha usafirishaji wa makasha na kampeni za kimataifa
Halmashauri ya bandari nchini (KPA), imeimarisha ushirikiano wake na kampuni ya kimataifa ya usafirishaji kwa njia ya bahari, Maersk, katika juhudi za kuboresha huduma na kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo katika eneo la Afrika Mashariki.
Makubaliano hayo yameafikiwa katika mkutano uliofanyika katika makao makuu ya KPA jijini Mombasa ambapo Mkurugenzi wa Maersk Kanda ya Afrika Mashariki, Tito Okuku, alieleza kuwa kampuni hiyo ina nia ya kupanua shughuli zake zaidi nchini na katika eneo la Afrika Mashariki kwa ujumla.
Moja ya maeneo yatakayopata kipaumbele ni kuimarisha matumizi ya Kituo cha Makontena cha ndani cha Naivasha kinachotazamwa kama kitovu muhimu katika kushughulikia usafirishaji wa mazao ya kilimo kutoka Kenya kwenda masoko ya kimataifa, huku kikitoa njia ya haraka na ya kuaminika kwa wauzaji kufikia masoko ya kimataifa.
Mkurugenzi Mkuu wa KPA, Nahodha William Ruto, alieleza kukubaliana na hatua hiyo akisema ni wakati mwafaka kwa pande zote mbili kuimarisha ushirikiano huo.
Aidha alibainisha kuwa Bandari ya Mombasa pamoja na vituo vyake vya ndani vinaendelea kushuhudia ongezeko la shehena, na akahakikishia kuwa KPA iko tayari kushughulikia mahitaji yanayoongezeka kupitia maboresho ya miundombinu na huduma.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

