Uncategorized
Rais Ruto: Usajili wa makurutu wa NYS utaongezeka hadi laki moja
Rais William Samoei Ruto amesema usajili wa makurutu watakaojiunga na huduma ya vijana kwa taifa NYS utaongezeka kutoka vijana 18,000 hadi 100,000 katika miaka mitatu ijayo.
Akizungumza katika hafla ya 89 ya kufuzu kwa makurutu wa NYS katika kambi ya Gilgil katika kaunti ya Nakuru, Rais Ruto alisema ongezeko hilo linaonyesha uimarishaji katika mafunzo na ujuzi ili kudhibiti hali ya ukosefu wa kazi miongoni mwa vijana nchini.
‘’Serikali pia imeanzisha mipango kadhaa inayolenga kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa vijana’’ alisema rais Ruto.
Rais Ruto pia alisema NYS imekuwa yenye tija katika masuala ya kama ya kilimo, uhandisi na ujenzi miongoni mwa mengine.

Makurutu wa NYS katika kambi ya Gilgil katika kaunti ya Nakuru
“Tayari inazalisha unga wa mahindi, mafuta ya kupika, na bidhaa za matunda, kupunguza gharama, na kuzalisha mapato. Hivi karibuni, NYS pia itatoa sifa zinazotambulika kitaifa na kimataifa.” aliongeza rais Ruto.
Zaidi ya makurutu 18,000 idadi ambayo ni kubwa zaidi katika historia ya NYS, baada ya kufanya mafunzo ya miezi sita rais Ruto aliagiza wizara ya mambo ya ndani kuhakikisha makurutu 4000 wanajiunga na huduma ya kitaifa kwa polisi wakati wa kuwasajili makurutu 10,000 katika usajili ujao wa maafisa wa polisi.
Waliohudhuria hafla hiyo ni Gavana wa Nakuru Susan Kihika, waziri wa utumishi wa umma nchini Geoffrey Ruku na Kamanda Mkuu wa NYS James Tembur.
Taarifa ya Janet Mumbi
Uncategorized
Mshukiwa wa mauaji kuzuiliwa rumande kwa siku 7
Mahakama ya Kilifi imeagiza kuzuiliwa rumande mshukiwa wa mauaji ya Ruth Ochieng’ mwenye umri wa miaka 60 kutoka kaunti ya Kisumu baada ya mshukiwa Evans Otieno kukamatwa katika Kanisa la Newlife Prayer Center lililoko eneo la Mavueni kaunti ya Kilifi.
Otieno alitiwa nguvuni na maafisa wa usalama alipokiri kwamba alitekeleza mauaji hayo mbele ya Mchungaji wa Kanisa hilo Ezekiel Odero, akitaka aombewe kama hatua moja wapo ya kutubu dhambi zake.
Hakimu wa Mahakama ya Kilifi Charles Obulutsa amesema Otieno atazuiliwa rumande kwa siku 7 ili kumuwezesha afisa wa polisi wa kituo cha polisi cha Seme mjini Kisumu anayechunguza kesi hiyo kufika Mahakamani.
Hakimu Obulutsa, ameeleza Mahakama kwamba wakati afisa huyo wa Polisi atakapofika katika Mahakama ya Kilifi atapewa idhini ya kumchukua mshukiwa ili afunguliwe mashtaka ya mauaji mjini Kisumu.
Awali Mahakama ilielezwa kwamba mwili wa mahehemu ulipatikana na kuthibitishwa kwamba alikuwa amenyongwa na uchunguzi zaidi ulikuwa unaendelea kabla ya mshukiwa kukamatwa katika maeneo ya Kanisa la Newlife Prayer Centre, eneo la Mavueni kaunti ya Kilifi.
Kesi hiyo itatajwa tena Februari 11 katika ili kuwakabidhi maafisa wa Polisi kutoka kaunti ya Kisumu mshtakiwa huyo.
Taarifa ya Teclar Yeri
Uncategorized
Wakenya wanaopata mshahara wa chini ya elfu 30 kuondolewa PAYE
Waziri wa Fedha nchini John Mbadi amesema serikali inalenga kuwaondolea ushuru wa PAYE wakenya wanaopata mshahara wa chini ya shilingi elfu 30 kwa mwezi huku wale wanaopata mshahara wa shilingi elfu 30 hadi laki tano wakitozwa ushuru wa asilimia 25.
Waziri Mbadi alisema hatua hiyo inalenga zaidi ya wakenya milioni 1.5 na hivi karibuni atawasilisha mswada bungeni ili pendekezo hilo liangaziwe na sheria ya ushuru ifanyiwe marekebisho kabla ya kupitishwa kwa mswada wa fedha wa mwaka wa 2026.
Waziri Mbali aliyasema hayo wakati wa kikao cha kukusanya maoni ya umma katika kaunti ya Meru ambapo alikuwa amefanya kikao cha mazungumzo na Rais William Ruto na kuafikiana kuhusu pendekezo hilo.
Waziri huyo wa fedha nchini aliongeza kwamba mswada huo pia utajumuisha pendekezo la kupunguza ushuru wa PAYE kwa asilimia 5 kwa wakenya wanaopokea mshahara wa kati ya shilingi elfu 32,050 kwa mwezi hadi shilingi laki tano, akisema punguzo hilo la asilimia 5 litasaidia wakenya kumudu gharama ya maisha.
“Tumekubaliana na Rais kwamba wananchi wenye kipato cha chini wanapaswa kupata nafuu kwenye mishahra yao kwani idadi kubwa ya wananchi wanapitia hali ngumu ya maisha na hatua hii itasaidia wakenya wengi kuwa na pesa mfukoni. Sidhani kama kuna mbunge yeyote atapinga pendekezo hilo”, alisema Mbadi.
Waziri huyo wa fedha alishikilia kwamba hatua hiyo inalenga kupunguza mzingo wa ushuru kwa wakenya wa kipato cha chini na cha kati na kuwasaidia kujikimu katika kipindi hiki cha gharama ya juu ya maisha.
Kwa sasa kikomo cha ushuru wa PAYE kinaathiri wakenya wengi wenye kupokea mshahara wa kuanzia shilingi elfu 24, akisema wataalamu wamebaini kwamba kupunguzwa kwa ushuru kutachangia matumizi ya nyumbani kuwa ya usawa na kusaidia kuimarisha uchumi unaokabiliwa na mahitaji duni.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

