Sports
Bandari Youth Watetea Ubingwa wa Pwani huku Free Nation na Jackals Waking’ara BingwaFest Kwale
Mabingwa watetezi Bandari Youth walithibitisha ubabe wao katika toleo la Pwani la mashindano ya Betika BingwaFest baada ya kuichapa SS Assad mabao 3–0 katika fainali ya soka ya wanaume iliyochezwa Uwanja wa Kwale, na hivyo kutetea taji lao kwa kishindo.
Baada ya mwanzo wa mchezo uliokuwa na ushindani wa karibu, Bandari Youth walifungua ukurasa wa mabao dakika ya 35 kupitia penalti iliyofungwa kwa ustadi na Don Otieno. Kipindi cha pili kilishuhudia mabingwa hao wakiongeza kasi, Steve Giragwa akifunga bao la pili dakika ya 58 kabla ya Mohamed Chaka kukamilisha ushindi huo kwa bao la tatu dakika ya 85.
Katika fainali ya wanawake, Ukunda Vision Starlets walitwaa ubingwa baada ya ushindi mwembamba wa bao 1–0 dhidi ya Kayatiwi Girls. Bao pekee la Patience Kasichana katika kipindi cha kwanza lilitosha kuipa Ukunda ushindi huo, huku wakionyesha uimara wa ulinzi hadi mwisho wa mchezo.
Kwa ushindi huo, Bandari Youth na Ukunda Vision Starlets walijinyakulia Shilingi milioni 1 kila mmoja. SS Assad na Kayatiwi Girls walipokea Shilingi 500,000 kila mmoja, huku washindi wa nafasi ya tatu, Kombani Youth FC na Ocean D Ladies, wakipata Shilingi 250,000 kila mmoja.
Katika mpira wa kikapu wa 3×3, Free Nation walifanikiwa kutetea taji lao la wanaume baada ya kuishinda Elites 21–16 katika fainali iliyokuwa na ushindani mkali. Kwa upande wa wanawake, Board Protector walitwaa ubingwa kwa ushindi wa 20–12 dhidi ya Wolverines.
Katika mechi za kuwania nafasi ya tatu, Bags waliishinda Reign kwa alama 15–13 katika kitengo cha wanawake, huku Akatsuki wakimaliza wa tatu kwa wanaume baada ya kuilaza Mtu Nne Bora kwa alama 22–11.
Free Nation na Board Protector walizawadiwa Shilingi 500,000 kila mmoja, Elites na Wolverines wakipokea Shilingi 250,000 kila mmoja, huku Bags na Akatsuki wakiondoka na Shilingi 100,000 kila mmoja.
Katika mchezo wa raga, ilikuwa ni siku ya Jackals waliotwaa mataji ya wanaume na wanawake. Timu ya wanawake ya Jackals iliwashinda Shanzu Queens kwa alama 5–3, huku wanaume wao wakiishinda Mombasa Sports Club Rugby kwa alama 26–14.
Kwa nafasi ya tatu, Migodi Leigh walishinda katika kitengo cha wanawake baada ya kuibuka na ushindi wa 3–0 dhidi ya TUM Marines Women, huku Behta Rugby wakichukua nafasi ya tatu kwa wanaume kwa kuichapa TUM Marines Men 26–0.
Jackals Men na Jackals Women walipokea Shilingi milioni 1 kila mmoja, wakati Mombasa Sports Club Rugby na Shanzu Queens wakizawadiwa Shilingi 500,000 kila mmoja. Migodi Leigh na Behta Rugby walijinyakulia Shilingi 250,000 kila mmoja baada ya kumaliza katika nafasi ya tatu.
Akizungumza katika Uwanja wa Kwale, Mkuu wa Chapa wa Betika, Eric Mwiti, alisema wana fahari kubwa kuona mafanikio ya msimu wa pili wa BingwaFest, akibainisha kuwa ushindani ulikuwa mkali na ushiriki wa jamii umeongezeka.
Aliongeza kuwa fainali za kitaifa zitafanyika katika eneo litakalochaguliwa kwa njia ya droo ili kuhakikisha uwazi na usawa, huku Kisumu iliyoandaa fainali za kwanza ikiondolewa kwenye mchakato huo ili kutoa nafasi kwa eneo jingine kunufaika na mashindano hayo ya kitaifa.
