News
Mashahidi wafichua maovu kwenye kesi ya Shakahola
Ushahidi wa kutisha umeendelea kufichuliwa katika kesi ya mauaji ya Shakahola, ambapo Mhubiri tata Paul Mackenzie na washukiwa wenzake 35 wanakabiliwa na mashtaka mazito ikiwemo ukatili wa watoto, mateso, na unyimwaji wa elimu.
Kesi hiyo iliendelea kusikilizwa mbele ya Hakimu mkuu Nelly Chepchirchir katika Mahakama ya Watoto ya Tononoka kaunti ya Mombasa huku mashahidi wanne wakitoa ushahidi wao.
Mmoja wa mashahidi, Maxwell Kisienya, ambaye ni Mkurugenzi wa shule ya Bridge International Academy Lungalunga, alieleza kuhusu mwanafunzi aliyetoweka baada ya kuondolewa shuleni kwa kushindwa kulipa karo mnamo tarehe 19 Oktoba 2017 na tokea hapo, shule haikupokea maombi yoyote ya uhamisho, wala hakujulikana alipoelekea mwanafunzi huyo.
Katika ushahidi wa kidijitali, Koplo Joseph Mwai, mtaalamu wa uchunguzi wa kidijitali kutoka Kitengo cha Kupambana na Ugaidi, ameeleza mahakama jinsi alivyovuna taarifa kutoka kwa simu ya shahidi ambapo aligundua picha nne za watu waliokonda kupita kiasi.
Aidha, mtaalamu wa upasuaji wa maiti, Dkt. Richard Njoroge, alithibitisha kwamba miili mingi kati ya ile 453 iliyofukuliwa kutoka makaburi ya halaiki ilikuwa katika hali ya kuharibika kupita kiasi huku akieleza kwamba katika baadhi ya miili, njaa kali ndiyo iliyotajwa kuwa chanzo cha kifo kutokana na ukosefu mkubwa wa uzito wa mwili.
Kwa mujibu wa daktari huyo, sampuli za meno, mifupa na kucha zilichukuliwa kutoka kwa miili hiyo na kufanyiwa vipimo vya DNA, ambapo baadhi ya waathiriwa sasa wametambuliwa kupitia familia zao.
Mahakama pia ilisikiliza ushahidi kutoka kwa Inspekta mkuu Job Wafula Wanyonyi, aliyekuwa miongoni mwa kikosi cha kwanza kilichofika Shakahola kufuatia ripoti za kijasusi, mnamo tarehe 13 mwezi Aprili 2023, ambapo aliwaokoa watu waliokuwa wakiishi kwenye vibanda duni, wengi wao wakiwa dhaifu kiasi cha kushindwa hata kuzungumza.
Aliongeza kuwa baadhi ya watu waliokamatwa walikuwa wakilinda maeneo hayo wakiwa na silaha kama rungu na jembe.
Kesi hiyo itaendelea kusikilizwa siku Jumatano, Septemba 17 mwaka huu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Wajumbe wa bunge la Seneti wazuru kaunti ya Kilifi
Baadhi ya wajumbe wa bunge la Seneti chini ya mpango wa Seneti mashinani wamefanya ziara katika majengo ya bunge la kaunti ya Kilifi na kupokelewa na Karani wa bunge hilo Michael Ngala.
Wajumbe hao wa sekta mbalimbali wa bunge la Seneti wakiongozwa na Daniel Chania, wametathmini masuala mbalimbali ya bunge la kaunti ya Kilifi kama lina uwezo wa kuandaa ziara ijayo ya Seneti mashinani.
Seneti Mashinani ilianzishwa chini ya kifungu cha 126 ibara ya kwanza ya Katiba ya Kenya ya mwaka 2010, kinachoruhusu kikao cha bunge lolote kufanyika mahali popote ndani ya taifa la Kenya na kuanza wakati wowote kitakapopangwa na bunge.
Malengo ya vikao hivyo katika kaunti ni pamoja na kuhamasisha umma kuhusu kazi za bunge na Seneti, kuimarisha ushiriki wa umma katika shughuli za Seneti kwenye ngazi ya kaunti sawa na kutoa hamasa kwa wananchi kwa lengo la kuhimiza ushiriki umma katika utawala.

