News
Ofisi ya ODPP imehitimisha rasmi kesi ya Mackenzie
Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) imehitimisha rasmi kesi yake dhidi ya mauaji ya Shakahola, ambapo Mhubiri tata Paul Mackenzie na wenzake 35 wanakabiliwa na mashtaka ya unyanyasaji, mateso na ukiukaji wa haki za watoto.
Kesi hiyo inayoendelea katika Mahakama ya watoto ya Tononika jijini Mombasa mbele ya Hakimu mkuu Nelly Chepchirchir ilianza mnamo tarehe 24 Julai 2024, na kukamilika ramsi kwa uwasilishaji wa mashahidi kutoka upande wa mashtaka.
Upande wa mashtaka ukiongozwa na Mkurugenzi msaidizi wa mashtaka ya umma, Jami Yamina, Victor Owiti, Betty Rubia, Biasha Khalifa, na Eunice Odongo katika kipindi cha kesi, waliwasilisha mashahidi 75 ambao walieleza vitendo vya unyanyasaji, mateso, na kukataliwa kwa haki ya elimu, ambayo yalifanyika katika Shakahola.
Mashahidi watatu akiwemo mtaalamu wa uchambuzi wa data kutoka kampuni ya mawasiliano ya Safaricom Dennis Muriithi walitoa ushahidi wao Mahakamani.
Muriithi amethibitisha kwamba baada ya kupata agizo kutoka kwa Mahakama walifanikiwa kufuatilia namba za simu zinazomilikiwa na Mackenzie, na kutoa taarifa za muhimu kwa uchunguzi.
Shahidi mwengine Israel Veronica, mwenye umri wa miaka 21 kutoka Chakama, mjini Malindi, ameelezea jinsi alivyolazimishwa na baba yake kuacha shule mwaka 2019, na baadaye familia yao ikahama kutoka Nairobi hadi Shakahola baada ya kuuza mali zao.
Naye Inspekta Phoebe Okomo kutoka Kitengo cha Ulinzi wa Watoto cha DCI Mombasa amesimulia kuhusu uokoaji wa watoto 27 kutoka Malindi, akielezea mazingira magumu waliyokuwa nayo watoto hao wakiwa Shakahola, ikiwemo kukosa chakula, kuteswa, na kupigwa.
Kesi hiyo itajadiliwa tena tarehe 14 Oktoba 2025 kwa ajili ya kuthibitisha kama maandiko ya kesi yameandikwa kwa ajili ya kuwasilishwa Mahakamani.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Wajumbe wa bunge la Seneti wazuru kaunti ya Kilifi
Baadhi ya wajumbe wa bunge la Seneti chini ya mpango wa Seneti mashinani wamefanya ziara katika majengo ya bunge la kaunti ya Kilifi na kupokelewa na Karani wa bunge hilo Michael Ngala.
Wajumbe hao wa sekta mbalimbali wa bunge la Seneti wakiongozwa na Daniel Chania, wametathmini masuala mbalimbali ya bunge la kaunti ya Kilifi kama lina uwezo wa kuandaa ziara ijayo ya Seneti mashinani.
Seneti Mashinani ilianzishwa chini ya kifungu cha 126 ibara ya kwanza ya Katiba ya Kenya ya mwaka 2010, kinachoruhusu kikao cha bunge lolote kufanyika mahali popote ndani ya taifa la Kenya na kuanza wakati wowote kitakapopangwa na bunge.
Malengo ya vikao hivyo katika kaunti ni pamoja na kuhamasisha umma kuhusu kazi za bunge na Seneti, kuimarisha ushiriki wa umma katika shughuli za Seneti kwenye ngazi ya kaunti sawa na kutoa hamasa kwa wananchi kwa lengo la kuhimiza ushiriki umma katika utawala.

Baadhi ya wajumbe wa bunge la Seneti chini ya mpango wa Seneti mashinani wamefanya ziara katika majengo ya bunge la kaunti ya Kilifi
Bunge la Seneti limeanza maandalizi ya vikao vitakavyofanyika nje ya Nairobi, ambavyo vinatarajiwa kufanyika mwezi Septemba 2026.
