News
Ripoti ya upasuaji wa maiti yabainisha kilichomuua polisi,Haiti
Upasuaji wa maiti ya Kennedy Mutuku Nzuve afisa wa polisi aliyefariki nchini Haiti umebaini kuwa alifariki kutokana na majeraha yanayoambatana na ajali ya barabarani.
Upasuaji wa mwili ulifanyika siku moja baada ya mwili wa afisa huyo kurejeshwa nchini Kenya kutoka nchini Haiti.
Mwili wa afisa huyo ulipokewa na familia yake katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa JKIA jijini Nairobi mwendo wa saa tatu jioni siku ya Ijumaa Septemba 26, 2025.
Nzuve alifariki Agosti tarehe 31 kwenye doria ya usalama nchini Haiti, na sasa familia yake inasema hatua ya mwili wa Nzuve kurejeshwa nchini imeleta afueni.
Nzuve ni miongoni mwa maafisa watatu wa polisi wa Kenya waliofariki wakiwa kwenye oparesheni nchini Haiti, katika mpango wa kimataifa wa usaidizi wa usalama unaoungwa mkono na umoja wa kimataifa.
Awali kuliibuka mkanganyiko kuhusu hatma ya afisa mwengine wa polisi Benedict Kabiru ambaye alikuwa miongoni mwa mafisa waliopelekwa nchini Haiti.
Mkuu wa sheria aliiambia mahakama kuwa hana ufahamu kuwa afisa huyo wa polisi alifariki dunia nchini Haiti, kinyume na matamshi ya rais William Ruto katika kikao cha baraza la umoja wa mataifa jijini New York nchini Marekani.
Kabiru, aliyetumwa nchini Haiti chini ya ujumbe wa msaada wa usalama wa kimataifa (MMS) alishukiwa kuuawa na magenge yenye silaha mnamo mwezi machi 2025.

Maafisa wa polisi wa Kenya wakishika doria nchini Haiti.(picha kwa hisani)
Miezi kadhaa baadaye, huduma ya kitaifa ya polisi nchini ilikuwa bado haijathibitisha kifo chake, ikisema juhudi za kumtafuta zingali zinaendelea.
Familia ilifika mahakamani ikitaka maelezo, ikidai maelezo hayo alizuiliwa na maafisa kutoka ofisi ya mwanasheria mkuu.
Mawakili wanaowakilisha familia hiyo, Jumatano 25, Septemba 2025, waliambia mahakama kwamba kukiri hadharani kwa Rais William Ruto kuwa Kabiru alikuwa miongoni mwa maafisa waliofariki Haiti, kunachukuliwa kuwa ushahidi.
“Ikiwa taarifa ya rais ni sahihi, basi inatupilia mbali ombi la habari kwa kuwa uthibitisho tayari umefanywa katika ngazi ya juu,” mahakama ilisikiza.
Wakati rais Ruto alitoa taarifa kwa umma katika mkutano wa Umoja wa Mataifa, Mwanasheria mkuu alisisitiza kuwa haijapokea taarifa kama hizo kutoka kwa utawala wa polisi.
Mkanganyiko huu, walalamishi walipinga na kusema ni madai ambayo yanahitaji ufafanuzi wa haraka.
Hata hivyo mkuu wa sheria aliomba muda zaidi ili kupata taarifa zaidi.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Wajumbe wa bunge la Seneti wazuru kaunti ya Kilifi
Baadhi ya wajumbe wa bunge la Seneti chini ya mpango wa Seneti mashinani wamefanya ziara katika majengo ya bunge la kaunti ya Kilifi na kupokelewa na Karani wa bunge hilo Michael Ngala.
Wajumbe hao wa sekta mbalimbali wa bunge la Seneti wakiongozwa na Daniel Chania, wametathmini masuala mbalimbali ya bunge la kaunti ya Kilifi kama lina uwezo wa kuandaa ziara ijayo ya Seneti mashinani.
Seneti Mashinani ilianzishwa chini ya kifungu cha 126 ibara ya kwanza ya Katiba ya Kenya ya mwaka 2010, kinachoruhusu kikao cha bunge lolote kufanyika mahali popote ndani ya taifa la Kenya na kuanza wakati wowote kitakapopangwa na bunge.
Malengo ya vikao hivyo katika kaunti ni pamoja na kuhamasisha umma kuhusu kazi za bunge na Seneti, kuimarisha ushiriki wa umma katika shughuli za Seneti kwenye ngazi ya kaunti sawa na kutoa hamasa kwa wananchi kwa lengo la kuhimiza ushiriki umma katika utawala.

