News
Mwandishi wa Vitabu vya Tamthilia Ngugi wa Thiong’o amefariki
Mwandishi nguli wa vitabu vya tamthilia Ngugi wa Thiong’o ameaga dunia akiwa na umri wa miaka 87.
Familia imethibitisha kifo chake kilichotokea siku ya Jumatano Mei 28, 2025 nchini Marekani.
Ngũgĩ wa Thiong’o ni mmoja wa waandishi mashuhuri na wenye ushawishi mkubwa kutoka Afrika, hasa nchini Kenya. Anafahamika sana kwa maandishi yake ya kifasihi, hasa Riwaya, Tamthilia, Insha na tafakari kuhusu Lugha, Siasa, Utamaduni na Ukoloni.
James Ngugi wa Thiong’o, baadaye alijulikana kama Ngũgĩ wa Thiong’o baada ya kuacha jina la Kikristo.
Alizaliwa tarehe 5 Januari 1938 katika kijiji cha Kamĩrĩthũ, eneo la Limuru katika kaunti ya Kiambu.
Ngugi alisoma katika shule ya upili ya Alliance High School – mojawapo ya shule za kitaifa nchini Kenya, kisha akaelekea katika chuo kikuu cha Makerere nchini Uganda na kuhitimu mwaka 1963 na akajiunga na chuo kikuu cha Leeds nchini Uingereza ambako aliendelea na masomo yake ya fasihi.
Ngũgĩ alianza kuandika vitabu katika lugha ya Kiingereza lakini baadaye aliacha kutumia Kiingereza katika kazi zake za fasihi na kuanza kuandika kwa lugha za Kikuyu na Kiswahili, kama njia ya kuendeleza utamaduni na lugha za Kiafrika.
Baadhi ya vitabu vyake maarufu ni pamoja na Weep Not, Child (1964) – riwaya ya kwanza ya Mwafrika kuchapishwa kwa Kiingereza.
Vingine ni pamoja na The River Between (1965), A Grain of Wheat (1967), Petals of Blood (1977), Devil on the Cross (Caitaani Mutharaba-ini, 1980) – aliandika akiwa gerezani, kwenye karatasi za chooni na Matigari (1986) – kitabu hiki kilipigwa marufuku Kenya kwa sababu ya ujumbe wake wa mapinduzi.
Baada ya vitisho vya kisiasa na kushambuliwa nchini Kenya, Ngũgĩ alihamia Uingereza, kisha Marekani, ambako ameendelea kufundisha katika vyuo vikuu mbalimbali hadi kifo chake.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Rais Ruto atia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya uwekezaji wa mali
Rais William Ruto ametia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya kitaifa ya uwekezaji wa mali (Sovereign Wealth Fund), hatua inayotajwa kuwa muhimu katika juhudi za Kenya za kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kulinda utajiri wa taifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa muda mrefu.
Utiaji huo wa saini ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi na unaweka msingi wa kisheria wa kuanzishwa na kusimamiwa kwa mfuko wa taifa wa uwekezaji wa mali na kwamba unatarajiwa kuiwezesha nchi kuhifadhi rasilimali za umma zinazobaki baada ya matumizi ya kawaida, kufadhili uwekezaji wa kimkakati na kuimarisha uwezo wa uchumi kukabiliana na misukosuko ya kifedha siku zijazo.
Sheria hiyo mpya inaleta mfumo rasmi wa usimamizi wa utajiri wa taifa kwa kutenga akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili uwekezaji katika miundombinu ya kimkakati ili kuongeza uimara wa kifedha nchini pamoja na kuhimiza matumizi yenye uwajibikaji ya rasilimali za umma.
Mfuko huo utatumika kuwekeza mapato ya ziada yanayotokana na rasilimali za asili na mali nyingine za umma, kwa lengo la kuhakikisha manufaa yake yanawanufaisha wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Aidha, mfuko huo unakusudia kupunguza athari za changamoto za kiuchumi kwa kutoa kinga ya kifedha wakati wa misukosuko ya uchumi.
Sheria hiyo ni sehemu ya ajenda pana ya serikali ya mageuzi ya uchumi inayolenga kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza uwazi na kuendeleza maendeleo endelevu.
Pia, sheria hiyo imeweka mfumo wa uongozi na usimamizi wa mfuko huo, ukiwemo utaratibu wa kuhakikisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi madhubuti katika uwekezaji na matumizi ya rasilimali za umma.
Maafisa wa serikali wameeleza kuwa Mfuko wa Taifa wa Uwekezaji wa Mali utakuwa na mchango mkubwa katika kufadhili miradi ya maendeleo yenye kipaumbele nchini huku ukihifadhi utajiri wa taifa kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Kupitishwa kwa sheria hiyo kunaiweka Kenya miongoni mwa mataifa yanayoongezeka duniani ambayo yameanzisha mifuko ya taifa ya uwekezaji wa mali kwa lengo la kulinda mali za taifa, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili malengo ya maendeleo ya muda mrefu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
IEBC yakosolewa dhidi ya masharti mapya kwa wanasiasa
Kiongozi wa vijana katika Chama cha Wiper kaunti ya Kwale Nyawa Masai ameikosoa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC kutokana na masharti mapya iliyotoa dhidi ya wanasaisa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Nyawa ameitaka Tume hiyo kuzingatia kanuni zake na taratibu za kuandaa uchaguzi na wala sio kila uchao kutoa masharti ambayo yanakinzana na majukumu ya Tume, akisema kuna taasisi zengine za umma zinafaa kuwajibika.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa katika eneo la Mwereni gatuzi dogo la Lungalunga kaunti ya Kwale, Nyawa aliesisitiza haja ya wanasiasa kupewa nafasi ya kuzungumza na wananchi sawa na kueleza sera zao bila ya vizuizi.
Kiongozi huyo wa vijana ambaye alitangaza nia yake ya kuwania kiti cha uwakilishi wadi ya Mwereni wakati wa uchaguzi ujao, amesema taifa la Kenya linazingatia demokrasia na kwamba kila taasisi inafaa kutekeleza majukumu yake.
“Katika uwaja wa siasa IEBC inakuzi moja tu kama msimamizi na kama msimamizi anaanza kutengeza sheria hapo ndipo anakosea, hii Kneya ni nchi ya demokrasia kwa hivyo IEBC isilete sheria nyingi na kufuatilia wanasiasa kuhusu pesa watatumia kwa kampeni, hiyo sio jukumu lake kuna taasisi inaitwa EACC”, alisema Nyawa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

