News
Wakimbizi nusu milioni wakabiliwa na baa la njaa, Dadaab
Ripoti iliyotolewa hivi karibu na Shirika la Chakula duniani WFP ilionyesha kwamba zaidi ya wakimbizi nusu milioni wanaoishi katika kambi za wakimbizi za Kakuma na Dadaab zilizoko nchini Kenya, wako katika hatari ya kuangamia kutokana na baa la njaa.
Kambi hizi ambazo zinahifadhi wakimbizi wengi zaidi kutoka nchini Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Somalia, ziko hatari iwapo zitakosa misaada ya chakula.
Kufuatia hali hiyo ambayo pia imechangiwa na mashirika ya kimataifa kusitisha ufadhili, sasa hali huenda ikawa tofauti baada ya taifa la Korea kwa ushirikiano na Kenya kutoa ufadhili wa shehena ya nafaka ya zaidi ya tani elfu 10 ambayo inakadiriwa kuwa kima cha shilingi milioni 1.2.
Katibu katika Idara ya uhamiaji nchini Belio Kipsang, aliyepokea msaada huo wa Chakula mjini Mombasa na kuhifadhiwa katika maghala ya Shirika la WFP, ameonya kwamba iwapo Kenya itakosa kupokea msaada kutoka kwa washirika na wafadhili wengine, basi italazimika kuchukua maamuzi magumu, ikiwemo kuwaondoa baadhi ya wakimbizi.
“Nyuma ya kila takwimu kuna familia ambazo ustahimilivu wao unaendelea kujaribiwa kila siku: akina mama wanaokosa kula ili watoto wao wapate chakula, watu walio katika mazingira hatarishi wakiruka milo, na vijana wanaokabiliwa na mustakabali usio na uhakika. Hizi si takwimu za kufikirika. Zinawakilisha watu halisi ambao heshima yao, afya yao na matarajio yao ya maisha yanategemea maamuzi tunayofanya kwa pamoja,” alisema.
Wakati wa hafla hiyo ya kupokea msaada huo wa chakula kwa wakimbizi wa Kakuma na Dadaab, Mkurugenzi wa Shirika la WFP nchini Kenya Betty Ka, alisema shehena ya nafaka itasaidia kuwahudumia takribani wakimbizi nusu milioni katika miezi ijayo.
“Usafirishaji huu unaonyesha umuhimu wa ushirikiano imara katika mnyororo wa ugavi wa misaada ya kibinadamu, ambapo ushirikiano huu kati ya Kenya, Mamlaka ya bandari Kenya (KPA), Shirika la viwango la Kenya(KEBS) na mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa kuhakikisha kwamba chakula cha msaada kinafanikishwa”,alisema Betty.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Aisha Jumwa akihama rasmi chama cha UDA
Mgombea wa kiti cha ugavana wa kaunti ya Kilifi Aisha Jumwa amekihama rasmi chama cha UDA, akisema atatangaza baadaye mwelekeo atakaochukua wa kisiasa.
Jumwa alitoa tangazo hilo katika kikao na Wanahabari kilichofanyika katika makaazi yake, eneo la Kakuyuni huko Malindi kaunti ya Kilifi leo siku ya Alhamis.
Hatua ya Jumwa ilijiri baada ya kuwepo na tetesi kwamba alikuwa na mipango ya kuhama chama hicho kutokana na sintofahamu za kisiasa ndani ya chama cha UDA kuhusu msimamo wake wa kisiasa wa kuwania nafasi ya ugavana wa Kilifi.
Hii sio mara ya kwanza kwa Jumwa kukihama Chama cha UDA na kurejea kwenye chama hicho, lakini hatua aliyoichukua sasa itabadili masimamo wa kisiasa kaunti ya Kilifi.
Itakumbukwa kwamba Jumwa amekuwa mwandani wa karibu wa rais William Ruto, lakini hatua aliyoichukua huenda ikabadili msimamo wa kisiasa kaunti ya Kilifi na Pwani kwa jumla.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Mahakama ya Kilifi yaagiza kuzuiliwa Washukiwa 7 wa mauaji
Mahakama ya Kilifi imeagiza kuzuiliwa kwa siku 14 washukiwa 7 wanaotuhmiwa kuhusika katika kifo cha mwanamke mmoja aliyekuwa na umri wa miaka 65, ambaye aliuwawa kwa tuhma za uchawi katika eneo la Malomani eneo bunge la Ganze kaunti ya Kilifi.
Washukiwa hao Gilbert Karisa Changawa, Selvestar Changawa Kahindi, Elizabeth Jackson Ngala, Dhahabu Kithi Kombe, Dzendere Palu Kalama, Agness Changawa na Kadzo Ngombo Bienge watazuiliwa katika kituo cha Bamba wakati uchunguzi ukiendelea.
Kulingana na Afisa mpelelezi kutoka kitengo cha DCI ameeleza mahakama kwamba ilikuwa mnamo tarehe 27 mwezi huu ambapo walipokea tarifa kwamba dama changawa alikuwa amekatwa kichwa na kuuwawa na watu wasiojulikana usiku huo.
Afisa mpelelezi pia ameeleza kuwa washukiwa ambao ni wanafamilia,siku kabla ya tukio husika walikuwa wameandaa kikao cha kudumisha Amani baada ya kifo kilichokuwa kimetokea kwa kijana mmoja mtoto wa mmoja kati ya washukiwa aliyefariki kaunti ya Mombasa baada ya kupigwa kwa tuhma za wizi.
Kutokana na kifo cha kijana huyo wanafamilia hao walimtuhmu dama kwamba ndiye aliyekuwa amemroga kijana huyo na kusababisha kifo hicho cha gafla, ambapo usiku huo Dama aliuwawa nyumbani kwake.
Washukiwa watarudishwa mahakamani tarehe 13 mwezi Agosti mwaka huu baada ya uchunguzi kukamilika.
Taarifa ya Teclar Yeri

