News
Wakaazi watishia kuandamana kufuatia uhaba wa maji Kilifi
Wakaazi wa kaunti ya Kilifi wametishia kuandamana hadi katika ofisi za Gavana wa kaunti ya Kilifi Gideon Mung’aro kufuatia uhaba maji uliyodumu kwa takribani mwezi mmoja katika baadhi ya maeneo ya kaunti hiyo.
Wakaazi hao wakiongozwa na Kiongozi wa kidini wa Kanisa la Kibaptist kanda ya Pwani Rev. Francis Katana, walisema suala la maji ni muhimu kwa jamii za kaunti ya Kilifi na kwamba serikali ya kaunti inafaa kulichukuliwa kwa uzito suala hilo na kulitatua.
Katana anasema idadi kubwa ya wakaazi hasa wa mji wa Malindi wamekuwa wakipitia changamoto hiyo kwa mda mrefu na hata baada ya kuwasilisha lalama zao kwa idara husika ikiwemo ofisi za Kampuni ya usambazaji maji ya Malindi, MAWASCO, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa kukabiliana na changamoto hiyo.
Kiongozi huyo wa kidini alisisitiza kwamba maandamano hayo yatafanywa kwa kuzingatia amani na kwamba wakaazi watatembea hadi katika ofisi za Gavana Mung’aro ili kuwasilisha lalama zao.
“Tumechoka na hii shida ya uhaba wa maji iliyodumu kwa mwezi mmoja sasa na tutafanya maandamano hadi kwa ofisi za Gavana ili atueleza shida iko wapi, mbona wakaazi tunahangaika na uhaba wa maji”, alisema Rev. Katana.
Viongozi hao wa kidini pamoja na wakaazi wamelalamikia kutoangaziwa kwa maslahi yao licha ya kuwasilisha lalama kwa viongozi na wawakilishi wa maeneo yao, wakisema wakati umefika sasa kwa viongozi kuwajibika ama wananchi watatumia mamlaka yao ya kidemokrasia kuwatimua kazini.
Kwa upande wake Mwanasiasa Peter Ziro aliitaka serikali ya kaunti ya Kilifi kutatua changamoto hiyo mara moja ili kuwapungumzia mahangaiko wakaazi hao, akisema serikali ya kaunti iko na raslimali za kutosha za kuzikabili changamoto zinazowakumba wananchi mashinani.
“Tunashangaa na serikali hii ya Gavana Mung’aro, yani suala la maji ambalo ni uhai kwa wananchi waliyomchagua analichukulia kama jambo la mzaa, watu wanahitaji maji kwa matumizi ya kinyumbani na tukiendelea hivi basi tutateseka. Viongozi waliopewa jukumu la kushughulia maslahi ya wananchi ni lazima wawajibike kikamilifu”, alisema Ziro.
Akijubu lalama hizo zilizoibuliwa na wakaazi hao, Mkurugenzi wa Kampuni ya usambazaji maji ya Malindi, (MAWASCO) Felix Wanje alikiri kuwepo kwa changamoto hiyo, akisema ilichangiwa na kukatwa kwa nguvu za umeme kutokana na deni la umeme ambalo bado halijalipwa.
“Changamoto kweli ipo na hiyo shida tunaishughulikia na wananchi watapata maji hivi karibuni. Tatizo hilo lilichangiwa na kukatwa kwa nguvu za umeme kutokana na deni ambalo bado tunadaiwa lakini tunalishughulikia suala hilo”, alieleza Wanje.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
EACC yafaulu kurejesha shilingi bilioni 7.8 zilizoporwa.
Tume ya maadili na kupambana na ufisadi EACC imesema imefaulu kurejesha shilingi bilioni 7.8 zilizoporwa.
EACC kwenye taarifa yake kwa vyombo vya habari, imeeleza kwamba fedha hizo zinajumuisha mali na raslimali za umma zilizopowa na baadhi ya wakenya wasiojali maslahi ya wengine na maendeleo ya taifa.
Tume hiyo ambayo ilitikwa jukumu la kukabili ufisadi na kuendeleza uadilifu kwa maafisa wa umma, mashirika na taasisi imekuwa ikifuatilia sakata mbalimbali za ubadhirifu wa mali ya umma ambao mara nyingi umekuw ukitekelezwa na baadhi ya wakenya ikiwemo viongozi wa kisiasa na maafisa wa idara mbalimbali za kiserikali.
