Entertainment
Sikutaka Pesa, Nilitaka Furaha – Bango Likaleta Vyote, Manu Bayaz
Afisa wa polisi ambaye pia ni muimbaji wa muziki wa Bango, Emmanuel Yaa Baya anayejulikana zaidi kwa jina la kisanii Manu Bayaz, amefichua kilichomsukuma kuingia kwenye muziki wa Bango.
Akihojiwa na Coco FM katika kipindi cha Coco Asubuhi, Bayaz alisema kwamba hajaanza muziki kwa ajili ya kutafuta pesa, bali alitaka kujifurahisha tu. Hata hivyo, nyimbo zake zilianza kuvutia watu wengi na kumpatia umaarufu mkubwa miongoni mwa mashabiki wa muziki wa Bango wengine wakiitisha huduma zake kwenye sherehe zao.
“Hapo awali haikuwa kwa ajili ya pesa. Nilianza kwa kujifurahisha, lakini watu wakaanza kupenda nyimbo zangu,” alisema Bayaz.
Kutokana na mafanikio hayo, Bayaz aliamua kubadili mtazamo na kuanza kuwekeza zaidi kibiashara kwenye muziki huo.
Akiendelea kuelezea safari yake ya muziki, alitaja changamoto kubwa aliyokumbana nayo kuwa ni kudhibiti kundi la wanamuziki, akisisitiza ugumu wa kuwaunganisha watu wenye malezi na mitazamo tofauti katika kundi moja.
“Kwenye bendi, kila mtu ametoka mazingira tofauti, amekuzwa kivyake. Kuwaunganisha watu kama kumi si jambo rahisi, lakini tunajitahidi,” alisema.
Bayaz analikumbuka kwa furaha tukio la malipo yake ya kwanza katika muziki wa Bango.
“Malipo yangu ya kwanza ndiyo experience nayoikumbuka maisha yangu ya mziki. Nililipwa shilingi elfu hamsini za Kenya (KSh 50,000), Mtu wa kwanza kumtaarifu habari hii ni babangu,” alisimulia.
Alieleza pia kuwa mapenzi yake ya muda mrefu kwa muziki wa Rhumba ndiyo yaliyomsukuma kuimba Bango, akieleza kuwa Bango ni aina ya Rhumba yenye ladha ya Pwani.
“Mimi napenda sana Rhumba. Nilivyoanza kuimba nikaona niende kwenye hiyo njia. Bango ni Rhumba tu, ila lina ladha ya Kipwani.”
Bayaz alianza kuimba akiwa na Sumilani Band na baadaye Ministers Band. Hata hivyo, aliachana na Sumilani baada ya kutofautiana kuhusu jina jipya alilopendekeza kwa bendi hiyo.
Bayaz pia alieleza kuwa alinunua vyombo vyake vya muziki kutoka China ili kuimarisha safari yake ya muziki, huku akiendelea kufanya kazi na bendi ya Sumilani kabla ya kuondoka.
Entertainment
Mimi Ndo Msanii Nimebaki Wengine ni Content Creators! – Hubby Africana
Msanii wa nyimbo za kizazi kipya, Hubby Africana, ameibua mjadala mpana mitandaoni baada ya kauli yake ya hivi karibuni aliyochapisha kupitia ukurasa wake wa Facebook.
Kupitia ujumbe huo, Hubby Africana alijinasibu kuwa yeye ndiye msanii halisi aliyebaki katika tasnia, akiwatuhumu wengine kwa kugeukia zaidi uundaji wa maudhui badala ya muziki.
Aliandika kwa kujiamini: “Mimi ndo msanii nimebaki🤔 hao wengine wamekua content creator😂😂 very soon mtanielewa #mnyama is coming stay tuned 🔥💯.”
Hubby Africana si jina geni kabisa pwani. Msanii huyo alishiriki kwenye makala ya kwanza ya Kilifi All Stars 2025, ambapo aliweza kumaliza katika nafasi ya saba kwa kupata kura 258. Ushiriki wake kwenye shindano hilo ulimuweka karibu zaidi na mashabiki na kumpa jukwaa la kuonesha kipaji chake.
Katika shindano hilo, aliingia na wimbo wake unaojulikana kama “Ndakukunda”, ambao ulimtambulisha rasmi kwa hadhira pana zaidi. Wimbo huo ulionyesha uwezo wake katika kuunganisha ladha ya muziki wa mapenzi na vionjo vya kisasa vinavyovutia kizazi cha sasa.
Kauli yake ya hivi karibuni inaonekana pia kuwa sehemu ya mkakati wa kujitangaza, hasa kwa kuzingatia alivyotumia kauli “#mnyama is coming.”
Je, Hubby analenga kujitofautisha na wengine na kujiweka katika daraja la kipekee? Swali kubwa linalobaki ni kama ataweza kusimama imara na kuthibitisha madai yake kupitia ubora wa kazi zake zijazo. Katika ulimwengu wa muziki, ushindani ni mkali—na mwisho wa yote, muziki mzuri ndio unaozungumza zaidi kuliko maneno. Tusubiri.
Entertainment
Live Yageuka Vita: Beka Ruga Amvaa Madundo Bila Huruma
Mtengeneza maudhui maarufu Beka Ruga amezua mjadala mkali mitandaoni baada ya kumkosoa vikali mchekeshaji Madundo wakati wa “live” aliyofanya pamoja na Bujra saa chache zilizopita.
Akijibu swali la kwa nini hajawahi kushirikiana na Madundo, Ruga hakuficha hisia zake. Alisema wazi kuwa haoni aina ya content ambayo wanaweza kufanya pamoja, akimtaja Madundo kama mtu anayependelea kuvaa nguo chafu na kukimbia mitaani kama sehemu ya burudani yake.
Kauli hiyo haikuishia hapo. Ruga aliendelea kusema kuwa kama angepewa nafasi ya kumbadilisha Madundo, angeanza kwa kumshauri aache kujipaka makaa na aanze kuzingatia usafi wake binafsi. Kwa mujibu wa Ruga, kujipaka makaa kunaweza kuwa na madhara kiafya, akihusisha hata hatari ya saratani.
Aidha, alimkosoa pia kwa kile alichokiita “kujidhalilisha” alipokuwa Tanzania, akidai kuwa Madundo alipiga picha na Gigy Money akiwa amevaa mavazi yasiyofaa hadharani.
Hata hivyo, licha ya ukosoaji huo mkali, Ruga alikanusha kuwa na bifu na Madundo. Alisema wote wanatoka eneo moja (Mkwale) na wana uwezo wa kufanya kazi nzuri pamoja—lakini akasisitiza kuwa Madundo anahitaji kubadilika ili kueleweka zaidi kwenye tasnia.
Sasa swali linabaki: je, huu ni ushauri wa kujenga au ni mashambulizi yaliyovuka mipaka?
Kwa upande mmoja, baadhi ya watu wanaona Ruga kama mtu anayesema ukweli ambao wengi wanaogopa kuusema. Kwa mwingine, wapo wanaoamini kuwa kila msanii ana mtindo wake wa kipekee, na kile kinachoonekana “cha ajabu” kwa mmoja, ndicho kinachomtofautisha na kumuinua mwingine.
Katika ulimwengu wa uundaji maudhui creation, utofauti ndio nguvu. Lakini pia, taswira na namna mtu anavyojiwasilisha vinaweza kuathiri namna anavyopokelewa na fursa anazopata.
Wewe unaonaje—Beka Ruga yuko sahihi au amevuka mipaka?

