News
Gavana Sakaja taabani kuhusu hoja ya kubanduliwa mamlakani
Zaidi ya Wawakilishi wadi 70 wa kaunti ya Nairobi walitia saini hoja ya kutokuwa na Imani na Gavana wa kaunti ya Nairobi Johnson Sakaja, ambayo inalenga kumbandua mamlakani iwapo hoja hiyo itapitishwa na bunge hilo.
Katika kikao cha siku ya Jumanne Agosti 25, 2025 katika bunge hilo ambacho kilihudhuriwa na Wawakilishi wadi 96 kati ya 122, Wawakilishi wadi hao walitia saini hoja hiyo ambayo pia inalenga kumtema nje Naibu Gavana wa kaunti hiyo James Muchiri.
Kikao hicho kilichoongozwa na Spika wa bunge hilo Ken Ng’ondi pamoja na kiongozi wa walio wengi katika bunge hilo Peter Imwatok, Niabu Kiranja wa wachache katika bunge hilo Mark Mugambi na Waithera Chenge, kimeweka wazi ajenda za kumtimua Gavana Sakaja na Muchiri.
Wawakilishi wadi hao walisema Gavana Sakaja pamoja na Naibu wake walishindwa kusimamia vyema raslimali za kaunti, ukiukaji wa Katiba, utumizi mbaya wa ofisi ya umma miongoni mwa masuala mengine ibuka.
Iwapo hoja hiyo itafaulu katika mchakato wa kumtimua Gavana Sakaja na naibu wake, basi moja kwa moja spika wa bunge hilo Ken Ng’ondi atachukua nafasi ya ugavana kwa kipindi cha siku 60 kabla ya uchaguzi wa ugavana kufanyika.
Hayo hayo yatategemea iwapo hoja hiyo itapitishwa katika bunge hilo baada ya Wawakilishi wadi wa Nairobi watakaporejelea vikao vya bunge mwezi Septemba na iwapo bunge la Seneti kwa kuzingatia kanuni za Katiba itaidhinisha hoja hiyo ya Wawakilishi wadi.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

