News
Wakaazi wa wakosoa kauli ya Rais Ruto dhidi ya viongozi wa kidini
Baadhi ya wakaazi kutoka kaunti ya Mombasa wamepinga matamshi ya Rais William Ruto kuwa viongozi wa kidini wamekuwa mstari wa mbele kuwachochea vijana dhidi ya serikali ya Kenya Kwanza.
Kulingana na wakaazi, vijana wa kizazi cha Gen-z wamechukua hatua ya kuandaa maandamano ya mara kwa mara, kukemea vitendo viovu kupitia mitandao ya kijamii kutokana na hali ngumu ya maisha na ukosefu wa uwajibikaji miongoni mwa viongozi wakuu serikalini na wala sio viongozi wa kidini wamewachochea.
Wakaazi hao wamemtaka Rais Ruto kukubali kukosolewa na viongozi wa kidini kwani viongozi hao wamekua wakitekeleza wajibu wao wa kuikosoa serikali kwa njia ya Amani.
“Kusema kweli ni kama Rais hataki kukosolewa kwa sababu hawa viongozi wanafanya kazi yao na wamekua wakifanya hivyo hata kwa serikali zilizopita na kama wewe mtu hutaki kukosolewa itakuwaje?” … aliuliza mmoja wa wakaazi.
Wakaazi hao aidha wameshikilia kuwa kando na viongozi wa kidini wao pia kama wananchi wana haki ya kuikosoa serikali kwani ni jukumu lao kikatiba huku wakiapa kutonyamazia madhila yanayotekelezwa na viongozi.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