Baadhi ya wajumbe wa bunge la Seneti chini ya mpango wa Seneti mashinani wamefanya ziara katika majengo ya bunge la kaunti ya Kilifi
Bunge la Seneti limeanza maandalizi ya vikao vitakavyofanyika nje ya Nairobi, ambavyo vinatarajiwa kufanyika mwezi Septemba 2026.
Kaunti ya Kilifi ni miongoni mwa kaunti zilizoteuliwa kuwa kati ya zile zitazoandaa vikao hivyo kwa ajali ya umma kuwa na uelewa zaidi kuhusu shughuli za bunge hilo.
Wajumbe hao walikuwa na malengo pia ya kubaini upatikanaji wa miundombinu na huduma muhimu ili kuiwezesha Seneti kufanya uamuzi.
Kaunti nyingine zilizowahi kuandaa Seneti Mashinani ni pamoja na kaunti ya Uasin Gishu mwaka 2018, ikifuatiwa na kaunti ya Kitui mwaka 2019, kaunti ya Turkana mwaka 2023 na kaunti ya Busia mwaka 2025.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Sakata ya mafuta yaathiri sekta ya uchukuzi nchini
Huenda watumizi wa magari ya uchukuzi wa umma, wahudumu wa tuktuk na bodaboda wakalazimika kuongeza nauli kwa abiria kutokana na changamoto za ukosefu wa mafuta nchini na kuathiri zaidi shughuli za uchukuzi.
Hatua hii imetakana na changamoto za uhaba wa mafuta nchini baada ya kuibuka kwa sataka ya uagizaji wa mafuta ghushi kupitia bandari ya Mombasa.
Kulingana na serikali kupitia Wizara ya Kawi, sakata hiyo ya shilingi bilioni 12 ilikuwa imelata tani elfu 60 za mafuta ya petroli kinyume cha sheria pamoja na mipango ya serikali ya uagizaji mafuta wa serikali kwa serikali yaani G to G.
Sakata hii imepelekea Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya kudhibiti kawi na bei za mafuta nchini EPRA Daniel Kiptoo, Katibu katika Idara ya petroli nchini Mohammed Liban na mkurugenzi wa Kampuni ya Kenya Pipeline Joe Sang kujiuzulu.
Kujiuluzu kwao kumetokana na kukamatwa na maafisa wa idara ya upelelezi wa jinai nchini DCI, kwa ushirikiano na Tume ya maadili na kupambana na ufisadi nchini EACC baada ya kutilia shaka zabuni iliyopewa kampuni binafsi ya One Petroleum Limited inayomilikwa na mfanyibiashara mashuhuri jijini Mombasa.

Wahudumu wa sekta ya bodaboda wakikabiliwa na changamoto za uhaba wa mafuta ya Petroli
Siku ya Jumanne, Waziri wa Kawi nchini Opiyo Wandanyi alifanya kikao na wakurugenzi wa kampuni za mafuta nchini na kuagiza shehena ya mafuta katika bandari ya Mombasa kurejeshwa kwani serikali haitambua shehena hiyo.
“Wahusika wa sakata hiyo walikuwa na njama ya kuongeza bei ya mafuta nchini kwa shilingi 14 zaidi kwa lita wakitumia nafasi ya vita vinavyoendelea kati ya Iran na Marekani na Israel, hiyo hatuta kubali”, alisema Wandayi.
Hatua hiyo ilikuwa inalenga pia kukwepa mpango wa serikali wa uagizaji mafuta kutoka mataifa ya miliki za kiarabu wa serikali kwa serikali yaani G to Go, akisema wahusika wa sakata ya ufisadi ni lazima wachukuliwe hatua.
Itakumbukwa kwamba rais William Ruto hivi majuzi alidokeza kwamba wahusika wote wa sakata ya ufisadi kwenye sekta ya mafuta watachukuliwa hatua, akishililia kwamba serikali haitakubali ufisadi nchini, huku akikosa kuweka wazi hatma ya maafisa hao wakuu wa serikali.
“Hawa walaghai wa mambo ya mafuta watakipata, hawaweze kuhepa kwa sababu haiwezekani katika taifa letu la Kenya watu wanaone tuko na shida ya mashariki ya kati wanakuja kukoroga shida nyengine hapa Kenya, serikali itakabiliana kikamilifu na wafisadi”, alisema Rais Ruto.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