Sasa macho yote yanaelekezwa kwenye fainali za kitaifa, ambapo mabingwa kutoka kanda mbalimbali watakutana kuwania ubingwa wa jumla.
Sports
Wakili George Kithi akabidhiwa rasmi Cheti cha uenyekiti wa bodi ya Michezo marufu kama Sports Arts and Social Development Fund (SASDF)
Waziri wa Wizara ya Masuala ya Vijana, Uchumi bunifu na Michezo, Salim Mvurya, ameshudia hafla rasmi ya kukabidhiwa uenyekiti wa Bodi ya Sports, Arts and Social Development Fund (SASDF) kutoka kwa Luteni Jenerali Mstaafu Jackson Tuwei kwenda kwa Mheshimiwa wakili George Kithi. Hafla hiyo ilifanyika, jijini Nairobi hii leo.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Mvurya alimpongeza Luteni Jenerali (Mstaafu) Tuwei kwa uongozi wake wa mfano na kujitolea kwake katika kipindi chake cha utumishi. Alibainisha kuwa chini ya uongozi wake, bodi hio iliimarika na kuwa taasisi imara na yenye mwitikio zaidi katika kusaidia na kuendeleza vipaji vya Wakenya.
Aidha, Waziri alieleza imani yake kwa uongozi wa Mheshimiwa wakili George Kithi, akimhakikishia ushirikiano na msaada kamili kutoka kwa Wizara katika kutekeleza majukumu ya Bodi kwa kipindi chake cha miaka mitatu.
SASDF inaendelea kuwa nguzo muhimu katika kulea na kukuza vipaji vya Kenya, pamoja na kuimarisha hadhi ya nchi kimataifa kupitia michezo na uchumi wa ubunifu. Kupitia uwezeshaji wa wanamichezo, wasanii na wadau wa utamaduni, mfuko huo unachangia pakubwa katika ukuaji wa sekta za michezo na ubunifu nchini.
Sports
Bingwa wa dunia mbio za mitaa 1500 Faith Kipyegon ateuliwa kuwania tuzo za kila mwaka za ‘Laureus World Sportswoman of the Year.’
Nyota wa mbio za masafa ya kati kutoka Kenya, Faith Kipyegon, amepata uteuzi wake wa tatu mfululizo kuwania tuzo ya Mwanamichezo Bora wa Kike wa Mwaka katika hafla maarufu ya Laureus World Sports Awards, hatua inayozidi kuthibitisha ubabe wake katika kizazi hiki cha wanariadha.
Tuzo hizo, zinazotambuliwa kimataifa kama “Oscars za Michezo”, huandaliwa na Laureus Sport for Good Foundation na hulenga kutambua mafanikio ya kipekee, uthabiti na mchango chanya wa michezo duniani.
Uteuzi wa Kipyegon kwa miaka mitatu mfululizo unaonyesha si tu kipaji chake, bali pia uimara wa kiwango chake cha juu kwa muda mrefu. Mwaka 2024 aliteuliwa baada ya msimu wa kihistoria wa 2023 ambapo alivunja rekodi tatu za dunia na kushinda dhahabu mbili katika Mashindano ya Dunia.
Mwaka 2025 alirejea tena kwenye orodha ya wateule kufuatia mafanikio makubwa katika Michezo ya Olimpiki ya Paris, ambako aliweka historia kwa kuwa mwanamke wa kwanza kushinda medali tatu za dhahabu mfululizo katika mbio za mita 1,500.
Sasa mwaka 2026, anawania tuzo hiyo tena baada ya kuvunja rekodi yake mwenyewe ya dunia ya mita 1,500 na kutwaa taji lake la nne la dunia katika msimu bora wa 2025.
Katika kinyang’anyiro cha mwaka huu, Kipyegon anakutana na ushindani mkali kutoka kwa nyota wengine wa kimataifa akiwemo Sydney McLaughlin-Levrone, Melissa Jefferson-Wooden, Aitana Bonmati, Aryna Sabalenka, na Katie Ledecky.
Uteuzi huu unaendeleza hadhi ya Kipyegon kama mmoja wa wanariadha bora zaidi duniani na fahari kubwa kwa Kenya katika jukwaa la kimataifa.

