Business
Muungano wa bodi za leseni za vileo wapinga sera ya NACADA
Muungano wa bodi za kudhibiti na kutoa leseni za vileo nchini umepinga vikali pendekezo la Sera ya Mwaka 2025 ya Mamlaka ya Kudhibiti Matumizi ya Pombe na Dawa za Kulevya (NACADA), wakidai kuwa linaenda kinyume na ugatuzi na kuondoa mamlaka ya kikatiba ya serikali za kaunti katika usimamizi wa biashara ya vileo.
Wakizungumza mjini Diani kaunti ya Kwale, wanachama wa Muungano huo wakiongozwa na Mwenyekiti wao, Julius Owino, walisisitiza kuwa serikali za kaunti ndizo zenye jukumu la kisheria na kikatiba la kutoa leseni, kusimamia, na kutekeleza sheria zinazohusu uuzaji wa pombe.
“Sera hii ya NACADA ni jaribio la kuingilia majukumu ya kaunti na itaathiri mapato ya serikali za kaunti, kaunti lazima zisalie na mamlaka kamili ya kusimamia biashara ya vileo kama ilivyowekwa katika Katiba,” alisema Owino.
Owino pia aliitaka NACADA kushirikiana na kaunti kwa njia ya mashauriano badala ya kujaribu kuchukua majukumu yao, akiongeza kuwa ushirikiano thabiti ndio utaleta mafanikio katika udhibiti wa pombe na dawa za kulevya.
Kauli yake iliungwa mkono na Richard Osongo, Mwenyekiti wa wamiliki wa baa katika kaunti ya Kwale, ambaye alitoa onyo kali dhidi ya kile alichokiita “unyanyasaji wa mamlaka za kaunti na NACADA.”
Muungano huo ulieleza kuwa utatoa mapendekezo rasmi kwa serikali ya kitaifa na kuhimiza mjadala wa wazi kabla ya utekelezaji wowote wa sera hiyo mpya.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
Business
KPA yaimarisha usafirishaji wa makasha na kampeni za kimataifa
Halmashauri ya bandari nchini (KPA), imeimarisha ushirikiano wake na kampuni ya kimataifa ya usafirishaji kwa njia ya bahari, Maersk, katika juhudi za kuboresha huduma na kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo katika eneo la Afrika Mashariki.
Makubaliano hayo yameafikiwa katika mkutano uliofanyika katika makao makuu ya KPA jijini Mombasa ambapo Mkurugenzi wa Maersk Kanda ya Afrika Mashariki, Tito Okuku, alieleza kuwa kampuni hiyo ina nia ya kupanua shughuli zake zaidi nchini na katika eneo la Afrika Mashariki kwa ujumla.
Moja ya maeneo yatakayopata kipaumbele ni kuimarisha matumizi ya Kituo cha Makontena cha ndani cha Naivasha kinachotazamwa kama kitovu muhimu katika kushughulikia usafirishaji wa mazao ya kilimo kutoka Kenya kwenda masoko ya kimataifa, huku kikitoa njia ya haraka na ya kuaminika kwa wauzaji kufikia masoko ya kimataifa.
Mkurugenzi Mkuu wa KPA, Nahodha William Ruto, alieleza kukubaliana na hatua hiyo akisema ni wakati mwafaka kwa pande zote mbili kuimarisha ushirikiano huo.
Aidha alibainisha kuwa Bandari ya Mombasa pamoja na vituo vyake vya ndani vinaendelea kushuhudia ongezeko la shehena, na akahakikishia kuwa KPA iko tayari kushughulikia mahitaji yanayoongezeka kupitia maboresho ya miundombinu na huduma.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
Business
Wakulima wa Mananasi Magarini walilia soko
Wakulima wa matunda aina ya nanasi katika eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi wanaitaka serikali kuwatafutia soko ili kuuza bidhaa zao ambazo zinaendelea kuharibika msimu huu.
Kulingana na wakulima hao hakuna soko ambapo wanaweza kuuza bidhaa hizo kwa bei nzuri hali inayofanya wakulima wengi kuuza kwa bei ya chini ili kuepuka kuharibika kwa katunda hayo.
Wakizunumza na cocofm wakulima hao walisema kuwa kwa sasa wanakadiria hasara kwani matunda ni mengi.
Wakati huo huo wakulima hao wameitaka serikali ya kaunti kujenga viwanda.
Ni kauli ambayo imeongwa mkono na wafanyibiashara wa matunda mjini Kilifi kaunti ya Kilifi ambao walisema kuwa matunda mengi msimu huu huharibika kutokana na idadi ndogo ya wateja.
“Serikali itutafutie soko pamoja na kujenga viwanda ili kusaidia wakulima na wafanyibiashara wa matunda aina ya mamanasi, kuuza matunda yao ili kuawaepushia hasara hasa wakati huu ambapo matunda ni mengi.”
Taarifa ya Pauline Mwango

