News
Jeremiah Kioni: Gachagua anafanyakazi kisiri na rais Ruto
Katibu Mkuu wa chama cha Jubilee Jeremiah Kioni amedai kuwa aliyekuwa naibu Rais Rigathi Gachagua anafanya kazi na rais William Ruto kisiri.
Kulingana na Kioni, Gachagua alikutana na viongozi katika kaunti ya Narok katika tarehe ambayo haijatajwa, ambapo alijaribu kueleza ni kwa nini chama cha DCP kilikuwa kinamnyima muaniaji wa wadi ya Narok mjini Joshua Ole Kaputa tiketi ya chama hicho kwenye uchaguzi mdogo ujao.
Kioni alidokeza kwamba mkutano huo ulikuwa na wanachama 15, miongoni mwao wakiwemo makasisi na kwamba kulikuwa na mpango uliowekwa kati yake na rais Ruto na Joshua angeteuliwa baadaye.
“Gachagua aliwaambia kuwa William Ruto tayari ametuma wajumbe kwao na walikuwa na mpango wa kuweka vyama vyao katika hali ya udhabiti kisha wakutane kujadiliana,” alidai Kioni.
Kioni hata hivyo alikana kufichua maelezo zaidi kuhusu mkutano huo wa siri, akisema “Alijieleza mwenyewe”.
Alishikilia kuwa chama cha Jubilee kiko tayari kufanya kazi na vyama vyenye nia moja na hakitashirikiana na yeyote anayehusika na mikataba mibaya ya kisiasa.
“Tungependa kufanya kazi na vyama vyenye nia moja ambavyo vinaamini katika kumbandua rais William madarakani “pata watu wako na mimi nipate wangu”, alibainisha Kioni.
Wakati huo huo aliwataka vijana kujiandikisha kuwa wapiga kura kwenye zoezi la usajili endelevu lililoanza rasmi Septemba 29, 2025
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

