Connect with us

Entertainment

#UlijanjarukaVipi! Safari ya Mpishi Nguli, Don Moses: Kutoka Kukosa Karo Hadi Kuwa Head Chef

Published

on

Katika dunia ya leo ambapo changamoto za kiuchumi zimewaacha vijana wengi wakihangaika, simulizi ya Don Moses ni mwanga wa matumaini kwa wengi.

Akiwa mgeni katika kipindi cha Janjaruka 254, kinachorushwa kila siku ya wiki kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa, Moses alisimulia safari yake ya ajabu kutoka kwa kijana aliyezuiwa na karo ya shule hadi kuwa mpishi mashuhuri hadi kuwa Head Chef aliyesimamia wapishi waliosomea fani hiyo chuoni.

Baada ya kuhitimu kidato cha nne, Moses alikuwa ameweka ndoto ya kujiunga na chuo lakini maisha yalikuwa na mpango tofauti. Mama yake alipata ajali mbaya, hali iliyolazimu familia kuhamishia raslimali kwenye matibabu badala ya karo yake ya chuo.

“Nilijua wazi kuwa singeweza kulazimisha familia ichague kati ya maisha ya mama na elimu yangu. Ilibidi nitafute njia mbadala,” anasema Moses.

Jiko la YouTube: Darasa la Ukombozi

Akiwa hana karo, lakini akiwa na shauku, Moses alianza kujifunza sanaa ya upishi kupitia video za YouTube. Binamu yake, Moses Gambo, ndiye aliyemfungulia mlango wa maarifa kwa kumtambulisha kwenye tutorials mbalimbali mtandaoni.

Ni ujuzi huo wa mtandaoni uliomfungulia milango ya ajira katika hoteli za kifahari, ambapo aliweza kupanda ngazi hadi kuwa mpishi mkuu (Head Chef) — akiongoza wapishi waliopitia vyuo vya kitaaluma. Ni mafanikio ambayo wengi hawakuyatarajia kutoka kwa kijana ambaye hakuingia darasa la kawaida, bali alikaa mbele ya skrini.

“Najua kwenye upishi kuna kupika mashendea ama kupika chakula kibaya ila sijawahi kufeli. Siku zote mimi ni makini na ratio ya viungo. Ndiyo silaha yangu,” anasema kwa kujiamini.

Mwaka wa Mageuzi: 2020

Kama ilivyokuwa kwa wengi, mwaka wa janga la COVID-19 – 2020 – ndiyo ulikuwa mwaka wa mabadiliko makubwa kwa Moses. Akiwa na muda mwingi na motisha mpya, alianza kupika kibiashara, akihudumia watu waliokuwa majumbani.

“Kabula ya hapo, nilikuwa napika kwa kujifurahisha tu. Lakini corona ilinifungua macho. Nikaanza kuona kuwa mapishi ni biashara yenye nguvu,” anasema Moses.

Karo Iliyogeuka Mtaji

Kipindi fulani baadaye, Moses alipata nafasi ya kujiunga na chuo hatimaye. Lakini kwa mshangao wa wengi, alikataa ofa hiyo kwa hiari na kuomba fedha hizo zitumike kupanua biashara yake ya upishi.

“Nitamudu gharama ya chuo siku moja. Kwa sasa, najenga misingi. Muda wa kusoma utafika,” anasema.

💡 Ushauri kwa Vijana: Anza na Kile Kilicho Mkono Wako

Don Moses sasa ni sauti ya matumaini kwa vijana wengi wanaohisi kuwa elimu ya juu au mtaji mkubwa ndio tiketi pekee ya mafanikio. Anasisitiza umuhimu wa kuanza na huduma, si lazima mtaji.

“Kama huna kazi wala mtaji, toa huduma kwanza. Ukiwa na bidii na ubunifu, malipo yatafuata,” anashauri.

Leo hii, sehemu kubwa ya mapato ya Moses huingia moja kwa moja kwenye ununuzi wa vifaa bora vya upishi, huku akiendeleza ndoto yake ya kuwa mmoja wa wapishi wakubwa zaidi nchini Kenya.

Continue Reading
1 Comment

1 Comment

  1. Austine oscar

    June 6, 2025 at 10:12 pm

    Tumeona kazi zako Boss kupitia mm mkufunzi wako heko na kupa cha zaidi nakuombea heri na mafanikio mema na uishi maisha marefu ju isingekuwa ww singekuwa mahali nilipo nashkuru Mungu Sana kwa umbali umenitoa ningetamani pia mm nifike mahali upo na Niko na Imani kubwa Sana hata ww mwenyewe walijuwa hilo ila IPO siku 🧨🙏

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Entertainment

Arsenal Ikishinda Kombe Nitampa Main Man Rio Gari na Dadangu – Shuga Boy

Published

on

Mjadala mkali umeibuka katika kipindi cha COCO Asubuhi baada ya Shuga Boy, shabiki wa Manchester United, kuweka dau zito na la kushangaza dhidi ya Main Man Rio ambaye ni shabiki wa Arsenal.

Akizungumza kwenye kipindi cha COCO Asubuhi, kinachoendeshwa na Tatu Sure—inayojumuisha Shuga Boy mwenyewe, Main Man Rio na Solomon Zully—Shuga Boy alifunguka, akidai kuwa Arsenal hawana uwezo wa kubeba hata kombe moja msimu huu licha ya matarajio makubwa kutoka kwa mashabiki wao.

Kwa mujibu wa Shuga Boy, mashabiki wa Arsenal wamekuwa wakijipa matumaini makubwa ya kutwaa hadi vikombe vinne, lakini hali halisi uwanjani haioneshi dalili hizo. Alienda mbali zaidi na kuweka dau la kipekee kwa Main Man Rio, ambaye ni shabiki mkubwa wa Arsenal.

