News
Mboko: Serikali lazima ikomeshe mauaji dhidi ya Wanawake
Mbunge wa Likoni Mishi Mboko ameitaka serikali kuhakikisha inakomesha mauaji ya kiholela na unyanyasaji wa kingono dhidi ya Wanawake nchini.
Akizungumza na Wanahabari, Mishi alisema ni jambo la kusikitisha na kuhuzunisha kuona Wanawake wakiendelea kuuawa kila uchao na katika mazingira ya kutatanisha pasi na hatua zozote za kisheria kuchukuliwa dhidi ya wahusika.
Mbunge huyo aliitaka serikali kuongeza ufadhili kwa Muungano wa Wabunge Wanawake ili kuwawezesha kufanikisha kampeni ya kuhamasisha kwa umma dhidi ya ukatili wa kijinsia.
“Ni lazima visa kama hivi vikomeshwe, tumechoka na mauaji ya kila mara ya wanawake nchini na sisi pia tuko na haki ya kuishi na tunaiambia serikali kupitia bunge itenge pesa kupitia muungano wa wabunge wanawake ili kuelimisha jamii kuhusu kukomesha mauaji ya wanawake nchini”, alisema Mishi.

Mbunge wa Likoni na Wanawake wakipinga mauaji ya kiholela dhidi ya wanawake
Wakati huo huo aaliwataka maafisa wa usalama kushika doria kikamilifu hasa katika maeneo yanayokumbwa na visa vya ukatili dhidi ya wanawake huku akipendekeza mashirika yasiokuwa ya kiserikali kushirikiana na viongozi katika juhudi za kukomesha visa hivyo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

