News
Migos: Serikali imetoa shilingi bilioni 7.2 kwa Wahadhiri kusitisha mgomo
Waziri wa Elimu nchini Julius Migos amesema ana matumaini kwamba mgomo wa Wahadhiri wa vyuo vikuu vya umma kote nchini utasitishwa hivi karibu.
Waziri Migosi alisema siku ya Jumamosi na Jumapili, Maafisa wa serikali, wadau wa sekta ya elimu na viongozi wa vyama vya Wahadhiri nchini walifanya mazungumzo ya faraga katika kaunti ya Machakos na ripoti rasmi itatolewa kwa umma.
Akizungumza na Wanahabari, Waziri Migos alisema mazungumzo hayo yanatarajiwa kuibuka na suluhu na huenda wiki hii shughuli za masomo katika vyuo vikuu vya umma zikarejea kama kawaida.
Waziri Migos, alidokeza kwamba Tume ya kutathmini mishahara na marupurupu ya wafanyikazi wa umma nchini SRC imetoa shilingi bilioni 7.2 kwa Wahadhiri kama malipo ya malimbikizi ya mkataba wa makubaliano wa CBA wa mwaka wa 2017-2021.
“Serikali, wadau wa elimu na viongozi wa vyama vya wahadhiri wa vyuo vikuu nchini UASU walifanya mkutano kaunti ya Machakos kuzungumza kuhusu mgomo wa wahadhiri na tayari Tume ya SRC imetoa shilingi bilioni 7.2 kuma malipo ya malimbikizi ya mkataba wa makubaliano wa CBA wa mwaka wa 2017-2021, japo wahadhiri walikuwa wametaka shilingi bilioni 7.9”, alisema Migos.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

