International News
Israel na Marekani zazidisha mashambulizi dhidi ya Iran
Kwa siku ya tano mfululizo Jeshi la Israel kwa ushirikiano na Marekani, limefanya mashambulio mapya katika ardhi ya Iran dhidi ya kile imekitaja kuwa kuangamiza kabisa utawala wa kigaidi huku ikiionya Iran kujiandaa kwa mashambulio makubwa zaidi yatakayoisambaratisha miundombinu ya kijeshi ya nchi hiyo.
Mashambulio hayo ya usiku wa kuamkia leo Machi 4, yalilenga mji Tehran na Beirut, kama mwendelezo wa hujuma nzito za kijeshi baada ya lile shambulio la Februari 28, lililomuua kiongozi wa kidini Ayatola Ali Khameni.
Mwendelezo huo wa mashambilizi sasa yanaifikisha idadi ya watu waliouawa katika pande zote mbili takribani watu 700.
Mataifa kama vile Ufaransa, Urusi, na China yalitoa wito wa kusitishwa kwa haraka vita hivyo, lakini kauli ya Rais wa Marekani Donald Trump haionyeshi dalili za kukomeshwa kwa mashambulio hayo baada ya kudokeza katika taarifa yake, kwamba vita hivyo huenda vikachukua zaidi ya wiki 5.
Kwa upande wake, Iran inazidisha mashambulizi yake dhidi ya taasisi muhimu za Israel na Marekani katika eneo la Mashariki ya kati na shambulio la hivi punde kabisa likilenga ubalozi wa Marekani huko Dubai na bandari Ya Fujairah.
Pia mashambulio hayo yanaendelezwa nchin Israel, ambako Idadi ya vifo vya Waisreali inazidi kuongezeka, ingawa hakuna taarifa kuhusu idadi kamili.
Viongozi wa juu wa Israel wamepiga marufuku kutangaza au kupiga picha mashambulizi yanayoyafanya ndani ya Israel.
Mashambilizi haya sasa yamesambaa katika eneo la Ghuba huku Mataifa ya kigeni yakianzisha mkakati wa kuwahamisha raia wao ambao wamekwama kufuatia kufungwa kwa anga za mataifa hayo.
Iran pia imefunga Mlango wa Bahari ya Hormuz ambayo ni muhimu kwa kupitisha takriban mapipa milioni 20 ya mafuta kila siku.
Hatua hii tayari imeathiri biashara ya kimataifa.
Taarifa ya Eric Ponda
International News
Vita vya Iran vyasambaratisha biashara za kimataifa.
Vita vya Iran vinaweza kuisha hivi karibuni au kuendelea kwa miezi kadhaa licha ya tamko la rais wa Marekani Donald Trump kuhusu mpango ya kumaliza vita hivyo.
Iwapo vita hivyo vitakomeshwa basi Hormuz itakapofunguliwa tena ilhali mtihani halisi utakuwa ni vipi minyororo ya usambazaji wa nishati, mbolea na bidhaa nyingine itaweza kurejea haraka.
Wakati wale wenye matumaini wakianza kuhisi kwamba vita kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran vilikuwa karibu kumalizika, mgogoro huo wa mwezi mzima unachukua mwelekeo mwingine tena.
Rais wa Marekani Donald Trump alionya Tehran kwamba hakutakuwa na kurudi nyuma kuhusu mashambulizi yaliyoongozwa ya Marekani, kinyume na kauli yake kwamba hivi karibuni Marekani itaondoka Iran na hatua za kijeshi za nchi hiyo zitakomeshwa ndani ya wiki mbili au tatu zijazo.
Iran, kwa upande wake, inaruhusu idadi ndogo ya meli kupita katika Mlango wa Hormuz, huku ikikanusha kuwa mazungumzo yoyote ya kusitisha vita yanaendelea.
Wataalamu wengi wanakubaliana juu ya jambo moja muhimu: kadiri mzozo huu unavyoendelea kwa muda mrefu, ndivyo athari zake zitakavyokuwa mbaya zaidi kwa usambazaji wa nishati duniani, mfumuko wa bei na uthabiti wa uchumi.
Benki ya hifadhi ya Shirikisho ya Dallas, ambayo ni sehemu ya mfumo wa benki kuu ya Marekani, ilitabiri mapema mwezi huu kwamba kufungwa kwa mlango huo kwa miezi mitatu au zaidi kungesababisha ukuaji wa pato la taifa la dunia kupungua kwa asilimia 2.9 kwa mwaka katika robo ya pili ya mwaka.
International News
Trump asema Marekani itasitisha vita dhidi ya Iran
Rais Donald Trump amesema kwamba Marekani itaondoka Iran hivi karibuni na hatua za kijeshi za nchi hiyo zitakomeshwa ndani ya wiki mbili au tatu zijazo.
Rais Trump alisema Marekani imefikia malengo iliyojiwekea kabla ya kuanza kwa mashambulizi ya anga dhidi ya Iran mwezi uliyopita kwa ushirikiano na Israel.
Aidha aliongeza kuwa lengo la kuizuia Iran kuwa na uwezo wa kuunda silaha za nyuklia limefikiwa na sasa Marekani inamaliza kazi.
Trump pia aliema Marekani sasa inatawala anga za Iran na pia imepata mabadiliko ya utawala kufuatia mauaji ya viongozi wakuu wa kisiasa na kijeshi.
Aliwataja viongozi hao wapya mjini Tehran kama walio na misimamo mikali na waadilifu zaidi, ikilinganishwa na watangulizi wao.
Trump pia alisema viongozi wa Iran wanaomba kufanya makubaliano na Marekani ili kumaliza vita, madai ambayo hapo awali yalipingwa na Iran na kuongeza kwamba vita vinaweza kumalizika bila makubaliano kati ya pande hizo mbili.
Kuhusu athari za vita hasa kupanda kwa bei ya mafuta, rais Trump alisema bei itashuka mara tu Marekani itakapomaliza hatua zake za kijeshi.

