News
Achani, Aagiza wizara 10 zilizogatuliwa kupeana kandarasi kwa Vijana
Gavana wa kaunti ya Kwale Fatuma Achani ameagiza wizara 10 zilizogatuliwa katika serikali za kaunti kupeana kandarasi za kutekeleza miradi ya maendeleo kwa makundi ya akinamama na vijana katika kaunti hiyo ili kukabiliana na suala la ukosefu wa ajira na kupunguza viwango vya umaskini.
Kulingana na Gavana Achani, kufikia sasa jumla ya kampuni 300 za akina mama na vijana zimesajiliwa huku kampuni 105 zikipewa kandarasi za ujenzi wa zahanati, shule za Chekechea, upanuzi wa mabomba ya maji miongoni mwa kandarasi zengine.
Gavana Achani alisema hatua hiyo itasaidia wakaazi wa Kwale kujiajiri na kupunguza viwango vya umaskini.
“Nilisema akina mama na vijana waunde kampeni ili tuweze kujiajiri kwani hali ya uchumi kwa sasa hivi ni mbaya kwani saa hizi pale serikali ya kaunti imefikishwa haiwezi kuajiri na ni lazima tutafute njia mbadala za ni vipi watu watawezepata nafasi za ajira”, alisema Achani.

Kwa upande wake Katibu wa Wizara ya Huduma za Jamii na Ukuzaji Talanta katika serikali ya kaunti ya Kwale Riziki Mwasoza alisema kuwa wamekuwa wakiwapa mafunzo kina mama na vijana waliosajili kampuni na kuwajimiza kutumia kampuni hizo kusaka zabuni katika mashirika ya kibinafsi.
“Kama idara mwaka uliopita tuliwafanyia mafunzo akinamama na vijana ya siku tatu ili kujua jinsi ya kusimamia mapato yao”, alisema Mwasoza.
Nao wakaazi ambao wanamiliki kampuni na waliofaidika na kandarasi za serikali ya Kwale wakiongozwa na Mathew Kailu kutoka Shimbahills alieleza kwamba tangu wasajili kampuni hizo wamepata zabuni za hadi shilingi milioni 9 zinazowapa faida kubwa na kufanya miradi mbali mbali ya kuwajimu kimaisha.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

