National News
Shahidi wa 28 na 29 Waelezea Mahakama Masaibu Waliyopitia Shakahola
Kesi inayomhusu Mhubiri tata Paul Mackenzie na wenzake 92 imesikizwa katika Mahakama ya Mombasa, ambapo shahidi wa 28 na 29 wameeleza ushahidi wao Mahakamani.
Shahidi wa 28, ambaye ni mtoto ametoa ushahidi wake katika chumba cha faraga ambapo amesema kwamba alikamatwa na maafisa wa polisi pamoja na familia yake baada ya wazazi wake kuwaachisha shule kutokana na mafunzo ya Mackenzie.
Mtoto huyo ameeleza kwamba baba yake alikuwa akipinga mafunzo ya Mackenzie lakini baadaye alijiunga na kisha kuhamia Shakahola na familia yake ambapo alishuhudia Mackenzie akikusanya watu na kuwaagiza kufunga kula na kunywa, kabla ya kufanikiwa kutoroka hadi kituo cha watoto huko Watamu.
Kwa upande wake Shahidi wa 29, ameiambia Mahakama hiyo kwamba alipoteza watoto wake 7 kutokana na kufunga kula na kunywa, akisema walinzi waliokuwa wakilinda eneo hilo walichukua chakula chake chote kilichokuwa nyumbani kwao.
Shahidi huyo amesema wakati huo alikuwa mjamzito na alilazimika kufunga ili kuua mtoto aliyekuwa tumboni na wafuasi wa Mackenzie walikuwa hawaruhusiwi kuomboleza kifo chochote katika eneo hilo la Shakahola.
Mackenzie na wenzake 92 wanakabiliwa na mashtaka 238 ikiwemo mauaji ya halaiki, ugaidi, mafunzo ya itikadi kali miongoni mwa mashtaka mengine yanayodaiwa kuyatekeleza kati ya mwaka 2020 na 2023 katika msitu wa Shakahola kaunti ya Kilifi.
Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa mbele ya Hakimu mkuu Alex Ithuku.
National News
Umoja wa mataifa wapunguza bajeti yake kwa bola milioni 577
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amependekeza kupunguzwa kwa bajeti ya umoja huo ya mwaka ujao kwa dola milioni 577, hatua ambayo itapunguza asilimia 18 ya kazi.
Akizungumza mbele ya kamati ya bajeti ya Baraza kuu la umoja wa mataifa, Guterres alisema umoja huo bado haujapokea mchango wa karibu dola milioni 900 kutoka kwa wanachama mwaka huu wa 2025.
Umoja wa mataifa unapendekeza bajeti ya dola bilioni 3 kwa mwaka 2026, ikiwa na upungufu wa asilimia 15 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka huu.
Umoja wa Mataifa unakabiliwa na mgogoro wa kifedha uliosababishwa pakubwa na hatua ya Marekani kutolipa ada yake, kutokana na sera mpya za Rais Donald Trump.
Hatua hii ya umoja wa mataifa huenda ukachangia changamoto kubwa kwa mataifa wanachama hasa yanayotegemea pakubwa juhudi za umoja huo katika masuala mbalimbali ikiwemo usalama.
Editor's Picks
Bangi Yanaswa Daraja la Sabaki – Malindi, Kaunti ya Kilifi
Maafisa wa Usalama wamenasa shehena ya Bangi katika daraja la Sabaki, Mjini Malindi Kaunti ya Kilifi, iliyokuwa imefichwa kwenye makasha ndani ya basi lililokuwa likisafiri kitoka Lamu kwenda Mombasa.
Basi hilo lilisimamishwa na Maafisa wa usalama katika kizuizi Cha Polisi kilichoko daraja hilo kwa shughuli ya kawaida ya ukaguzi wa magari na mizigo, ambapo magunia mawili ya bangi hiyo yalipatikana yamefichwa katika sehemu ya Mizigo ndani ya basi hilo.
Dereva na Kondakta wa basi hilo, mali ya kampuni ya mabasi ya Tawakal, walikamatwa, ingawa abiria anayeaminika ndiye mwenye kusafirisha bangi hiyo alitotoka mtego huo na bado anatafutwa na Maafisa Polisi.
Waliokamatwa sasa wanazuiliwa katika kituo cha Polisi cha Mjini Malindi huku uchunguzi zaidi unapoendelea.
Maafisa hao wanasema, walipata vidokezo kuhusiana na bangi hiyo ambayo bado haijajulikana thamani yake.
Katika siku za hivi karibuni, Daraja hilo la Sabaki limekuwa chini ya oparesheni kali ya maafisa wa usalama kutokana kuongezeka Kwa idadi ya vyombo vya usafiri, hasa Malori ambayo yaaminika kutumika kwa zaidi kwa biashara haramu kutoka Kaunti za Tana River na Lamu kuingia Kaunti za Kilifi na Mombasa.
Dereva huyo na Kondakta wake watafikishwa mahakamani hivi karibuni huku maafisa wa Polisi wakitia wito kwa wanachi kutoa habari zitakazosaidia kumtia nguvuni mshukiwa mkuu.

