Sports
Arsenal Karibu Kufikia Makubaliano Mapya na Beki Gabriel
Klabu ya Arsenal ipo katika hatua za mwisho za mazungumzo na beki wao wa kati, Gabriel Magalhães, kuhusu mkataba mpya.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 raia wa Brazil, bado ana mkataba unaoendelea hadi mwaka 2027, lakini klabu hiyo imekuwa ikijadiliana naye kuhusu masharti mapya ya kuboresha mkataba huo.
Ikumbukwe kuwa mazungumzo hayo yamepiga hatua kubwa, na makubaliano yanaelekea kukamilika hivi karibuni.
Taarifa hiyo inakuja kama faraja kubwa kwa The Gunners wakati wanajiandaa kwa msimu wa uhamisho wa majira ya joto, ambapo wanatarajiwa kufanya usajili muhimu ili kuimarisha kikosi.
Gabriel amekuwa mchezaji wa msingi chini ya kocha Mikel Arteta, ingawa msimu wake ulimalizika mapema mwezi Aprili kufuatia majeraha ya paja yaliyomlazimu kufanyiwa upasuaji.
Hata hivyo, beki huyo anatarajiwa kuwa fiti kabla ya msimu mpya kuanza.
Katika msimu uliomalizika wa mwaka 2024/2025, Gabriel alifunga magoli matano katika mashindano yote akiwa na Arsenal.
Sports
Bingwa wa Afrika mbio za mita 100 mkenya Ferdinand Omanyala azidi kuthibitisha ubora wake mbio Botswana Golden Grand Prix akimaliza wa pili na sekunde 9.95
Mwanariadha mwenye kasi zaidi barani Afrika, Ferdinand Omanyala, amethibitisha kurejea kwake katika kiwango cha juu kwa mbio za kuvutia za sekunde 9.95 kwenye mashindano ya Botswana Golden Grand Prix yaliyofanyika Jumapili, Aprili 26 jijini Gaborone.
Katika fainali ya wanaume ya mita 100 iliyokuwa na ushindani mkali, Mkanada Jerome Blake alishinda kwa sekunde 9.93, huku mwenzake Andre De Grasse na Omanyala wakitumia sekunde 9.95 katika ushindani wa karibu sana. Ingawa awali ilionekana kama nafasi ya pili iligawanywa, matokeo rasmi yalimweka Omanyala katika nafasi ya tatu kwa tofauti ndogo sana.
Licha ya nafasi hiyo, matokeo hayo yaliashiria mbio ya tatu mfululizo kwa Omanyala kukimbia chini ya sekunde 10 ndani ya siku saba tu, na kukamilisha kurejea kwa nguvu kwa mshikiliaji wa rekodi ya Afrika. Mkenya huyo alianza mfululizo huo kwa ushindi wa sekunde 9.98 katika Addis Ababa Grand Prix Aprili 18, kabla ya kuwapa mashabiki wa nyumbani burudani kwa ushindi wa sekunde 9.96 katika mashindano ya Kip Keino Classic jijini Nairobi Aprili 24.
Mfululizo huu wa matokeo unaashiria kurejea kwa nguvu kwa Omanyala baada ya msimu mgumu wa 2025 uliokumbwa na majeraha na kutokuwepo kwa uthabiti, ambapo alishindwa kushuka chini ya kiwango muhimu cha sekunde 10.
Sasa macho yanaelekezwa kwenye World Athletics Relays zitakazofanyika Mei 2–3, pia jijini Gaborone, ambapo Omanyala anatarajiwa kuiongoza timu ya Kenya katika mbio za kupokezana vijiti za 4x100m. Mashindano hayo yatakuwa hatua muhimu kuelekea kufuzu kwa michuano ya Ultimate Championship itakayofunga msimu.
Kwa kuzingatia mashindano yajayo ya Continental Tour Gold na michuano mikubwa kama Michezo ya Jumuiya ya Madola itakayofanyika Glasgow, kurejea huku kwa kasi kwa Omanyala kumekuja wakati muafaka anapojenga upya kasi yake dhidi ya wanariadha bora duniani.

