News
Mwandishi wa Vitabu vya Tamthilia Ngugi wa Thiong’o amefariki
Mwandishi nguli wa vitabu vya tamthilia Ngugi wa Thiong’o ameaga dunia akiwa na umri wa miaka 87.
Familia imethibitisha kifo chake kilichotokea siku ya Jumatano Mei 28, 2025 nchini Marekani.
Ngũgĩ wa Thiong’o ni mmoja wa waandishi mashuhuri na wenye ushawishi mkubwa kutoka Afrika, hasa nchini Kenya. Anafahamika sana kwa maandishi yake ya kifasihi, hasa Riwaya, Tamthilia, Insha na tafakari kuhusu Lugha, Siasa, Utamaduni na Ukoloni.
James Ngugi wa Thiong’o, baadaye alijulikana kama Ngũgĩ wa Thiong’o baada ya kuacha jina la Kikristo.
Alizaliwa tarehe 5 Januari 1938 katika kijiji cha Kamĩrĩthũ, eneo la Limuru katika kaunti ya Kiambu.
Ngugi alisoma katika shule ya upili ya Alliance High School – mojawapo ya shule za kitaifa nchini Kenya, kisha akaelekea katika chuo kikuu cha Makerere nchini Uganda na kuhitimu mwaka 1963 na akajiunga na chuo kikuu cha Leeds nchini Uingereza ambako aliendelea na masomo yake ya fasihi.
Ngũgĩ alianza kuandika vitabu katika lugha ya Kiingereza lakini baadaye aliacha kutumia Kiingereza katika kazi zake za fasihi na kuanza kuandika kwa lugha za Kikuyu na Kiswahili, kama njia ya kuendeleza utamaduni na lugha za Kiafrika.
Baadhi ya vitabu vyake maarufu ni pamoja na Weep Not, Child (1964) – riwaya ya kwanza ya Mwafrika kuchapishwa kwa Kiingereza.
Vingine ni pamoja na The River Between (1965), A Grain of Wheat (1967), Petals of Blood (1977), Devil on the Cross (Caitaani Mutharaba-ini, 1980) – aliandika akiwa gerezani, kwenye karatasi za chooni na Matigari (1986) – kitabu hiki kilipigwa marufuku Kenya kwa sababu ya ujumbe wake wa mapinduzi.
Baada ya vitisho vya kisiasa na kushambuliwa nchini Kenya, Ngũgĩ alihamia Uingereza, kisha Marekani, ambako ameendelea kufundisha katika vyuo vikuu mbalimbali hadi kifo chake.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