Baadhi ya wajumbe wa bunge la Seneti chini ya mpango wa Seneti mashinani wamefanya ziara katika majengo ya bunge la kaunti ya Kilifi
Bunge la Seneti limeanza maandalizi ya vikao vitakavyofanyika nje ya Nairobi, ambavyo vinatarajiwa kufanyika mwezi Septemba 2026.
Kaunti ya Kilifi ni miongoni mwa kaunti zilizoteuliwa kuwa kati ya zile zitazoandaa vikao hivyo kwa ajali ya umma kuwa na uelewa zaidi kuhusu shughuli za bunge hilo.
Wajumbe hao walikuwa na malengo pia ya kubaini upatikanaji wa miundombinu na huduma muhimu ili kuiwezesha Seneti kufanya uamuzi.
Kaunti nyingine zilizowahi kuandaa Seneti Mashinani ni pamoja na kaunti ya Uasin Gishu mwaka 2018, ikifuatiwa na kaunti ya Kitui mwaka 2019, kaunti ya Turkana mwaka 2023 na kaunti ya Busia mwaka 2025.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Sakata ya mafuta yaathiri sekta ya uchukuzi nchini
Huenda watumizi wa magari ya uchukuzi wa umma, wahudumu wa tuktuk na bodaboda wakalazimika kuongeza nauli kwa abiria kutokana na changamoto za ukosefu wa mafuta nchini na kuathiri zaidi shughuli za uchukuzi.
Hatua hii imetakana na changamoto za uhaba wa mafuta nchini baada ya kuibuka kwa sataka ya uagizaji wa mafuta ghushi kupitia bandari ya Mombasa.
Kulingana na serikali kupitia Wizara ya Kawi, sakata hiyo ya shilingi bilioni 12 ilikuwa imelata tani elfu 60 za mafuta ya petroli kinyume cha sheria pamoja na mipango ya serikali ya uagizaji mafuta wa serikali kwa serikali yaani G to G.
Sakata hii imepelekea Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya kudhibiti kawi na bei za mafuta nchini EPRA Daniel Kiptoo, Katibu katika Idara ya petroli nchini Mohammed Liban na mkurugenzi wa Kampuni ya Kenya Pipeline Joe Sang kujiuzulu.
Kujiuluzu kwao kumetokana na kukamatwa na maafisa wa idara ya upelelezi wa jinai nchini DCI, kwa ushirikiano na Tume ya maadili na kupambana na ufisadi nchini EACC baada ya kutilia shaka zabuni iliyopewa kampuni binafsi ya One Petroleum Limited inayomilikwa na mfanyibiashara mashuhuri jijini Mombasa.

Wahudumu wa sekta ya bodaboda wakikabiliwa na changamoto za uhaba wa mafuta ya Petroli
Siku ya Jumanne, Waziri wa Kawi nchini Opiyo Wandanyi alifanya kikao na wakurugenzi wa kampuni za mafuta nchini na kuagiza shehena ya mafuta katika bandari ya Mombasa kurejeshwa kwani serikali haitambua shehena hiyo.
“Wahusika wa sakata hiyo walikuwa na njama ya kuongeza bei ya mafuta nchini kwa shilingi 14 zaidi kwa lita wakitumia nafasi ya vita vinavyoendelea kati ya Iran na Marekani na Israel, hiyo hatuta kubali”, alisema Wandayi.
Hatua hiyo ilikuwa inalenga pia kukwepa mpango wa serikali wa uagizaji mafuta kutoka mataifa ya miliki za kiarabu wa serikali kwa serikali yaani G to Go, akisema wahusika wa sakata ya ufisadi ni lazima wachukuliwe hatua.
Itakumbukwa kwamba rais William Ruto hivi majuzi alidokeza kwamba wahusika wote wa sakata ya ufisadi kwenye sekta ya mafuta watachukuliwa hatua, akishililia kwamba serikali haitakubali ufisadi nchini, huku akikosa kuweka wazi hatma ya maafisa hao wakuu wa serikali.
“Hawa walaghai wa mambo ya mafuta watakipata, hawaweze kuhepa kwa sababu haiwezekani katika taifa letu la Kenya watu wanaone tuko na shida ya mashariki ya kati wanakuja kukoroga shida nyengine hapa Kenya, serikali itakabiliana kikamilifu na wafisadi”, alisema Rais Ruto.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

