News
Serikali yahimizwa kufidia wakaazi wa Owino Uhuru
Shirika la kimazingira la Center for Justice Governance and Environmental Action limetoa makataa ya siku 30 kwa serikali kutekeleza uamuzi wa Mahakama ya juu wa kulipa fidia ya shilingi bilioni 1.3 kwa jamii ya Owino Uhuru kaunti ya Mombasa.
Hii ni kufuatia uamuzi huo ambao ulitolewa zaidi ya mwaka mmoja uliopita.
Mkurugenzi mkuu wa Shirika hilo Phyllis Omido alisema ni hali ya kusikitisha kuona hadi kufikia sasa serikali haijatekeleza agizo hilo la Mahakama licha ya madhara makubwa yaliyowapata wenyeji wa eneo hilo kutokana na sumu ya Lead kutoka kwa kiwanda ambacho kilikuwa kimejengwa eneo hilo.
Omido alisema kutotengwa kwa fedha hizo katika makadirio ya nyongeza ya bajeti ya mwaka wa 2025/26 yaliyowasilishwa bungeni tarehe 3 Machi mwaka huu kunaonyeshwa kupuuzwa kwa amri hiyo ya Mahakama.
Baadhi ya watu katika kijiji cha Owino Uhuru walifariki dunia kutokana na sumu hiyo na wengine kusalia na madhara mengi ya kiafya.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Ethekon: Uchaguzi mkuu utakuwa huru, haki na uwazi
Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC imeanza rasmi zoezi la kuwasajili wapiga kura wapya kote nchini, huku ikilenga kuwasajili wapiga kura milioni 6.2, kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Mwenyekiti wa Tume hiyo Erastus Ethekon aliwahakikishia wakenya kwamba makamishna wa tume hiyo watahakikisha uchuguzi mkuu ujao unakuwa huru, haki na uwazi.
Akizungumza katika kaunti ya Kwale wakati wa kuzindua wa zoezi la usajili wa wakipiga kura kote nchini, Ethekon alisema serikali imewekeza raslimali za kutosha za kufanikisha zoezi hilo.
“Nataka kuwahakikishia wakenya kwamba tumejipanga kama IEBC na tuko na raslimali za kutosha kuhakikisha zoezi la usajili wa wapiga kura linaendeshwa vyema na uchaguzi mkuu utakuwa huru, haki na wazi ili kuhakikisha wakenya wanatekeleza jukumu lao la kidemokrasia na hatua hiyo tutafikia idadi ya wapiga kura zaidi ya milioni 27”, alisema Ethekon.
Naye Naibu Mwenyekiti wa IEBC Fahima Araphat alisema tayari maafisa wapya wa IEBC elfu 12 wameajiriwa kuhakikisha zoezi hilo liendeshwa vyema ili kusajili idadi kubwa ya wapiga kura
“Sisi tunafanya kazi yetu bila kuegemea upande wowote wa kisiasa na tuko tayari kuhakikisha anashinda uchaguzi anatangazwa mshindi kwa haki, na kama tuko na makarani elfu 12 na wote wasajili wapiga kura wapya elfu 10 kila moja tutakuwa na idadi kubwa ya wapiga kura, sasa hiyo ndio tunalenga kupata”, alisema Fahima.
Kwa upande wake Gavana wa kaunti ya Kwale Fatuma Achani, aliipongeza tume hiyo kwa zoezi hilo endelevu la wapiga kura, akisema ni hatua ya kipekee kwa jamii ambazo zimekosa fursa ya kujisajili kama wapiga kura.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
IEBC yasema idadi ya wanaojisajili ni ndogo mno
Zoezi endelevu la usajili wa wapiga kura kote nchini limeng’oa nanga huku maafisa wa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC wakilenga idadi kubwa ya vijana katika zoezi hilo.
Katika kaunti ya Kilifi eneo bunge la Kilifi Kazkazini, zoezi hilo limefanyika katika vituo vinne tofauti huku idadi ndogo ya wapiga kura ikishuhudiwa licha ya vuguvugu la TUKO KADI kuanzishwa na vijana ili kuwajisajili wapiga kura.
Akizungumza na Wanahabari wakati wa zoezi hilo, Naibu Afisa wa usajili wa wapiga kura katika eneo bunge la Kilifi Kazkazini Abdul Mohammed aliwarai vijana kujitokeza kwa wingi na kujisajili.
Mohammed pia aliwarai vijana kukoma kutumiwa vibaya na wanasiasa kwa manufaa yao binafsi, akipongeza vuguvugu lilionzishwa na vijana la TUKO KADI kama njia moja ya kuwahamasisha vijana kujisajili kama wapiga kura.
“Tumeanza zoezi hili na tunawahimiza vijana wajitokeze kwa wingi na kujisajili kama wapiga kura ili kutumia nafasi hiyo kuchagua viongozi wanawataka na wala wasikubali kutumiwa vibaya na wanasiasa”, alisema Mohammed.
Kwa upande wao baadhi ya vijana waliojisajili waliwarai vijana wenzao kujitokeza kwa wingi na kushiriki zoezi hilo ili kuchagua viongozi wanaohisi wataleta maendeleo sawa na kubuni nafasi za ajira.
Taarifa ya Elizabeth Mwende