Kaunti ya Kilifi ni miongoni mwa kaunti zilizoteuliwa kuwa kati ya zile zitazoandaa vikao hivyo kwa ajali ya umma kuwa na uelewa zaidi kuhusu shughuli za bunge hilo.
Wajumbe hao walikuwa na malengo pia ya kubaini upatikanaji wa miundombinu na huduma muhimu ili kuiwezesha Seneti kufanya uamuzi.
Kaunti nyingine zilizowahi kuandaa Seneti Mashinani ni pamoja na kaunti ya Uasin Gishu mwaka 2018, ikifuatiwa na kaunti ya Kitui mwaka 2019, kaunti ya Turkana mwaka 2023 na kaunti ya Busia mwaka 2025.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Sakata ya mafuta yaathiri sekta ya uchukuzi nchini
Huenda watumizi wa magari ya uchukuzi wa umma, wahudumu wa tuktuk na bodaboda wakalazimika kuongeza nauli kwa abiria kutokana na changamoto za ukosefu wa mafuta nchini na kuathiri zaidi shughuli za uchukuzi.
Hatua hii imetakana na changamoto za uhaba wa mafuta nchini baada ya kuibuka kwa sataka ya uagizaji wa mafuta ghushi kupitia bandari ya Mombasa.
Kulingana na serikali kupitia Wizara ya Kawi, sakata hiyo ya shilingi bilioni 12 ilikuwa imelata tani elfu 60 za mafuta ya petroli kinyume cha sheria pamoja na mipango ya serikali ya uagizaji mafuta wa serikali kwa serikali yaani G to G.
Sakata hii imepelekea Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya kudhibiti kawi na bei za mafuta nchini EPRA Daniel Kiptoo, Katibu katika Idara ya petroli nchini Mohammed Liban na mkurugenzi wa Kampuni ya Kenya Pipeline Joe Sang kujiuzulu.
Kujiuluzu kwao kumetokana na kukamatwa na maafisa wa idara ya upelelezi wa jinai nchini DCI, kwa ushirikiano na Tume ya maadili na kupambana na ufisadi nchini EACC baada ya kutilia shaka zabuni iliyopewa kampuni binafsi ya One Petroleum Limited inayomilikwa na mfanyibiashara mashuhuri jijini Mombasa.

Wahudumu wa sekta ya bodaboda wakikabiliwa na changamoto za uhaba wa mafuta ya Petroli
Siku ya Jumanne, Waziri wa Kawi nchini Opiyo Wandanyi alifanya kikao na wakurugenzi wa kampuni za mafuta nchini na kuagiza shehena ya mafuta katika bandari ya Mombasa kurejeshwa kwani serikali haitambua shehena hiyo.
“Wahusika wa sakata hiyo walikuwa na njama ya kuongeza bei ya mafuta nchini kwa shilingi 14 zaidi kwa lita wakitumia nafasi ya vita vinavyoendelea kati ya Iran na Marekani na Israel, hiyo hatuta kubali”, alisema Wandayi.
Hatua hiyo ilikuwa inalenga pia kukwepa mpango wa serikali wa uagizaji mafuta kutoka mataifa ya miliki za kiarabu wa serikali kwa serikali yaani G to Go, akisema wahusika wa sakata ya ufisadi ni lazima wachukuliwe hatua.
Itakumbukwa kwamba rais William Ruto hivi majuzi alidokeza kwamba wahusika wote wa sakata ya ufisadi kwenye sekta ya mafuta watachukuliwa hatua, akishililia kwamba serikali haitakubali ufisadi nchini, huku akikosa kuweka wazi hatma ya maafisa hao wakuu wa serikali.
“Hawa walaghai wa mambo ya mafuta watakipata, hawaweze kuhepa kwa sababu haiwezekani katika taifa letu la Kenya watu wanaone tuko na shida ya mashariki ya kati wanakuja kukoroga shida nyengine hapa Kenya, serikali itakabiliana kikamilifu na wafisadi”, alisema Rais Ruto.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