Tume hiyo ya EACC ilifafanua kwamba kumekuwa na ongezeko la visa vya uporaji wa mali ya umma, ikisisitiza kwamba maafisa wa Tume hiyo wako makini kuhakikisha ufisadi nchini unakomeshwa.
Afisa mkuu mtendaji wa EACC Abdi Ahmed Mohamud, alisema kwamba viwango vya ufisadi nchini vingali juu na makachero wa EACC wamefanikiwa kukabiliana na visa vya ufisadi kwa asilimia 72 katika kipindi cha miaka miwili iliyopita.
Mohamud aliongeza kuwa tume hiyo imefanikiwa kurejesha shilingi bilioni 7.8 zilizokuwa zimeporwa katika kipindi cha miaka miwili, huku akiahidi kwamba mikakati zaidi imeekezwa kuhakikisha ufisadi unakomeshwa nchini.
“Juhudi tulizoweka katika kukabiliana na ufisadi nchini zimefaulu lakini kuna haja ya ushirikiano na washikadau
Wakati huo huo alieleza wasiwasi wake kuhusu kiwango cha hasara kilichorekodiwa katika miaka ya hivi karibuni akifichua kuwa takriban shilingi bilioni 10.74 zilipotea kupitia ufisadi katika kipindi chab miaka miwili pekee iliyopita.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Waziri Wandayi asema hatajiuzulu
Waziri wa Kawi nchini Opiyo Wandayi ameweka wazi kwamba hatajiuzulu licha ya shinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi wa kisiasa na mashirika ya kijamii, kumtaka ajiuzulu.
Wandayi alisema haoni sababu za kuchukua uamuzi huo kwani hausiki kivyovyote na sakata ya uagizaji wa mafuta ghushi, akisema uchunguzi unaendelea kuhusu suala hilo.
Akijubu maswali yalioulizwa na wabunge mbele ya kamati ya Kawi katika bunge la kitaifa, inayoongozwa na David Gikaria, Waziri hiyo alisema hadi kufikia sasa hajajua kiini kilichowashinikiza maafisa watatu katika wizara yake waliohusisha na sakata hiyo kujiuzulu.
Wandayi alithibitisha kwamba Idara ya Mafuta chini ya Wizara ya Kawi nchini iliomba msamaha wa vigezo fulani kutoka kwa Shirika la ukadiriaji wa bidhaa nchini (KEBS) kupitia barua za tarehe 26 na 27 Machi 2026. Msamaha huo ulitolewa baadaye na Wizara ya Biashara na Viwanda nchini inayoongozwa na Lee Kinyanjui kuridhinia msamaha huo tarehe 28 Machi 2026.
Aidha alifichua kwamba Kamati ya uratibu wa Meli (VAC) ilibaini mnamo tarehe 18 Machi 2026 kuwa meli iliyokuwa imepangwa ilikuwa imepakia mizigo katika bandari ya Jebel Ali lakini haikuweza kupita katika Mlango wa Bahari wa Hormuz, hali iliyozua hofu ya uwezekano wa pengo la usambazaji wa mafuta.
Ilibainika kwamba kauli ya mashirika mbalimbali iliyopendekeza mzigo wa dharura uliwasilishwa kwa Katibu wa Wizxara ya Kawi na mafuta nchini Mohammed Liban kuidhinisha.
Waziri Wandayi hata hivyo alipoulizwa ni wapi hasa usambazaji wa mafuta ulikwama, aliwaelekeza wabunge kwa taratibu za ndani za Kampuni ya usambazaji mafuta (KPC), akisema kuwa kampuni hiyo ilipokea ripoti ya bandari ya kupakia mizigo tarehe 27 Machi ili kuhakikisha inazingatia viwango vinavyohitajika.
Wakati huo huo alidokeza kwamba hakuna na ufahamu kwamba sakata hiyo ilikuwa kinyume na mpango wa uagizaji wa mafuta wa serikali kwa serikali yani G to G, akisema hatua hiyo ndio iliyopelekea kuanzishwa kwa ucnguzi na maafisa wa DCI.

