News
ODM yatishia kujiondoa katika serikali jumuishi
Huenda mpango wa serikali jumuishi uliobuniwa na rais William Ruto na aliyekuwa Kinara wa chama cha ODM hayati Raila Odinga ukavunjika iwapo masuala ibuka yaliyowasilishwa na Chama cha ODM yatakosa kutimizwa.
Chama hicho kimekosoa jinsi baadhi ya wafuasi wa chama cha UDA kujitenga na mwenzao wa ODM licha ya kuwepo na mpango wa serikali jumuishi pamoja na kukosoa kutishiwa kwa baadhi ya viongozi wa ODM kujiondoa na chama hicho ili wajiunge na UDA.
Kiongozi wa walio wachache katika bunge la kitaifa Junet Mohammed alisema kuna njama ya kusambaratishwa kwa ushawishi wa chama cha ODM katika maeneo ya Nyanza na Pwani kwani kuna taarifa kwamba baadhi vya viongozi wa chama hicho wamekuwa wakishurutishwa na maafisa wa Ikulu ya rais.
Junet ambaye pia ni mbunge wa Suna Mashariki, alisisitiza kwamba ODM kujiunga na UDA haikuwa na makusudi bali serikali ilihitaji msaada wa viongozi wa chama hicho ili kulinusuru taifa kwani lilikuwa linaelekea mahali pabaya.
“Hatuko kwa serikali jumuishi kimakosa ama kimakusudi wala kwa mualiko bali tuliingia katika serikali jumuishi kutokana na serikali ya rais Ruto kutaka msaada watu ili kulinusuru taifa lakini kama uongozi wa UDA unaona kumetengeza misingi na umaarufu mashinani tunaweza kuwaacha watengeze serikali yao mwaka 2027”, alisema Junet.
Kiongozi huyo ambaye pia ni Mwanachama wa Kamati kuu ya chama hicho alisema wataisha mkutano wa dharura wa Kamati kuu ili kuangazia suala hilo kwani mvutano huo huenda ukazidi kushamiri iwapo hakutakuwa na mikakati mwafaka.
Katika siku za hivi majuzi katika siasa za mashinani, chama cha UDA kimeonekana kikiendeleza siasa za kuimarisha chama hicho pamoja na kusajili wanachama wapya ili kujienga umaarufu zaidi kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Viongozi wa UDA walionekana kutangaza hadharani kwamba hakutakuwa na mpango wa kusimamisha mgombea mmoja katika eneo kwenye serikali jumuishi yaani Zoning bali kila kiongozi akijipange kisiasa na kupambana katika nyadhfa anayoelenga kushikilia wakati wa uchaguzi mkuu ujao.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

