News
Wakimbizi nusu milioni wakabiliwa na baa la njaa, Dadaab
Ripoti iliyotolewa hivi karibu na Shirika la Chakula duniani WFP ilionyesha kwamba zaidi ya wakimbizi nusu milioni wanaoishi katika kambi za wakimbizi za Kakuma na Dadaab zilizoko nchini Kenya, wako katika hatari ya kuangamia kutokana na baa la njaa.
Kambi hizi ambazo zinahifadhi wakimbizi wengi zaidi kutoka nchini Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Somalia, ziko hatari iwapo zitakosa misaada ya chakula.
Kufuatia hali hiyo ambayo pia imechangiwa na mashirika ya kimataifa kusitisha ufadhili, sasa hali huenda ikawa tofauti baada ya taifa la Korea kwa ushirikiano na Kenya kutoa ufadhili wa shehena ya nafaka ya zaidi ya tani elfu 10 ambayo inakadiriwa kuwa kima cha shilingi milioni 1.2.
Katibu katika Idara ya uhamiaji nchini Belio Kipsang, aliyepokea msaada huo wa Chakula mjini Mombasa na kuhifadhiwa katika maghala ya Shirika la WFP, ameonya kwamba iwapo Kenya itakosa kupokea msaada kutoka kwa washirika na wafadhili wengine, basi italazimika kuchukua maamuzi magumu, ikiwemo kuwaondoa baadhi ya wakimbizi.
“Nyuma ya kila takwimu kuna familia ambazo ustahimilivu wao unaendelea kujaribiwa kila siku: akina mama wanaokosa kula ili watoto wao wapate chakula, watu walio katika mazingira hatarishi wakiruka milo, na vijana wanaokabiliwa na mustakabali usio na uhakika. Hizi si takwimu za kufikirika. Zinawakilisha watu halisi ambao heshima yao, afya yao na matarajio yao ya maisha yanategemea maamuzi tunayofanya kwa pamoja,” alisema.
Wakati wa hafla hiyo ya kupokea msaada huo wa chakula kwa wakimbizi wa Kakuma na Dadaab, Mkurugenzi wa Shirika la WFP nchini Kenya Betty Ka, alisema shehena ya nafaka itasaidia kuwahudumia takribani wakimbizi nusu milioni katika miezi ijayo.
“Usafirishaji huu unaonyesha umuhimu wa ushirikiano imara katika mnyororo wa ugavi wa misaada ya kibinadamu, ambapo ushirikiano huu kati ya Kenya, Mamlaka ya bandari Kenya (KPA), Shirika la viwango la Kenya(KEBS) na mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa kuhakikisha kwamba chakula cha msaada kinafanikishwa”,alisema Betty.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Mbunge wa Nyali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila
Mbunge wa Nyali kaunti ya Mombasa Mohamed Ali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila kwenye kaunti hiyo, akisema anafanya siasa zake bila kujali dini, kabila au hata eneo.
Akizungumza huko Nyali, Ali alisema kuna baadhi ya viongozi katika kaunti ya Mombasa, ambao wamekuwa wakiendekeza propaganda za kumhusisha na siasa za migawanyiko ili kumharibia jina taifa linapojiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao wa 2027.
Ali ambaye alitangaza kuwania wadhifa wa ugavana kaunti ya Mombasa, aliwataka viongozi kufanya siasa zao kwa kunadi sera zao kwa wakaazi na maendeleo ambayo watatekeleza na sio kutumia suala la ukabila kuwachafulia wengine jina.
“2017 hakuna mtu aliniita mkabila, 2022 hakuna mtu aliniita mkabila, 2027 wanasema Mohamed Ali ni mkabila.Mimi Mohamed Ali, mimi nauliza nikisimama hapa juu ya gari, niseme kabila zote za Kenya wanaweza pewa nafasi ya ugavana ni kuna makosa?,basi sasa wanazunguka wakisema Mohamed ni mkabila kwasababu ameanza kufungua watu macho’’ alisema Ali.
Aidha, Ali alisema ataendelea kuzuru maeneo mbalimbali ya kauti ya Mombasa kunadi sera zake na kuwataka wakaazi wa kaunti hiyo kuwachagua viongozi wanaofaa ambao wataimarisha kaunti hiyo kimaendeleo.
‘’Mimi nimewaambia nitatembea hii Mombasa kwa uwezo wake mwenyezi mungu kutetea wananchi wa Mombasa’’ aliongeza Ali
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Vifo vya Wanawake wajawazito Kilifi
Kaunti ya ni Kilifi ni miongoni mwa kaunti ambazo ziko na Idadi kubwa ya vifo vya wanawake wajawazito wanaofariki dunia wakati wa kujifungua pamoja na vile vya watoto wachanga.
Katika kikao ambacho kiliwaleta pamoja waandishi wa habari, hafla ambayo ilfanyika katika ukumbi wa kibaoni mjini Kilifi, kupitia wakfu wa Shina ilibainika visa hivyo vinachangiwa na ukosefu wa hamasa kwa akina mama wajawazito hasa walioko mashinani kuhusu umuhimu wa kula lishe bora, kutokuhudhuria kliniki kutokana na mila na tamaduni na pia hali ya umasikini.
Akizungumzia hilo Nazi Kivutha ambaye ni mwanzilishi wa wakfu wa Shina alisema kando na ukosefu wa ufahamu huo wa akina mama kuhusu uzazi usalama kaunti ya Kilifi hamasa za kutosha hazijatolewa ipasavyo maeneo ya mashinani.
“Hapa kaunti ya Kilifi viwango vya umasikini viko juu na hilo linawafanya wanawake wengi kushindwa kumudu lishe bora na pia wengi wao bado wamekumbatia mila na tamaduni na ndio maana wanaamini kukandwa na wakunga na kupuuza kuhudhuria kliniki ili kujifungua Salama” alisema Bi Kivutha
Kwa upande wake Winnie Barawa alisema baadhi ya wanawake wajawazito wanafariki dunia kutokana ukosefu wa damu mwilini hali ambayo inachangia kwa vifo hivyo na kuwataka kuzingatia ulaji wa vyakula bora na pia kuhudhurikia kliniki mara kwa mara.
“Utapata wengi kiwango chao damu kiko chini mno hali ambayo inawaweka mama na mtoto katika hatari ya kufariki dunia” alisema Winnie Barawa.
Hata hivyo walisema kupitia mradi wa okoa mama na mtoto chini ya wakfu wa Shina mikakati inaendelea kuwekwa ili kudhibiti vifo hivyo.
Haya yanajiri miezi michache baada ya mratibu wa huduma ya afya kaunti ya Kilifi Edward Mumbo kutoa takwimu hizo zikiwemo zile za watoto njiti
Taarifa ya Janet Mumbi

