Business
Serikali yachukua hatua za haraka kupunguza bei za mafuta
Mamlaka ya kudhibiti bei ya mafuta nchini EPRA imetangaza kupunguzwa kwa bei ya mafuta ya Petroli, Dizeli na Taa humu nchini.
Kaimu Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka hiyo Mhandisi Joseph Oketch katika taarifa aliyoitoa, ametangaza kupunguzwa kwa bei ya mafuta ya petroli kwa shilngi 9.37, mafuta ya Dizeli kwa shilingi 10.21 huku bei ya mafuta ya Taa ikisalia kama kawaida.
Oketch amesema hatua hiyo ni baada ya Hazina ya kitaifa kupunguza ushuru wa mafuta kwa asilimia 8 kutoka asilimia 13 ili kuchangia kupungua kwa gharama ya ununuzi wa mafuta baada serikali kutenga shilingi bilioni 6.5 za ruzuka ya mafuta.
Hatua hii imejiri mda mchache tu baada ya Mamlaka hiyo awali kutangaza bei ya mafuta ya Petroli kupanda kwa shilingi 28 kwa lita na mafuta ya Dizeli yakipanda kwa shilingi 40 kwa lita, hatua iliyosababisha viongozi wa upinzani kutishia kuitisha maandamano ya kitaifa kushinikiza kupunguzwa kwa bei hizo za mafuta nchini.
Hata hivyo katika taarifa ya Mamlaka ya EPRA, ilisema mafuta ya Petroli sasa yatauzwa kwa shilingi 197.60 kwa lita, huku mafuta ya Dizeli yakiungwa kwa shilingi 196.63 kwa lita na mafuta ya Taa yakisalia shilingi 152.78 kwa lita, katika jiji la Nairobi.
Mjini Mombasa, bei ya mafuta ya Petroli sasa itauzwa kwa shilingi 194.32, mafuta ya Dizeli yakiuzwa kwa shilingi 193.35 huku mafuta ya Taa yakiuzwa kwa shilingi 149.49 kwa lita na mjini Kilifi bei hiyo ya mafuta ikipungua na mafuta ya Petroli sasa yatauzwa kwa shilingi 195.18, mafuta ya Dizeli yakiuzwa kwa shilingi 194.22 huku mafuta ya Taa yakiuzwa kwa shilingi 150.36 kwa lita.
Hata hivyo Mamlaka hiyo imesema tangazo hilo limezingatia notisi ya kisheria nambari 70 na kwamba bei hiyo mpya ya mafuta inaanza kutekelezwa mara moja na itadumu kwa kipindi cha mwezi mmoja hadi tarehe 14 mwezi Mei mwaka huu.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
Business
Wafanyibiashara wa mitumba eneo la Diani wafunga biashara zao
Wafanyibiashara wa mitumba katika soko la Diani, kaunti ya Kwale, wamelazimika kufunga biashara zao kutokana na kudorora kwa shughuli za kibiashara katika kipindi hiki cha msimu wa watalii wachache na mvua zinazoendelea kushuhudiwa katika eneo hilo.
Wafanyabiashara hao wanasema idadi ya wanunuzi imepungua kwa kiasi kikubwa, hali iliyosababisha nguo nyingi kukosa soko.
Kulingana na wafanyibiashara hao wanategemea zaidi watalii wa ndani na nje na kutokana na msimu huu kuwa uko uko chini wateja wamepungua hali inayofanya maisha kuwa mgumu.
Wanasema wamelazimika kutupa baadhi ya nguo kwani zimesalia sokoni kwa muda mrefu hadi zingingine kuharibika, jambo ambalo limepelekea kupata hasara kubwa.
Aidha, wameongeza kuwa bei ya nguo za mitumba imeendelea kupanda ambapo wananunua ngunia moja kwa shilingi elfu 40 huku mauzo yakizidi kushuka.
“ Biashara imedorora sai kwani hakuna wateja ikizingatiwa kuwa tunategemea sana watalii na sasa hakuna wageni hata imetulazimu kutupa nguo kwani ngigi zimeharibika baada ya kukaa kwa mda mrefu bila kununuliwa”.
Taarifa ya Pauline Mwango
Business
Mamlaka ya AFA yahimiza upanzi wa mkorosho
Mamlaka ya Kilimo na Chakula nchini AFA, imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha taifa linaboresha mazao yake na kuchangia uzalishaji wa chakula nchini.
Hatua hii imechangia zaidi na mikakati endelevu ya kuwawezesha wakulima kufahamu mipango endelevu ya uimarishaji wa Kilimo cha sasa na kwa kuzingatia utumiaji wa mifumo bora ya kilimo.
Mamlaka hiyo ambapo inaendeleza kampeni ya kuhamisha wakulima kuhusu umuhimu wa kilimo cha Korosho imesisitiza haja ya ujumuishaji wa wakulima, wawekezaji na wadau mbalimbali ili kupiga jeki sekta ya Kilimo huku ikiahidi kuendeleza hamasa kwa jamii za kaunti za Pwani kuhusu kilimo cha korosho na utafutaji wa soko huru.
Katika Kongamano la kitaifa lililoandaliwa katika kaunti ya Kwale, Mamlaka hiyo iliwapa wakulima kutoka kaunti sita za Pwani miche ya mikorosho elfu mia moja katika juhudi za kukuza kilimo cha zao hilo nchini.
Katibu katika Idara ya Kilimo nchini Paul Kiprono, alisema mpango huo unalenga kuwawezesha wakulima kuongeza uzalishaji wa korosho na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kongamano hilo, Kiprono alitoa wito kwa serikali za kaunti pamoja na wadau wa sekta ya kilimo kushirikiana kwa karibu ili kuboresha kilimo cha korosho.
“Kenya ilikuwa ikiongoza katika zao la mkorosho katika miaka ya 1990 lakini kutokana na changamoto za kibiashara zao hilo lilishuka katika masoko ya kimataifa kutokana na ukosefu wa kuwekezaji kwa wakulima lakini sasa tumeanza kupiga hatua kwani tunazalisha zaidi ya tan elfu 9 za korosho”, alisema Rono.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa AFA, Cornelly Serem, alisema mamlaka hiyo imejizatiti kuboresha kilimo cha korosho kupitia utoaji wa miche bora na mafunzo kwa wakulima ili kuongeza tija.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

