News
Mahamoud Ali Ashinda Uchaguzi wa AUC
Mgombea wa wadhifa ya uwenyekiti wa Tume ya umoja wa Afrika AUC, Mahmoud Ali Youssouf kutoka Djibouti, sasa ndiye Mwenyekiti mpya wa Tume hiyo baada ya kushinda kwa kura 33 katika awamu ya 7.
Hii ni baada ya Raila Odinga kutoka Kenya kujiondoa katika kinyang’anyiro hicho baada ya kushindwa na Mahmoud katika awamu ya tano na sita katika kinyang’anyiro hicho.
Mahmoud, ambaye katika awamu ya saba amepata kura 33, ambayo ni thuluthi mbili ya kura zote zilizopigwa katika ukumbi wa Nelson Mandela jijini Addis Ababa nchini Ethiopia, amepewa majukumu yake rasmi.
Wachanganuzi wa maswala ya kisiasa wameipongeza serikali ya Kenya kwa kuonyesha juhudi za kuyashawishi mataifa ya Afrika kumuunga mkono Odinga, japo matokeo hayakuridhisha.
Hata hivyo wanaogombea nafasi hiyo ilikuwa ni pamoja na Raila Odinga wa Kenya, Mahmoud Ali Youssouf wa Djibouti na Richard Randriamandrato wa Madagascar, huku mataifa ya Sudan, Burkina Faso, Mali, Gabon, Niger na Guinea yakifungiwa nje ya uchaguzi huo kutokana na vita katika mataifa hayo.
News
Washukiwa 5 wa uhalifu wanazuiliwa na polisi Likoni
Maafisa wa polisi katika eneo bunge la Likoni kaunti ya Mombasa wanawazuiliwa washukiwa 5 wa uhalifu waliokamatwa katika oparesheni iliyofanyika maeneo ya Duduz na Bufallo siku ya Jumatatu tarehe mosi Juni 2026.
Washukiwa waliokamatwa ni Brian Musa mwenye umri wa miaka 24, Abubakar Mahasi wa umri wa miaka 20, Juma Kassim mwenye umri wa miaka 16, Omar Gobeko maarufu Mboga mwenye umri wa miaka 19 na Jackson Mwambu mwenye umri wa miaka 26.
Msako huo uliongozwa na mkuu wa kituo cha polisi cha Shelly Beach pamoja na kikosi cha maafisa wa polisi.
Maafisa wa Polisi wamesema mshukiwa Brian Musa anakabiliwa na tuhuma za maandalizi ya kutenda kosa la jinai, huku Ababakar Mahasi, Juma Kassim na Omar Gobeko wakihusishwa na tuhuma za wizi wa mabavu.
Mshukiwa mwengine Jackson Mwambu anahusishwa na tuhuma za kupatikana na mali ya serikali kinyume cha sheria.
Katika oparesheni hiyo, maafisa wa polisi walifanikiwa kupata vielelezo mbali mbali ikiwemo panga tatu pamoja na koti la jeshi la KDF.
Taarifa ya Joseph Jira
News
DCI waomba muda zaidi dhidi ya kesi ya Keziah
Mahakama ya Kilifi imeagiza kuendelea kuzuiliwa kwa siku 6 zaidi Alice Auma Omondi anayetuhumiwa kuhusika kwenye kesi ya mauaji ya mtoto Keziah aliyekuwa na umri wa miaka 7.
Hakimu wa Mahakama hiyo Ivy Wasike ametoa agizo hilo baada ya afisa anayechunguza kesi hiyo Evans Baraza kuiambia Mahakama kwamba bado hawajakamilisha uchunguzi wao.
Alice Auma Omondi anayedaiwa kuwa Mamake mshukiwa mkuu wa mauaji hayo Dennis Otieno Odour kwa jina maarufu Dennis Mkikuu alikamatwa kama mshukiwa wa kwanza na kufikishwa Mahakamani tarehe 6 mwezi Mei 2026 ambapo aliagizwa kuzuiliwa kwa wiki tatu ili ashirikiane na maafisa wa polisi kumtafuta mshukiwa mkuu.
Hata hivyo wiki moja baadaye mshukiwa mkuu Dennis alikamatwa na kufikishwa katika Mahakama ya Shanzu ambapo bado anazuiliwa kufuatia kesi ya mauaji dhidi yake.
Maafisa wa DCI wanamshuku Alice kwamba anahusika kwenye kesi hiyo kwa kuharibu ushahidi huku maafisa hao wakipendekeza kwamba Alice pia anafaa kufunguliwa mashtaka baada ya uchunguzi kamili.
Kesi hiyo itatajwa tarehe 8 mwezi huu wa Juni.
Taarifa ya Teclar Yeri
