News
Wataalam wa uchumi samawati wakataa matumizi ya “Ring Net”
Wataalam wa maswala ya uchimi wa bahari nchini wamesistiza marufuku ya uvuvi wa kutumia nyavu aina ya Ring Net wakisema nyavu hizo zinaharibu zao la samaki baharini.
Wakiongozwa na Stanley Chai, wataalam hao walisema nyavu hizo zinafaa kutumika kuanzia umbali wa maili tano baharini kutoka ufuoni hali ambayo wavuvi wa kawaida hapa nchini kwa sasa hawana uwezo wa kufika umbali huo.
Chai alidokeza kuwa nyavu hizo zinapotumika hunasa mayai ya samaki baharini hali inayosambaratisha na kuharibu kizazi cha viumbe hai baharini.
“Watu wetu hawa wavuvi wadogo wadogo wanatumia ndoana, uvuvi wa ring net nitakwambia si uvuvi mzuri hasa kama utakuja kwa maji yasiyo ya kina kirefu, ring net inabeba mpaka mayai ya samaki, ukiona nakala ya sheria zetu ambazo hazijachapishwa kwenye gazeti rasmi la serikali tumesema uvuvi wa ring net uruhusiwe umbali wa maili tano kuendelea na sio chini ya hapo kwa sababu chini ya hapo ndio samaki huzaana”, alisema Chai
Wakati huo huo Chai alisistiza umuhimu wa utekelezaji mpango wa kuingiza samaki nchini kutoka mataifa ya nje ili kuongeza kipato kupitia kodi na kuwezesha wavuvi kwa vifaa bora vya kuendeleza shughuli zao baharini.
“Wale samaki wakubwa tukiwaingiza hapa nchini tusiliseni ile ya dola elfu hamsini, hiyo ni kitu kidogo, yule samaki akiingizwa hapa nchini tunakusanya mabilioni, sasa hizi mabilioni tumesema nini kwa zile nakala ya sheria? tumesema zile pesa zitakazopatikana kwa biashara ya samaki asilimia 70 ziende kwa serikali kuu, asilimia 20 ziende kwa kaunti zinazopakana na bahari hindi, hii asilimia 10 iekezwe kuboresha wavuvi wadogowadogo halafu asilimia 10 ziende kwa vikundi vya maendeleo baharini-BMU, wale wavuvi moja kwa moja wanaweza kununua maboti makubwa nakupata uwezo wa kwenda kule chini”, aliongeza mtaalam Chai.
Kwa mda wavuvi eneo la pwani wamekuwa wakilalamikia serikali kuwafadhili na vifaa vya kisasa vya uvuvi ikiwepo boti zinazostahamili mawimbi baharini ili waweze kufika maji makuu na kuongeza pato la samaki.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

