News
Maelfu ya wakaazi wajitokeza kwenye matibabu ya bila malipo chuo kikuu cha pwani
Wiki ya matibabu ya bila malipo ya mwaka 2025 inakamilika jumapili ya tarehe 2, Novemba 2025, katika chuo kikuu cha Pwani kaunti ya kilifi, huku ikivutia maelfu ya wakaazi waliowasili kutafuta huduma za matibabu.
Wakaazi waliofika katika kambi hiyo ya matibabu walisema zoezi hilo linawapa fursa adimu ya kupata suluhu kwa matatizo yao ya kiafya, ambapo dawa za matibabu imekuwa changamoto kwa kuzifikia.
Wakaazi mmoja baada ya mwengine walieleza hisia zao kuhusiana na zoezi hili lililoasisiwa na wakfu wa wakili George Kithi, Chuo kikuu cha Pwani, COCOFM na wadau mbalimbali.
Akizungumza katika chuo kikuu cha pwani kunakoendelea zoezi hilo, mkurugenzi wa George Kithi Foundation, wakili George Kithi alisema wakaazi wa kaunti ya Kilifi wanauhitaji mkubwa wa huduma bora za afya.
Kithi alidokeza kuwa zoezi hilo litakuwa likifanywa mara kwa mara ili kuhakikisha wakaazi wa Kilifi na Pwani kwa jumla wanafikia huduma bora za afya, ili jamii iweze kuwa yenye afya inayostahili.

Wakili George Kithi akitembelea baadhi ya wagonjwa katika chuo kikuu cha pwani Kilifi.
Kwa upande wake mhadhiri wa chuo kikuu cha pwani profesa Halim Shauri, alipongeza uanzilishi wa mpango huo akidokeza kuwa chuo kikuu cha pwani kina mikakati ya kujenga hospitali kuu ambayo mbali na kutoa mafunzo ya kitaalamu, pia itasaidia kutoa huduma za afya kwa wakaazi wa pwani.

Baadhi ya wagonjwa waliofika katika chuo kikuu cha Pwani mjini Kilifi kupokea matibabu ya bila malipo.
Naye naibu msimamizi wa mpango wa kambi ya wiki ya matibabu ya bila malipo katika wakfu wa George Kithi daktari Julius Nyamawi, amesema zoezi hili limefaidi wakaazi wengi ambao wamekuwa na changamoto ya kupata matibabu.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

