News
Murkomen: Serikali Kubuni Kitenga Maalum Kuchunguza Mizozo ya Ardhi Pwani
ARDHI-
Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen amesema serikali inalenga kubuni kitenga maalum cha maafisa wa usalama watakaochunguza mizozo ya ardhi katika eneo la Pwani.
Katika kikao na Wanahabari, Waziri Murkomen amesema hatua hiyo itahakikisha ardhi zote zenye mizozo zinatatuliwa kwa usawa kwani idadi kubwa ya wakaazi wa Pwani wamekuwa wakihangaishwa katika ardhi zao.
Murkomen amesema Wizara ya usalama kwa ushirikiano na ile ya ardhi nchini na jamii mashinani watahakikisha utata huo unapata suluhu la kudumu sawa na kuwawezesha wananchi kupata hati miliki za ardhi zao.
Wakati huo huo amedokeza kwamba analenga kubuni sera maalum itakayosaidia kuajiri maafisa wa usalama kila mwaka ili kuimarisha usalama wa taifa huku akiwaonya wakenya dhidi ya kushiriki ufisadi wakati wa zoezi la kusajili makurutu.
Waziri Murkomen yuko katika ukanda wa Pwani kwa ziara ya wiki moja kutathmani maswala ya kiusalama ambapo alianza na kaunti ya Mombasa kisha kaunti ya Kwale, Kilifi, Lamu, Tanariver na kaunti ya Taita taveta kabla ya kukamilisha ziara hiyo.
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

