News
Viongozi wa upinzani waendelea kuisuta serikali
Viongozi wa upinzani wameikosoa serikali kwa kukosa kutekeleza ahadi walizotoa kwa wananchi hasa katika kufufua miradi ya kiuchumi nchini.
Wakiungumza katika kaunti ya Kakamega viongozi hao wakiongozwa na kinara wa Chama cha DCP Rigathi Gachagua waliomba wakaazi kushirikiana na kuiondoa serikali katika uchaguzi mkuu ujao.
Viongozi hao walimshtumu Rais William Ruto pamoja na kinara wa chama cha ODM Raila Odinga kwa kile walichosema ni kuwatelekeza wakaazi wa ukanda wa magharibi kila msimu wa baada ya uchaguzi mkuu.
“Nyinyi mnampatia kura anatoa fujo, anaitwa, anaingia kwa serikali anawaacha nyinyi kwa mataa, sasa mimi nimefukuza Ruto kule kwa mlima, nimefunga mlima kifunguo iko hapa kwa gari”,alisema Gachagua.
Kwa upande wake kinara wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alieleza matumaini ya ushirikiano wao na Gachagua, akisema wanaamini wakipata uungwaji mkono wa wananchi wanambandua rais Ruto mamlakani.
Viongozi hao wanasema serikali imeshindwa kudhibiti taifa hasa kupunguza gharama ya maisha na kutimiza ahadi ya miradi ya maendeleo ya kufaidi mahasla.
“Sisi tumekosana na William Ruto kwa sababu ule mkataba ambao tuliandishana naye kama watui wa mkoa wa magharibi amekataa”,alisema Cleophas Malala.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

