News
Upasuaji wa maiti wagundua vipande 4 vya risasi kichwani.
Ripoti ya upasuaji wa maiti ya mchuuzi wa barakoa aliyepigwa risasi kwa karibu na maafisa wa polisi wakati wa maandamano jijini Nairobi imebaini kuwa vipande 4 vya risasi vilibaki kwenye ubongo wa mchuuzi huyo Boniface Kariuki Mwangi.
Upasuaji wa maiti uliofanywa Alhamisi Julai 3, 2025 ulibaini kuwa Kariuki alifariki kutokana na majeraha ya kichwa yaliyosababishwa na risasi aliyopigwa na polisi siku hiyo.
Shughuli ya upasuaji huo iliendeshwa na wapasuaji wakiongozwa na daktari wa serikali Bernard Media kwa kushirikiana na daktari wa familia Peter Ndegwa.
Madaktari hao walibaini kuwa vipande vingine viwili viliondolewa na madaktari wakati Mwangi alipokuwa hai.
Uchunguzi huo haukuweza kuthibitisha kwa uhakika wakati halisi wa kifo chake huku madakrati wakieleza kuwa ubongo wa Mwangi huenda ulikuwa umekufa siku kadhaa kabla ya familia kuarifiwa rasmi.
Maafisa wa polisi wanaohusishwa na tukio hilo wanaendelea kuzuiliwa na polisi.
Mwangi alipigwa risasi na polisi wakati wa maandamano ya kushinikiza naibu inspekta wa polisi Eliud Lagat kujiuzulu, kufiatia kifo cha mwanablogu na mwalimu Albert Ojwang’.
Baadaye Lagat alijiondoa ofisini kwa mda ili kupisha uchunguzi kuhusiana na mauaji hayo, japo shinikizo za kuondoka ofisini kabisa ziliendelea kupitia maandamano ya vijana wa kizazi cha Gen Z.
Mwanablogu huyo Ojwang’ atazikwa Julai 4, 2025 nyumbani kwao kaunti ya Homa bay.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

