News
Rais Ruto atangaza siku 7 za taifa kuomboleza kifo cha Odinga
Rais William Ruto ametangaza siku 7 za taifa kuomboleza kifo cha Raila Amollo Odinga pamoja na bendera ya taifa kupeperushwa nusu mlingoti katika ofisi zote za umma na balozi za Kenya kwenye mataifa ya ugahibuni.
Katika hotuba yake kwa taifa, Rais Ruto amesema mazishi ya Marehemu Odinga yatakuwa ya kitaifa na jukumu hilo litatekelezwa na Wanajeshi chini ya uongozi wa Mkuu wa majeshi nchini Charles Kahariri.
Kiongozi wa nchi, ametaja kamati ya mipango ya mazishi ya Odinga ambayo itaongozwa na Naibu Rais Prof Kithure Kindiki kwa ushirikiano na Kakake mkubwa Odinga, Seneta Oburu Oginga pamoja na familia ya Odinga na viongozi wengine.
“Kutokana na kifo cha Waziri mkuu wa zamani Raila Odinga, kutakuwa na siku 7 za kuomboleza kifo cha ndugu yetu na Kamati ya mipango ya mazishi itaongozwa na Naibu Rais Prof Kithure Kindiki na Kakake Odinga, Seneta Oburu Oginga na atapewa heshima ya kitaifa ikiongozwa na wanajeshi”, alisema Rais Ruto.
Kiongozi wa nchi, hata hivyo amesema mkuu wa mawaziri nchini Musalia Mudavadi, Waziri wa madini Hassan Ali Joho, Kiongozi wa wengi bungeni Kimani, Ichungwah, na kiongozi wa wachache bungeni Junet Mohamed, Mke wa Odinga Mama Ida Odinga na baadhi ya familia ya Odinga wataondoka nchini hadi India kwa mipango ya usafirishaji wa mwili wa Odinga hadi Kenya.
Wakati huo huo ametoa risala za rambirambi kwa familia ya Odinga na wakenya kwa jumla na kutaja kama kiongozi aliyekuwa mkakamavu na kupigania demokrasia huku akiwataka wakenya kuwa na utulivu wakati mipango ya mazishi inapoendelea.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

