Uncategorized
Timu ya taifa ya wanaume ya hoki ya Kenya, Chui, yashindwa kwa mara ya pili mfululizo kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika (ACN)
Timu ya taifa ya hoki ya wanaume ya Kenya, Chui, ilipata kichapo chake cha pili mfululizo katika mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (ACN) baada ya kufungwa 3-1 na mabingwa watetezi Afrika Kusini siku ya Jumapili huko Ismailia, Misri.
Matokeo hayo yalikuja siku moja tu baada ya Kenya kupoteza kwa 2-1 dhidi ya wenyeji Misri siku ya Jumamosi.
Keenan Horne, Mustapha Cassiem, na Davis Calvin waliifungia Afrika Kusini, huku Bethuel Masambu akipachika bao pekee la kufutia machozi kwa Kenya.
Chui walianza vizuri, wakilishambulia lango la Afrika Kusini mapema na kulazimisha kosa la kiulinzi lililosababisha Samkelo Mvimbi kutolewa nje kwa rafu kali mwishoni mwa robo ya kwanza, ambayo ilimalizika bila bao.
Dakika nne tu tangu kuanza kwa robo ya pili, Horne alifunga kupitia penalti kona, na kuipa Afrika Kusini uongozi. Baada ya hapo, kasi ya Kenya ilianza kushuka baada ya Charles Ashiundu kupata adhabu ya muda kwa mwenendo usio wa kiungwana.
Cassiem aliongeza bao la pili kwa Afrika Kusini dakika ya 23 kwa shuti safi la uwanjani, na kuwapa mabingwa hao uongozi wa 2-0 hadi mapumziko.
Katika robo ya tatu, Kenya ilibadilisha mbinu na kufanikiwa kupata penalti kona dakika ya tisa, ambapo Masambu alifunga na kupunguza pengo, jambo lililowasha tena matumaini ya kurejea mchezoni.
Hata hivyo, Afrika Kusini ilijipanga upya na kuimarisha safu ya ulinzi, huku kiungo wa Sikh Union, Cliff Omari, akikosa nafasi nzuri ya kufunga akiwa karibu na goli. Dakika tatu baada ya kuanza kwa robo ya mwisho, Davis Calvin alihakikisha ushindi wa Afrika Kusini kwa kufunga kupitia penalti kona nyingine, na kufanya matokeo kuwa 3-1.
Kenya sasa itamenyana na Ghana siku ya Jumanne, wakitafuta ushindi wao wa kwanza kwenye mashindano haya, huku Afrika Kusini ikitarajiwa kukutana na Misri.
Mapema siku hiyo ya Jumapili, Ghana iliicharaza Zambia kwa mabao 5-0. Baadaye jioni, Misri ilitarajiwa kumenyana na Nigeria kabla ya mashindano kusimama kwa mapumziko siku ya Jumatatu.
Uncategorized
Mshukiwa wa mauaji kuzuiliwa rumande kwa siku 7
Mahakama ya Kilifi imeagiza kuzuiliwa rumande mshukiwa wa mauaji ya Ruth Ochieng’ mwenye umri wa miaka 60 kutoka kaunti ya Kisumu baada ya mshukiwa Evans Otieno kukamatwa katika Kanisa la Newlife Prayer Center lililoko eneo la Mavueni kaunti ya Kilifi.
Otieno alitiwa nguvuni na maafisa wa usalama alipokiri kwamba alitekeleza mauaji hayo mbele ya Mchungaji wa Kanisa hilo Ezekiel Odero, akitaka aombewe kama hatua moja wapo ya kutubu dhambi zake.
Hakimu wa Mahakama ya Kilifi Charles Obulutsa amesema Otieno atazuiliwa rumande kwa siku 7 ili kumuwezesha afisa wa polisi wa kituo cha polisi cha Seme mjini Kisumu anayechunguza kesi hiyo kufika Mahakamani.
Hakimu Obulutsa, ameeleza Mahakama kwamba wakati afisa huyo wa Polisi atakapofika katika Mahakama ya Kilifi atapewa idhini ya kumchukua mshukiwa ili afunguliwe mashtaka ya mauaji mjini Kisumu.
Awali Mahakama ilielezwa kwamba mwili wa mahehemu ulipatikana na kuthibitishwa kwamba alikuwa amenyongwa na uchunguzi zaidi ulikuwa unaendelea kabla ya mshukiwa kukamatwa katika maeneo ya Kanisa la Newlife Prayer Centre, eneo la Mavueni kaunti ya Kilifi.
Kesi hiyo itatajwa tena Februari 11 katika ili kuwakabidhi maafisa wa Polisi kutoka kaunti ya Kisumu mshtakiwa huyo.
Taarifa ya Teclar Yeri
Uncategorized
Wakenya wanaopata mshahara wa chini ya elfu 30 kuondolewa PAYE
Waziri wa Fedha nchini John Mbadi amesema serikali inalenga kuwaondolea ushuru wa PAYE wakenya wanaopata mshahara wa chini ya shilingi elfu 30 kwa mwezi huku wale wanaopata mshahara wa shilingi elfu 30 hadi laki tano wakitozwa ushuru wa asilimia 25.
Waziri Mbadi alisema hatua hiyo inalenga zaidi ya wakenya milioni 1.5 na hivi karibuni atawasilisha mswada bungeni ili pendekezo hilo liangaziwe na sheria ya ushuru ifanyiwe marekebisho kabla ya kupitishwa kwa mswada wa fedha wa mwaka wa 2026.
Waziri Mbali aliyasema hayo wakati wa kikao cha kukusanya maoni ya umma katika kaunti ya Meru ambapo alikuwa amefanya kikao cha mazungumzo na Rais William Ruto na kuafikiana kuhusu pendekezo hilo.
Waziri huyo wa fedha nchini aliongeza kwamba mswada huo pia utajumuisha pendekezo la kupunguza ushuru wa PAYE kwa asilimia 5 kwa wakenya wanaopokea mshahara wa kati ya shilingi elfu 32,050 kwa mwezi hadi shilingi laki tano, akisema punguzo hilo la asilimia 5 litasaidia wakenya kumudu gharama ya maisha.
“Tumekubaliana na Rais kwamba wananchi wenye kipato cha chini wanapaswa kupata nafuu kwenye mishahra yao kwani idadi kubwa ya wananchi wanapitia hali ngumu ya maisha na hatua hii itasaidia wakenya wengi kuwa na pesa mfukoni. Sidhani kama kuna mbunge yeyote atapinga pendekezo hilo”, alisema Mbadi.
Waziri huyo wa fedha alishikilia kwamba hatua hiyo inalenga kupunguza mzingo wa ushuru kwa wakenya wa kipato cha chini na cha kati na kuwasaidia kujikimu katika kipindi hiki cha gharama ya juu ya maisha.
Kwa sasa kikomo cha ushuru wa PAYE kinaathiri wakenya wengi wenye kupokea mshahara wa kuanzia shilingi elfu 24, akisema wataalamu wamebaini kwamba kupunguzwa kwa ushuru kutachangia matumizi ya nyumbani kuwa ya usawa na kusaidia kuimarisha uchumi unaokabiliwa na mahitaji duni.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

