News
Bitok: Wanafunzi wa Gredi ya 9 kutumia KEMIS kujiunga na shule za Upili
Wanafunzi wa Gredi ya 9 watajiunga na shule za sekondari mwaka ujao kwa kutumia mfumo mpya wa kielektroniki wa kuwasajili wanafunzi maarufu kama KEMIS.
Kulingana na Katibu katika Wizara ya Elimu nchini Julius Bitok, Serikali imebuni mfumo huo wa kieletroniki ili kuhakikisha wanafunzi wote walioko Gredi ya 9 wanajiunga na shule za sekondari.
Bitok ametangaza kwamba wanafunzi milioni 1.2 walioko Gredi ya 9 watajiunga na Gredi ya 10 katika shule za sekondari mwakani.
Mfumo huo wa kieletroniki uliovumbuliwa wiki iliyopita jijini Nairobi utanakili wanafunzi wote nchini kuanzia shule za Chekechea, msingi, upili, taasisi za kiufundi na vyuo vikuu.
Awali Wizara hiyo ilikuwa ikitumia mfumo wa NEMIS kuchukua takwimu za wanafunzi katika shule za umma ili itume mgao wa fedha za elimu ya bure kisha baadaye ikabadili hadi KEMIS huku kamati ya bunge kuhusu elimu ikiongozwa na Mwenyekiti wake Julius Melly ikiunga mkono mfumo huo na kuitaka Wizara hiyo kuhakikisha inanakili wanafunzi wote nchini.
Bitok amesema kila mtoto atapata nafasi katika shule za sekondari licha ya kuwa na shule chache za sekondari nchini.
Kulingana na takwimu katika Wizara hiyo kuna shule elfu 10 za sekondari huku idadi ya wanafunzi ikiwa kubwa mno ikilinganishwa na shule za sekondari.
Taarifa ya Elizebeth Mwende
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

