News
Mahamoud Ali Ashinda Uchaguzi wa AUC
Mgombea wa wadhifa ya uwenyekiti wa Tume ya umoja wa Afrika AUC, Mahmoud Ali Youssouf kutoka Djibouti, sasa ndiye Mwenyekiti mpya wa Tume hiyo baada ya kushinda kwa kura 33 katika awamu ya 7.
Hii ni baada ya Raila Odinga kutoka Kenya kujiondoa katika kinyang’anyiro hicho baada ya kushindwa na Mahmoud katika awamu ya tano na sita katika kinyang’anyiro hicho.
Mahmoud, ambaye katika awamu ya saba amepata kura 33, ambayo ni thuluthi mbili ya kura zote zilizopigwa katika ukumbi wa Nelson Mandela jijini Addis Ababa nchini Ethiopia, amepewa majukumu yake rasmi.
Wachanganuzi wa maswala ya kisiasa wameipongeza serikali ya Kenya kwa kuonyesha juhudi za kuyashawishi mataifa ya Afrika kumuunga mkono Odinga, japo matokeo hayakuridhisha.
Hata hivyo wanaogombea nafasi hiyo ilikuwa ni pamoja na Raila Odinga wa Kenya, Mahmoud Ali Youssouf wa Djibouti na Richard Randriamandrato wa Madagascar, huku mataifa ya Sudan, Burkina Faso, Mali, Gabon, Niger na Guinea yakifungiwa nje ya uchaguzi huo kutokana na vita katika mataifa hayo.
News
NCTC yaanzisha hamasa mashinani kudhibiti ugaidi
Kituo cha kitaifa cha kukabiliana na ugaidi yaani National Counter Terrorism Centre (NCTC) kimeanzisha mpango wa kutoa hamasa za kuwaepusha wananchi na masuala ya ugaidi hasa maeneo ya Shakahola katika eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi.
Akizungumza katika eneo hilo, Afisa mkuu wa kituo hicho Grace Kaparo aliwataka wazazi kufuatilia kwa ukaribu mienendo ya watoto wao kama njia mojawapo ya kuzuia michipuko ya makundi ya ugaidi.
Kaparo alidokeza kwamba mpango huo unalenga kupunguza visa vya uhalifu miongoni mwa vijana sambamba na kuwajengea mustakabali bora wa maisha yao.
Hamasa hiyo inajiri baada ya kushughudiwa maafa ya watu zaidi ya 400 katika msitu wa Shakahola kutokana na mafunzo ya itikadi kali huku mshukiwa mkuu wa mauaji hayo akiwa katika mikono ya maafisa wa polisi.
“Tumekuja Shakahola kuelimisha jamii kuepusha makundi ya kigaidi na jinsi ya kutambua watu walio na itikadi kali ili kuepusha watu kuangamia kama hapa Shakahola watu wangekuwa na ufahamu wangeepuka maafa”, alisema Grace.
Kwa upande wake Naibu Kamishna eneo Malindi kaunti ya Kilifi Harrison Matevwa aliwataka maafisa wa utawala eneo hilo kuendeleza hamasa za mara kwa mara kwa wakaazi wa maeneo yao ili kutathmini changamoto zinazowakumba na kuzitatua mara moja.
“Naiambia kamati ya usalama eneo hili kutembea na kufanya baraza za usalama kuweza kuskia ile wananchi wanapitia kwa sababu wengi wanakosa usaidizi ndio watu wahalifu wakija wanaweza kuwapotosha”alisema Harrison.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Wakurugenzi wa Kampuni ya Bima ya Direct Line waagizwa kufika Mahakamani
Mahakama ya Malindi imewaamuru wakurugenzi wa Kampuni ya Bima ya Direct Line kufika Mahakamani binafsi kwa ajili ya kuhojiwa.
Hii ni baada ya kampuni hiyo kushindwa kutekeleza amri ya Mahakama ya kulipa fidia ya shilingi milioni 2.26 kwa mwanamke aliyejeruhiwa vibaya katika ajali ya barabarani iliyokea Oktoba 6, mwaka 2016.
Kampuni hiyo, inayohusishwa na familia ya mfanyabiashara mashuhuri nchini ilishindwa kumlipa Hellen Waiyaki kiasi cha shilingi 2,259,825 kama ilivyoamriwa na Mahakama.
Waiyaki aliwasilisha kesi Mahakamani baada ya kampuni hiyo kukosa kutekeleza wajibu wake wa kulipa kiwango hicho cha pesa licha ya kuagizwa na Mahakama kufuatia ajali hiyo iliyohusisha basi la Tahir Sheikh Said Transporters Limited, maarufu kama TSS Bus Company, yenye nambari ya usajili KBZ 475S.
Akitoa uamuzi huo, Hakimu Mwandamizi wa Mahakama ya Malindi, Joy Wesonga, alisema ni lazima wakurugenzi hao wafike Mahakamani binafsi na kujieleza, akisema kampuni hiyo imekuwa ikiwazuia wananchi kufikia ofisi zao.
“Wakurugenzi hao watahitajika kufika mahakamani wakiwa na kuwasilisha vitabu vya hesabu vilivyokaguliwa vya kampuni, taarifa za benki pamoja na sajili ya mali za kampuni kwa kipindi cha miaka miwili ya mwisho ya kifedha ili Mahakama iweze kubaini uwezo wa kifedha wa kampuni hiyo na hali ya shughuli zake za kibiashara nchini Kenya.” alisema Hakimu Wesonga.
Katika hati kiapo kilichowasilishwa mahakamani kupitia wakili wake George Wakahiu, Hellen Waiyaki alisema alikuwa abiria ndani ya gari hilo ambalo lilikuwa likiendeshwa kwa uzembe kabla ya kupinduka na kusababisha ajali iliyomwacha na majeraha mabaya mwilini.
Kesi hiyo itaendeleza mnamo Julia 31 mwaka huu
Taarifa ya Mwanahabari wetu
