Business
KPA inamatumaini bandari ya Mombasa kuimarika zaidi
Mkurugenzi mkuu wa halmashauri ya bandari nchini, nahodha William Ruto, ameibua matumaini mapya kuhusu uboreshaji wa Bandari ya Mombasa baada ya kutangaza hatua mbalimbali za kisasa zinazolenga kuongeza ufanisi wa shughuli za bandari.
Akizungumza kwenye kikao na viongozi wa chama cha mawakala wa forodha nchini (KIFWA), nahodha Ruto alisema KPA imeanza kutekeleza miradi muhimu kama kudhibiti kina cha bahari kwa ajili ya kupokea meli kubwa, ujenzi wa Gati ya kwanza katika eneo la Dongo Kundu, pamoja na uendelezaji wa Gati 19B ili kupanua uwezo wa bandari ya Mombasa kushughulikia mizigo zaidi.
Alieleza kuwa KPA pia imewekeza kwenye mitambo ya kisasa yenye ufanisi wa nishati, ikiwemo kreni za ‘rubber-tyred gantry’, hatua ambayo itapunguza muda wa meli kukaa bandarini na kuongeza kasi ya kazi.
Katika hatua nyingine, Ruto alisema utekelezaji wa mifumo ya kiotomatiki utaongeza kasi ya huduma hususan kwenye lango la bandari, akibainisha kuwa mageuzi ya kidijitali ndiyo dira ya kufanikisha shughuli za bandari kwa viwango vya kimataifa.
Pia alisisitiza umuhimu wa bandari ya Lamu, akisema kituo hicho kinazidi kuimarika kama nguzo muhimu ya mradi wa LAPSSET, huku akialika viongozi wa KIFWA kufanya ziara ya kujifunza kwenye bandari hiyo.
Kwa upande wake, mwenyekiti wa KIFWA kanda ya Pwani, Rajab Hamisi, aliwapongeza wanachama kwa kazi yao thabiti, na kuishukuru KPA kwa kuendeleza ushirikiano unaolenga kuongeza ushindani na ufanisi katika sekta ya usafirishaji.
Taarifa Mwanahabari wetu.
Business
KPA yaimarisha usafirishaji wa makasha na kampeni za kimataifa
Halmashauri ya bandari nchini (KPA), imeimarisha ushirikiano wake na kampuni ya kimataifa ya usafirishaji kwa njia ya bahari, Maersk, katika juhudi za kuboresha huduma na kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo katika eneo la Afrika Mashariki.
Makubaliano hayo yameafikiwa katika mkutano uliofanyika katika makao makuu ya KPA jijini Mombasa ambapo Mkurugenzi wa Maersk Kanda ya Afrika Mashariki, Tito Okuku, alieleza kuwa kampuni hiyo ina nia ya kupanua shughuli zake zaidi nchini na katika eneo la Afrika Mashariki kwa ujumla.
Moja ya maeneo yatakayopata kipaumbele ni kuimarisha matumizi ya Kituo cha Makontena cha ndani cha Naivasha kinachotazamwa kama kitovu muhimu katika kushughulikia usafirishaji wa mazao ya kilimo kutoka Kenya kwenda masoko ya kimataifa, huku kikitoa njia ya haraka na ya kuaminika kwa wauzaji kufikia masoko ya kimataifa.
Mkurugenzi Mkuu wa KPA, Nahodha William Ruto, alieleza kukubaliana na hatua hiyo akisema ni wakati mwafaka kwa pande zote mbili kuimarisha ushirikiano huo.
Aidha alibainisha kuwa Bandari ya Mombasa pamoja na vituo vyake vya ndani vinaendelea kushuhudia ongezeko la shehena, na akahakikishia kuwa KPA iko tayari kushughulikia mahitaji yanayoongezeka kupitia maboresho ya miundombinu na huduma.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
Business
Wakulima wa Mananasi Magarini walilia soko
Wakulima wa matunda aina ya nanasi katika eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi wanaitaka serikali kuwatafutia soko ili kuuza bidhaa zao ambazo zinaendelea kuharibika msimu huu.
Kulingana na wakulima hao hakuna soko ambapo wanaweza kuuza bidhaa hizo kwa bei nzuri hali inayofanya wakulima wengi kuuza kwa bei ya chini ili kuepuka kuharibika kwa katunda hayo.
Wakizunumza na cocofm wakulima hao walisema kuwa kwa sasa wanakadiria hasara kwani matunda ni mengi.
Wakati huo huo wakulima hao wameitaka serikali ya kaunti kujenga viwanda.
Ni kauli ambayo imeongwa mkono na wafanyibiashara wa matunda mjini Kilifi kaunti ya Kilifi ambao walisema kuwa matunda mengi msimu huu huharibika kutokana na idadi ndogo ya wateja.
“Serikali itutafutie soko pamoja na kujenga viwanda ili kusaidia wakulima na wafanyibiashara wa matunda aina ya mamanasi, kuuza matunda yao ili kuawaepushia hasara hasa wakati huu ambapo matunda ni mengi.”
Taarifa ya Pauline Mwango

