Sports
Haller Ajiunga Rasmi na Utrecht Baada ya Kuondoka Borussia Dortmund
Kilabu ya Borussia Dortmund ya Ujerumani imethibitisha kwamba mshambuliaji wa taifa la Ivory Coast Sebastien Haller amejiunga na klabu ya Uholanzi, Utrecht, kwa mkataba wa kudumu.
Inaripotiwa kuwa Haller amejiunga kwa uhamisho wa bure baada ya kuruhusiwa kuvunja mkataba wake na Dortmund mwaka mmoja kabla ya muda wake kuisha.
Raia huyo wa taifa la Ivory Coast mwenye umri wa miaka 31 alitumikia nusu ya pili ya msimu uliopita kwa mkopo Utrecht, klabu aliyowahi kuichezea kati ya mwaka 2015 na 2017. Kuondoka kwake kunahitimisha kipindi kigumu akiwa Dortmund.
Baada ya kusajiliwa kwa dau la euro milioni 31 ($36m) kutoka Ajax mwaka 2022, Haller aligunduliwa kuwa na saratani ya korodani wiki chache baadaye na akakaa nje kwa miezi sita akipokea matibabu.
Alikosa penalti katika siku ya mwisho ya msimu wa 2022-23 kwenye sare ya 2-2 nyumbani dhidi ya Mainz, matokeo yaliyoiwezesha Bayern Munich kutwaa ubingwa wa Bundesliga.
Hata hivyo, mshambuliaji huyo wa zamani wa West Ham na Eintracht Frankfurt ndiye aliyefunga bao la ushindi kwa Ivory Coast katika fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka jana dhidi ya Nigeria.
Entertainment
Arsenal Ikishinda Kombe Nitampa Main Man Rio Gari na Dadangu – Shuga Boy
Mjadala mkali umeibuka katika kipindi cha COCO Asubuhi baada ya Shuga Boy, shabiki wa Manchester United, kuweka dau zito na la kushangaza dhidi ya Main Man Rio ambaye ni shabiki wa Arsenal.
Akizungumza kwenye kipindi cha COCO Asubuhi, kinachoendeshwa na Tatu Sure—inayojumuisha Shuga Boy mwenyewe, Main Man Rio na Solomon Zully—Shuga Boy alifunguka, akidai kuwa Arsenal hawana uwezo wa kubeba hata kombe moja msimu huu licha ya matarajio makubwa kutoka kwa mashabiki wao.
Kwa mujibu wa Shuga Boy, mashabiki wa Arsenal wamekuwa wakijipa matumaini makubwa ya kutwaa hadi vikombe vinne, lakini hali halisi uwanjani haioneshi dalili hizo. Alienda mbali zaidi na kuweka dau la kipekee kwa Main Man Rio, ambaye ni shabiki mkubwa wa Arsenal.
“Nilimwambia Main Man Rio, wakibeba kombe nitampa gari yangu. Sasa naongeza dau—wakishinda kikombe msimu huu, nitampa gari yangu pamoja na dadangu,” alisema Shuga Boy kwa msisitizo, kauli iliyozua kicheko na mjadala mkali studio.
Kauli hiyo imekuja katika kipindi ambacho Arsenal wamekuwa wakionyesha ushindani mkubwa chini ya kocha Mikel Arteta, wakijijenga kama moja ya timu zinazowania ubingwa wa Premier League. Licha ya maendeleo hayo, ukosefu wa vikombe katika misimu mingi bado unawapa wapinzani wao nafasi ya kuwabeza.
Kwa upande mwingine, Manchester United nao wanapitia kipindi cha mabadiliko, wakijaribu kurejea kwenye ubora wao wa zamani waliouonyesha enzi za Sir Alex Ferguson. Licha ya changamoto, bado wana historia nzito ya mafanikio, jambo linalowapa mashabiki wao kujiamini wanapojadili soka la Uingereza.
Usiku wa leo, macho ya mashabiki yataelekezwa kwenye mchezo wa ligi kati ya Manchester United dhidi ya Leeds United—mchezo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkali, huku Shuga Boy akitumaini timu yake itapata ushindi na kuendeleza presha kwa wapinzani wao.
Wakati mabishano yakiendelea mitandaoni na kwenye studio za redio, swali kubwa linabaki: Je, Arsenal wataweza kuwanyamazisha wakosoaji wao kwa kubeba angalau kombe moja msimu huu, au kauli ya Shuga Boy itageuka kuwa unabii?

