News
Ruku: Serikali kuajiri vijana laki moja kwa NYS
Serikali inalenga kuajiri zaidi ya vijana laki moja katika Shirika la huduma kwa vijana wa taifa NYS.
Waziri wa utumishi wa umma nchini Geoffrey Ruku amesema hatua hiyo itachangia kuboreshwa kwa huduma za umma sawa na kuhakikisha Shirika la NYS linakuwa nguzo muhimu kwa maendeleo ya taifa.
Akizungumza katika kaunti ya Machakos, Waziri Ruku amesema hatua hiyo itapunguza utegemeaji wa ufadhili wa umma kwani shirika hilo itapanua mikakati bora ya serikali ya kibiashara pamoja na kufanikisha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Waziri Ruku amelishinikiza bunge la kitaifa kuharakisha marekebisho ya mswada wa NYS ambao utawalishwa na Wizara yake bungeni ili kusawazisha mfumo wa kisheria wa shirika hilo.
Wakati huo huo amewataka vijana kukumbatia mipango ya serikali ya kujumuisha wananchi wote pamoja katika kufanikisha ajenda ya serikali ya maendeleo endelevu hadi mashinani.
News
Wanaomiliki silaha haramu kaunti ya Tana river waonywa
Idara ya usalama kanda ya Pwani imewaonya wananchi wanaomiliki silaha haramu katika kaunti ya Tana river.
Mshirikishi wa utawala kanda ya Pwani Paul Rotich aliwataka wanaomiliki silaha hizo kuzisalimisha mara moja kwa maafisa wa polisi katika kituoc cha polisi kiilichokaribu nao.
Akizungumza katika kikao cha kiusalama kaunti ya Tana river, Rotich alisema oparesheni ya kusaka silaha hizo imeenzishwa huku akiwaagiza machifu na manaibu wao kushirikiana na maafisa wa polisi ili kuhakikisha silaha hizo zinapatikana.
Rotich alisema zaidi ya bunduki 120 ziko mikononi mwa raia wa maeneo ya Bangale na Tana Kaskazini katika kaunti ya Tana river, akisema ni lazima zirudishwe kwa serikali.
“Tunataka zile bunduki zote mnazomiliki kinyume cha sheria mrudishe kwanza ndio tuongee mambo ingine, haiwezekana mnamiliki bunduki haramu na mnataka serikali iwalinde kwani mtaishi na majangili mpaka lini, hiyo maneno hatutakubali rudisheni bunduki ama tutaanzisha oparesheni kali”, alisema Rotich.
Hata hivyo wakaazi wa kaunti hiyo wamepongeza hatua hiyo ya serikali, wakiwarai wenyeji kukumbatia amani ili kuepuka umwagikaji wa damu katika kaunti hiyo.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Mahakama kuu yamzuia Kingi na Wetangula kujihusisha na siasa
Spika wa bunge la Kitaifa Moses Wetangula na spika wa bunge la Seneti Amason Kingi wamepigwa breki kujihusisha na mikutano ya kisiasa.
Hii ni kufuatia amri ya Mahakama kuu inayowataka wawili hao kukoma kujihusisha na uhamasishaji wa kisiasa kwa muda wakisubiri kusikilizwa kwa ombi linalopiga shughuli zao lilowasilishwa Mahakamani na Shirika la Vocal Africa.
Jaji wa Mahakama hiyo David Mburu, alitoa amri hiyo akiagiza kuwa ombi hilo lisikilizwe kwa umakini na washtakiwa wote wawasilishiwe stakabadhi za kesi hii leo.
Katika ombi hilo, Shirika la Vocal Africa linadai kuwa ushiriki wa maspika hao katika shughuli za kisiasa unaibua maswali mazito ya kikatiba kuhusiana na uhuru wa bunge na majukumu yaliyowekwa kwa maafisa wa serikali.
Vocal Africa pia limesisitiza kuwa, ingawa kila ana haki ya kuwa na maoni ya kisiasa na kushiriki katika maswala ya kisiasa, maspika wanashikilia ofisi za kikatiba ambazo hazihitaji upendelea bali zinahitaji uhuru wa kitaasisi.
Kwa muda sasa spika Kingi na Wetangula wameonekana katika mikutano mbalimbali ya kisiasa wakipigia debe ajenda ya rais William Ruto, kinyume na Katiba inayowalazimisha maspika kuangazia masuala ya bunge na shughuli zengine muhimu za kiserikali.
Taarifa ya Elizabeth Mwende

