News
Familia ya Kenyatta yatoa milioni 1.5 kusaidia Kanisa Katoliki Watamu
Familia ya rais mstaafu Uhuru Kenyatta imetoa shilingi milioni 1.5 kusaidia ujenzi wa kituo cha uchungaji cha Stella Maris Pastoral Center katika eneo la Watamu katika kaunti ya Kilifi.
Rais mstaafu Kenyatta alikuwa ameandamana na mkewe Bi Margaret Kenyatta pamoja na familia yao akiwemo Maina Gakuo na mkewe Anna Kadzo Gakuo Kenyatta, walipokelewa na Askofu wa Kanisa Katoliki jimbo la Malindi Willybard Lagho.
Kenyatta alilipongeza jimbo Katoliki la Malindi kwa kujitolea kujiimarisha kifedha kupitia mradi huo na kwamba aliahidi kulisaidia jimbo hilo hadi kituo hicho cha kichungaji kitakapokamilika.

Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, Bi Margaret Kenyatta, Askofu wa Malindi Willybard Lagho pamoja na mapadre na familia ya Kenyatta katika kituo cha Stella Maris, Watamu {picha kwa hisani}
Naye Askofu mkuu wa Kanisa Katoliki jimbo la Malindi Willybard Lagho, alishukuru msaada huo kutoka kwa familia ya rais mstaafu Uhuru Kenyatta kwa niaba ya Jumuiya ya Kikatoliki huku akipongeza juhudi za Mapadre wa jimbo hilo la Malindi katika kufanikisha uendelezi wa ujenzi wa kituo hicho hasa Padre Bernard Malasi, Padre Stephen Kadenge na Padre David Ndwiga.
Askofu Lagho, hata hivyo aliishukuru familia ya Kenyatta kwa ukarimu wao na kuwahakikishia kwamba dayosisi ya Malindi itawapa taarifa zaidi kuhusu maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho cha kichungaji.
Kituo hicho cha kichungaji cha Stella Maris kinatarajiwa kutumika kama kitovu cha kiroho, kijamii na kiuchumi kwa jumuiya ya kikatoliki na Jimbo kuu la Malindi mara kitakapokamilika.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

