News
Mwinyi: Serikali izuie Ubomozi wa Nyumba Elfu moja Changamwe
Viongozi wa kisiasa kaunti ya Mombasa wanaitaka serikali kuingilia kati na kuzuia ubomozi wa nyumba zaidi ya elfu moja katika maeneo ya Chaani, Migadini, Lilongwe na Portreitz katika eneo bunge la Changamwe.
Wakiongozwa na Mbunge wa Changamwe Omar Mwinyi, viongozi hao wamesema baadhi ya wanasiasa walio uongozini wamekuwa wakisaidia mabwenyenye kunyakua ardhi za wananchi walalahoi.
Akizungumza na Wanahabari katika eneo bunge lake, Mwinyi ameitaka serikali kutafuta suluhu la kudumu la migogoro ya mashamba katika kaunti ya Mombasa na eneo la Pwani kwa jumla.
Mbunge huyo hata hivyo amewataka wanasiasa kukoma kuwanyanyasa wananchi na badala yake kuwahudumia bila ubaguzi ili kuzikabili changamoto mbalimbali mashinani.
Kauli yake imejiri baada ya familia nyingi katika maeneo ya Chaani, Migadini, Lilongwe na Portreitrz kulalamikia ubomozi wa nyumba zao bila mikakati mwafaka ya kuhamishiwa katika ardhi mbadala.
News
Wanaomiliki silaha haramu kaunti ya Tana river waonywa
Idara ya usalama kanda ya Pwani imewaonya wananchi wanaomiliki silaha haramu katika kaunti ya Tana river.
Mshirikishi wa utawala kanda ya Pwani Paul Rotich aliwataka wanaomiliki silaha hizo kuzisalimisha mara moja kwa maafisa wa polisi katika kituoc cha polisi kiilichokaribu nao.
Akizungumza katika kikao cha kiusalama kaunti ya Tana river, Rotich alisema oparesheni ya kusaka silaha hizo imeenzishwa huku akiwaagiza machifu na manaibu wao kushirikiana na maafisa wa polisi ili kuhakikisha silaha hizo zinapatikana.
Rotich alisema zaidi ya bunduki 120 ziko mikononi mwa raia wa maeneo ya Bangale na Tana Kaskazini katika kaunti ya Tana river, akisema ni lazima zirudishwe kwa serikali.
“Tunataka zile bunduki zote mnazomiliki kinyume cha sheria mrudishe kwanza ndio tuongee mambo ingine, haiwezekana mnamiliki bunduki haramu na mnataka serikali iwalinde kwani mtaishi na majangili mpaka lini, hiyo maneno hatutakubali rudisheni bunduki ama tutaanzisha oparesheni kali”, alisema Rotich.
Hata hivyo wakaazi wa kaunti hiyo wamepongeza hatua hiyo ya serikali, wakiwarai wenyeji kukumbatia amani ili kuepuka umwagikaji wa damu katika kaunti hiyo.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Mahakama kuu yamzuia Kingi na Wetangula kujihusisha na siasa
Spika wa bunge la Kitaifa Moses Wetangula na spika wa bunge la Seneti Amason Kingi wamepigwa breki kujihusisha na mikutano ya kisiasa.
Hii ni kufuatia amri ya Mahakama kuu inayowataka wawili hao kukoma kujihusisha na uhamasishaji wa kisiasa kwa muda wakisubiri kusikilizwa kwa ombi linalopiga shughuli zao lilowasilishwa Mahakamani na Shirika la Vocal Africa.
Jaji wa Mahakama hiyo David Mburu, alitoa amri hiyo akiagiza kuwa ombi hilo lisikilizwe kwa umakini na washtakiwa wote wawasilishiwe stakabadhi za kesi hii leo.
Katika ombi hilo, Shirika la Vocal Africa linadai kuwa ushiriki wa maspika hao katika shughuli za kisiasa unaibua maswali mazito ya kikatiba kuhusiana na uhuru wa bunge na majukumu yaliyowekwa kwa maafisa wa serikali.
Vocal Africa pia limesisitiza kuwa, ingawa kila ana haki ya kuwa na maoni ya kisiasa na kushiriki katika maswala ya kisiasa, maspika wanashikilia ofisi za kikatiba ambazo hazihitaji upendelea bali zinahitaji uhuru wa kitaasisi.
Kwa muda sasa spika Kingi na Wetangula wameonekana katika mikutano mbalimbali ya kisiasa wakipigia debe ajenda ya rais William Ruto, kinyume na Katiba inayowalazimisha maspika kuangazia masuala ya bunge na shughuli zengine muhimu za kiserikali.
Taarifa ya Elizabeth Mwende