“Nilimwambia Main Man Rio, wakibeba kombe nitampa gari yangu. Sasa naongeza dau—wakishinda kikombe msimu huu, nitampa gari yangu pamoja na dadangu,” alisema Shuga Boy kwa msisitizo, kauli iliyozua kicheko na mjadala mkali studio.

Kauli hiyo imekuja katika kipindi ambacho Arsenal wamekuwa wakionyesha ushindani mkubwa chini ya kocha Mikel Arteta, wakijijenga kama moja ya timu zinazowania ubingwa wa Premier League. Licha ya maendeleo hayo, ukosefu wa vikombe katika misimu mingi bado unawapa wapinzani wao nafasi ya kuwabeza.

Kwa upande mwingine, Manchester United nao wanapitia kipindi cha mabadiliko, wakijaribu kurejea kwenye ubora wao wa zamani waliouonyesha enzi za Sir Alex Ferguson. Licha ya changamoto, bado wana historia nzito ya mafanikio, jambo linalowapa mashabiki wao kujiamini wanapojadili soka la Uingereza.

Usiku wa leo, macho ya mashabiki yataelekezwa kwenye mchezo wa ligi kati ya Manchester United dhidi ya Leeds United—mchezo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkali, huku Shuga Boy akitumaini timu yake itapata ushindi na kuendeleza presha kwa wapinzani wao.

Wakati mabishano yakiendelea mitandaoni na kwenye studio za redio, swali kubwa linabaki: Je, Arsenal wataweza kuwanyamazisha wakosoaji wao kwa kubeba angalau kombe moja msimu huu, au kauli ya Shuga Boy itageuka kuwa unabii?

Continue Reading

Entertainment

Watoe Nyingi… Mimi Natoa Moja! Kauli ya King Kiba Yazua Mjadala

Published

on

Staa wa Bongo Fleva Alikiba ameibua mjadala mzito kufuatia kauli yake aliyoitoa baada ya kufanya show kubwa na yenye mafanikio jijini Mwanza, nchini Tanzania.

Baada ya kupanda jukwaani na kuonesha kiwango chake cha juu cha uimbaji na burudani, King Kiba aliacha mashabiki wakizungumza zaidi si tu kuhusu show yake, bali pia kauli yake iliyokuja mwishoni mwa performance yake. Akiwa mbele ya umati mkubwa wa mashabiki, alisema kwa kujiamini:

“Watatoa ngoma nyingine na nyingine, na nyingine, na nyingine, na nyingine… halafu mimi natoa nyingine, moja tu.”

Kauli hiyo imezua tafsiri mbalimbali miongoni mwa mashabiki na wadau wa muziki, wengi wakiona kuwa ni ujumbe unaolenga tofauti iliyopo kati ya wasanii wanaotoa kazi nyingi kwa wakati mfupi na wale wanaochagua kutoa kazi chache lakini zenye ubora wa hali ya juu. Kwa muktadha huo, Alikiba anaonekana kusimama katika kundi la wasanii wanaoamini katika ubora kuliko wingi.

Kwa muda mrefu sasa, Kiba amekuwa akijulikana kwa mtindo wake wa utoaji wa muziki usio wa haraka, lakini unaolenga ubora wa juu na maisha marefu ya kazi zake sokoni. Hii ni tofauti na mwenendo wa sasa wa tasnia ya muziki wa kidigitali ambapo baadhi ya wasanii huchagua kutoa nyimbo mfululizo ili kubaki juu ya chati na kwenye algorithms za streaming platforms.

Kauli yake pia imekuja katika kipindi ambacho wimbo wake mpya Finale, aliomshirikisha Bien, unaendelea kufanya vizuri kwenye majukwaa ya kidigitali. Video ya wimbo huo imekuwa ikipata watazamaji wengi na maoni chanya kutoka kwa mashabiki wa Afrika Mashariki na kwingineko, hali inayoongeza uzito wa ujumbe wake kuwa kazi moja bora inaweza kuwa na athari kubwa kuliko nyingi zisizo na nguvu sawa.

Baadhi ya wachanganuzi wanasema kijembe hicho kimemlenga mpinzani wake wa karibu Diamond Platnumz ambaye ameachia nyimbo mbili (Happy na Joy) kwenye kipindi kifupi ambacho King Kiba kaachia wimbo mmoja unaofanya vizuri zaidi ya nyimbo za Simba.

Hata hivyo, mjadala unaoibuliwa na kauli hiyo una pande mbili. Wapo wanaounga mkono msimamo wa Kiba wakisema ubora ndiyo unaojenga legacy ya msanii. Lakini pia wapo wanaoamini kuwa katika ushindani wa sasa, consistency ya kutoa nyimbo mara kwa mara ni muhimu ili kubaki relevant kwenye soko lenye ushindani mkubwa.

Kwa mtazamo wa kina, kauli ya Alikiba si tu maneno ya jukwaani bali ni tafakari ya mkakati wake wa muziki na namna anavyoiona tasnia kwa ujumla. Inaibua swali muhimu kwa wasanii na mashabiki pia—je, thamani ya msanii ipo kwenye wingi wa kazi anazotoa, au kwenye ubora na uimara wa kazi chache anazoachia?

Hadi sasa, jambo moja liko wazi—kauli hiyo imefanikiwa kuamsha mjadala mkubwa, na kwa mtindo wa King Kiba, huenda hata hilo lenyewe ni sehemu ya mchezo wake wa kisanii.

Continue Reading

Trending