News
Wakulima Kilifi wanufaika na Ng’ombe wa maziwa.
Serikali ya kaunti ya Kilifi kupitia idara ya kilimo imeanzisha mpango wa kusambaza wa Ng’ombe wa maziwa kwa makundi ya wakulima wa mifugo kaunti hiyo.
Akizungumza na wanahabari wakati wa zoezi la ugavi wa ng’ombe hao eneo la Kakuyuni, waziri wa kilimo kaunti ya Kilifi Chula Mwagona alibainisha kuwa tayari jumla ya Ng’ombe 150 wamesambazwa katika maeneo mbalimbali ya kaunti hiyo kwa wafugaji.
Mwagona alikariri kuwa mradi huo unalenga kusambaza takriban ng’ombe 500 kwa makundi ya wafugaji ifikapo mwishoni mwa mpango huo.
“Kaunti ya kilifi idadi ya ng’ombe ambao tumesambaza inafika zaidi ya 150, kila kundi linapata ng’ombe 30 na saa hii tuko na makundi 17”, alisema Mwagona.
Wakati huo huo waziri huyo alidokeza kuwa mradi huo utapunguza pakubwa tatizo la uhaba wa maziwa ambao umekuwa ukikumba kaunti ya Kilifi mara kwa mara.
“Wakati kama huu uhaba wa maziwa umepunguwa kwa sababu maziwa yako kwa wingi, na kwa sababu sisi tumeanza kuwapatia wakulima ng’ombe tunatarajia kwamba ng’ombe wakianza kuzaa na kukamuliwa lile tatizo la maziwa ambalo tulikuwa tunapata litakuwa haliko”, aliongeza waziri huyo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

