National News
Chonga: Wakenya Wanaosafiri Ughaibuni Kusaka Ajira Hawazingatii Sheria za Leba
Mwenyekiti wa kamati ya Leba katika bunge la kitaifa Ken Chonga amesema baadhi ya wakenya ambao wanasafiri katika mataifa ya miliki za kiarabu kusaka ajira wamekosa kuzingatia sheria za Wizara ya Leba nchini na kuangukia mikononi mwa walaghai.
Chonga amesema ni lazima wakenya hao wachunguze mawakala wanaowasafirisha katika mataifa hayo kama wanatambulika na serikali, ndipo waingie katika mikataba ya uajiri ambayo imezingatia sheria za Leba nchini.
Akizungumza na Wanahabari mjini Kilifi, Chonga ambaye pia ni Mbunge wa Kilifi Kusini amesema ili wakenya waepuke madhila mbalimbali kutoka kwa waajiri wao katika mataifa hayo ni lazima wasafirishwe na mawakala waliosajiliwa na serikali.
Wakati huo huo amesema japo serikali iko mbioni kuhakikisha inawatafutia wakenya kazi katika mataifa ya ughaibuni ni lazima wanaosaka ajira za ughaibuni waingie katika mkataba wa uajiri kabla ya kusafiri nje ya nchi.
National News
Umoja wa mataifa wapunguza bajeti yake kwa bola milioni 577
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amependekeza kupunguzwa kwa bajeti ya umoja huo ya mwaka ujao kwa dola milioni 577, hatua ambayo itapunguza asilimia 18 ya kazi.
Akizungumza mbele ya kamati ya bajeti ya Baraza kuu la umoja wa mataifa, Guterres alisema umoja huo bado haujapokea mchango wa karibu dola milioni 900 kutoka kwa wanachama mwaka huu wa 2025.
Umoja wa mataifa unapendekeza bajeti ya dola bilioni 3 kwa mwaka 2026, ikiwa na upungufu wa asilimia 15 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka huu.
Umoja wa Mataifa unakabiliwa na mgogoro wa kifedha uliosababishwa pakubwa na hatua ya Marekani kutolipa ada yake, kutokana na sera mpya za Rais Donald Trump.
Hatua hii ya umoja wa mataifa huenda ukachangia changamoto kubwa kwa mataifa wanachama hasa yanayotegemea pakubwa juhudi za umoja huo katika masuala mbalimbali ikiwemo usalama.
Editor's Picks
Bangi Yanaswa Daraja la Sabaki – Malindi, Kaunti ya Kilifi
Maafisa wa Usalama wamenasa shehena ya Bangi katika daraja la Sabaki, Mjini Malindi Kaunti ya Kilifi, iliyokuwa imefichwa kwenye makasha ndani ya basi lililokuwa likisafiri kitoka Lamu kwenda Mombasa.
Basi hilo lilisimamishwa na Maafisa wa usalama katika kizuizi Cha Polisi kilichoko daraja hilo kwa shughuli ya kawaida ya ukaguzi wa magari na mizigo, ambapo magunia mawili ya bangi hiyo yalipatikana yamefichwa katika sehemu ya Mizigo ndani ya basi hilo.
Dereva na Kondakta wa basi hilo, mali ya kampuni ya mabasi ya Tawakal, walikamatwa, ingawa abiria anayeaminika ndiye mwenye kusafirisha bangi hiyo alitotoka mtego huo na bado anatafutwa na Maafisa Polisi.
Waliokamatwa sasa wanazuiliwa katika kituo cha Polisi cha Mjini Malindi huku uchunguzi zaidi unapoendelea.
Maafisa hao wanasema, walipata vidokezo kuhusiana na bangi hiyo ambayo bado haijajulikana thamani yake.
Katika siku za hivi karibuni, Daraja hilo la Sabaki limekuwa chini ya oparesheni kali ya maafisa wa usalama kutokana kuongezeka Kwa idadi ya vyombo vya usafiri, hasa Malori ambayo yaaminika kutumika kwa zaidi kwa biashara haramu kutoka Kaunti za Tana River na Lamu kuingia Kaunti za Kilifi na Mombasa.
Dereva huyo na Kondakta wake watafikishwa mahakamani hivi karibuni huku maafisa wa Polisi wakitia wito kwa wanachi kutoa habari zitakazosaidia kumtia nguvuni mshukiwa mkuu.

